Makardinali wanamshukuru Baba Mtakatifu Benedikto XVI
Kardinali Angelo Sodano, Dekano wa Makardinali kwa niaba ya Makardinali wote, Alhamisi,
tarehe 28 Februari 2013 amemshukuru na kumpongeza Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi
na sita kwa ushuhuda wa huduma za kitume, kwa ajili ya mafao ya Kanisa na ulimwengu
kwa ujumla.
Anamshukuru Baba Mtakatifu kwa maneno na wosia aliowaachia mara
baada ya kuhitimisha mafungo ya kiroho, pale alipowaambia kwamba, wametekeleza wajibu
wao kwa weledi, upendo na imani thabiti katika kumsaidia kutekeleza utume wake kama
Khalifa wa Mtakatifu Petro.
Makardinali wanamshukuru kwa ushuhuda wa maisha
na utume katika kipindi chote cha miaka minane ya uongozi wake kama Khalifa wa Mtakatifu
Petro. Lakini, kwa namna ya pekee, wakati huu anapong'atuka kutoka madarakani, ili
kutoa nafasi kwa Kiongozi mwingine, kuliendeleza Kanisa. Kuna mengi ambayo wamejifunza
kutoka kwake kama walivyokuwa wale wafuasi wa Emmaus walipokuwa wanatembea na Kristo
wakibadilishana mawazo kuhusu tukio kubwa katika maisha yao!