2013-02-28 11:27:46

Baadhi ya waamini wa Kanisa Katoliki China wanamshukuru Baba Mtakatifu Benedikto XVI


Baadhi ya Waamini wa Kanisa Katoliki nchini China wamemwandikia Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, barua ya shukrani na kumwomba katika sala na tafakari zake asiwasahau katika hija ya maisha yao ya kiiimani. Wanasema, walitamani kuona siku moja, anatembelea China ili kuwaimarisha ndugu zake katika imani wanaoendelea kuteseka kwa ajili ya Kanisa na Khalifa wa Mtakatifu Petro.

Waamini nchini China wanatambua na kuthamini mchango wake uliopania kuwaimarisha katika imani, matumaini na mapendo na kwamba, alionesha upendo mkubwa kwa wananchi wa China tangu alipochaguliwa kuliongoza Kanisa. Amekuwa ni kielelezo cha majadiliano ya kina miongoni mwa wananchi wa China ili kujenga na kuimarisha umoja na mshikamano.

Katika shida na mahangaiko ya wananchi wa China, ameonesha mshikamano na upendo wa kibaba! Wanamkumbuka kwa kuruhusu kuchapishwa kwa Misale ya Waamini kwa Lugha ya Kichina ambao kwa sasa ni msaada mkubwa katika Maadhimisho ya Mafumbo ya Kanisa. Wanaikumbuka ile barua aliyowaandikia kuwatia moyo kusonga mbele katika maisha na utume wao ndani ya Kanisa.







All the contents on this site are copyrighted ©.