Mshikamano wa: haki, amani na upendo kwa Waamini wanaoishi katika Nchi Takatifu
Maadhimisho ya Mwaka wa Imani sanjari na kumbu kumbu ya Jubilee ya miaka 50 ya Mtaguso
Mkuu wa Pili wa Vatican ni mwaliko na changamoto kwa waamini na watu wote wenye mapenzi
mema kuonesha mshikamano wa upendo kwa waamini wanaoishi katika Nchi Takatifu, ambao
miaka nenda miaka rudi, wameendelea kulinda na kutunza maeneo ya imani. Nchi Takatifu
inaonesha ile kiu ya haki, utu na heshima, ili kwa pamoja Jamii iweze kuwajibika kuwalinda
na kuwatunza wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii, ili kwa pamoja waweze kusimama
kidete kutetea mafao ya wengi pamoja na kuwajibika barabara
Baraza la Kipapa
kwa ajili ya Makanisa ya Mashariki katika barua yake kwa Mabaraza ya Maaskofu Katoliki,
sehemu mbali mbali za dunia linasema, kuna watu wanaendelea kuogelea katika dimbwi
la umaskini kwa kukosa mahitaji msingi ya maisha kutokana na ubinafsi uliokithiri.
Kila mtu anapaswa kuheshimiwa na kuthaminiwa utu wake, daima Jamii ikijikita kutafuta
mafao ya wengi pamoja na amani ya kudumu. Binadamu anatambua kwamba, hatima ya maisha
yake hapa duniani ni kutaka kuungana na Mwenyezi Mungu. Hii ndiyo imani inayoliongoza
Kanisa, kwa kujitahidi kutafuta umoja na mshikamano na Kristo.
Kardinali Leonardo
Sandri, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa kwa ajili ya Makanisa ya Mashariki anasema
kwamba, kunako mwaka 1964, Papa Paulo wa sita katika hija yake ya kichungaji katika
Nchi Takatifu; baadaye Mtumishi wa Mungu Yohane Paulo wa pili, alisema kwamba, hija
yake ambayo ilikuwa ni zawadi kubwa katika Maadhimisho ya Jubilee kuu ya Miaka 2000
ya Ukristo ilipania kujenga na kuimarisha umoja, udugu na amani, kwa kujikita katika
majadiliano ya kidini na kiekumene miongoni mwa Waamini wanaoishi katika Nchi Takatifu,
ili hatimaye, kuweza kupata suluhu ya migogoro na kinzani zinazojitokeza katika Nchi
Takatifu.
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, mara baada ya kurejea
mjini Vatican baada ya hija yake ya kichungaji aliwaombea Wakristo wanaoishi Mashariki
ya kati, ili kwa nguvu ya Roho Mtakatifu waweze kudumu katika uaminifu. Ili kuonesha
ukaribu wake na Wakristo wanaoishi Mashariki ya Kati, ambao wanakumbana na madhulumu
pamoja na changamoto mbali mbali, amewadhaminisha kuandika tafakari ya Ibada ya Njia
ya Msalaba, Ijumaa Kuu, kuzunguka Magofu ya Colosseo mjini Roma. Sehemu hii inahitaji
umoja na mshikamano katika fadhila ya imani.
Waamini wanachangamotishwa kuonesha
moyo wa mshikamano kwa kuchangia kwa hali na mali utunzaji wa maeneo matakatifu, tukio
ambalo linafanywa na Mama Kanisa, katika Ibada ya Ijumaa kuu. Msaada huu unalenga
kukoleza mchakato wa maendeleo endelevu unaofanywa na Kanisa mahalia katika sekta
mbali mbali za maisha. Mchango huu pia ni chanzo cha pato kwa Familia nyingi zinazokabiliana
na hali ngumu ya maisha, ili kuweza kuwahudumia: wagonjwa, wazee, watoto yatima na
walemavu.
Mshikamano kutoka kwa waamini sehemu mbali mbali za dunia, imekuwa
pia ni fursa ya kutoa ajira kwa vijana ili kuwajengea matumaini ya leo na kesho iliyo
bora zaidi. Lengo la mchango huu ni kujenga na kuimarisha uhuru wa kidini; majadiliano
ya kidini na kiekumene pamoja na kuwasaidia Wakristo ili waweze kuendelea kubaki katika
maeneo yao badala ya kukimbilia sehemu nyingine. Hapa ni kielelezo cha mateso na mahangaiko
ya binadamu, lakini mahali ambapo pia Mwenyezi Mungu anatukuzwa na mwanadamu anatakatifuzwa.
Baraza la Kipapa linawahimiza waamini kuchagia kwa hali na mali katika kuenzi shughuli
za imani na maendeleo Nchi Takatifu.