2013-02-26 08:13:29

Makardinali kuamua tarehe ya uchaguzi wa Papa mpya!


Padre Federico Lombardi msemaji mkuu wa Vatican, akizungumza na waandishi wa habari mjini Vatican, siku ya Jumatatu tarehe 25 Februari, 2013 anabainisha kwamba, mkutano wa Dekania ya Makardinali wenye dhamana ya kumchagua Khalifa wa Mtakatifu Petro katika kikao chake cha kwanza, utataja tarehe maalum ya kufanya uchaguzi wa Papa mpya. Ili kuwa na uhakika wa tarehe rasmi ya uchaguzi wa Papa, kuna haja kwa waamini na watu wote wenye mapenzi mema, kuendelea kuvuta subira hadi tarehe za mwanzo mwanzo za Mwezi Machi, 2013.

Makardinali wenye dhamana ya kupiga na kupigiwa kura wanapaswa kushiriki katika mkutano wa kumchagua Khalifa wa Mtakatifu Petro. Lakini pia wanaweza kutohudhuria mkutano huu kwa sababu mbali mbali kama vile ugonjwa. Kwa Kardinali ambaye anaamua kwa utashi wake mwenyewe kutohudhuria mkutano, hataruhusiwa tena kushiriki katika mkutano huo hata kama atakuwa amebadilisha uamuzi wake.

Wataalam wa sheria za Kanisa bado wanaendelea kukuna vichwa ili kutafuta jina ambalo Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita ataitwa mara baada ya kung’atuka rasmi kutoka madarakani; jina ambalo litaendelea kuonesha heshima na dhamana aliyokuwa nayo kama Khalifa wa Mtakatifu Petro. Papa ndiye mwenye dhamana ya kutomruhusu Kardinali yoyote yule kuingia na kushiriki mkutano wa Makardinali, pale inapoonekana kwamba, inafaa na kwa ajili ya mafao ya Kanisa.

Wakati wote wa mikutano ya Makardinali kama njia ya kufahamiana, kutathmini na kupembua hali ya Kanisa, changamoto na matarajio ya Watu wa Mungu, Makardinali hawataruhusiwa kuhojiwa wala kuzungumza na Waandishi wa Habari wakati wote wa mikutano yao kwani wanafungwa na siri ya mchakato mzima wa uchaguzi wa Papa Mpya.

Dekano wa Makardinali ambaye kwa sasa ni Kardinali Angelo Sodano ataamua tarehe na muda kwa Makardinali kuweza kukutana na kuendesha mikutano yao. Ndiye pia mwenye dhamana ya kufahamu ni Makardinali wangapi ambao wako tayari mjini Roma na wanaweza kuhudhuria mkutano wa Dekania ya Makardinali na wale ambao bado hawajawasili.








All the contents on this site are copyrighted ©.