2013-02-25 12:13:19

Wanazuoni wanaomboleza kifo cha Kardinali Julien Ries, bingwa wa elimu ya binadamu mintarafu maisha ya kiroho!


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, katika salam zake za rambi rambi kutokana na kifo cha Kardinali Julien Ries kwa Askofu Guy Harpigny wa Jimbo Katoliki la Tournai, Ubelgiji anasema, amepokea habari za msiba huu kwa masikitiko makubwa.

Anamwombea Marehemu kardinali Ries ili Mwenyezi Mungu aweze kumwangazia mwanga wa milele mja wake katika imani, aliyelihudumia Kanisa kwa mafundisho na tafiti zake mintarafu historia ya dini; sehemu ambayo alionesha umahiri mkubwa. Kardinali Ries ametolea ushuhuda wa imani yake kwa kukazia moyo wa majadiliano.

Kardinali Julien Ries, Jaalim mstaafu wa historia ya dini Chuo Kikuu cha Kikatoliki cha Louvain, Ubelgiji, tarehe 23 Februari 2013 amefariki dunia akiwa na umri wa miaka 93. Alizaliwa tarehe 14 Aprili 1920. Baada ya masomo na majiundo yake ya kikasisi akapadrishwa kunako tarehe 12 Agosti 1945. Katika maisha yake alijikita zaidi katika tafiti za kisayansi kiasi kwamba, wanazuoni wengi walimtambua kuwa ni kati ya waasisi uelewa wa binadamu mintarafu maisha yake ya kiroho.

Alikuwa ni mwandishi mahiri, hadi anaitupa mkono dunia alikwisha andika vitabu 650 vilivyotafsiriwa katika lugha kumi na moja za kimataifa. Kwa miaka mingi alifundisha katika Chuo Kikuu cha Kikatoliki cha Lovanio. Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, akamteua kuwa Kardinali kunako mwaka 2012 kwa kutambua mchango wake mkubwa katika tafiti za kisayansi.







All the contents on this site are copyrighted ©.