Rais Jakaya Mrisho Kikwete wa Tanzania Februari 24, 2013 aliungana na mamia ya wananchi
wa Uganda katika mazishi ya Mzee Amos Kaguta (97), Baba wa Rais Yoweri Museveni wa
Uganda, yaliyofanyika katika kijiji cha Rwakitura, Magharibi ya Uganda. Rais Kikwete
aliwasili katika mazishi hayo akitokea Addis Ababa, mji Mkuu wa Ethiopia alipohudhuria
Mkutano wa viongozi wa kutafuta amani ya kudumu katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya
Kongo.
Akitoa salamu zake za rambirambi katika msiba huo, Rais Kikwete alisema
kuwa Watanzania wapo pamoja na ndugu zao wa Uganda wakati huu wa majonzi na kusema
kuwa yeye binafsi anampa pole Rais Museveni na familia yake na kumtaka awe na moyo
wa subira katika kipindi hichi na kumuombea marehemu.
Rais Museveni alimshukuru
Rais Kikwete kwa kufika katika msiba huo ambapo alisema kuwa Marehemu Mzee Amos atakumbukwa
kwa kuithamini elimu ambapo aliwapeleka watoto wake shule na kwa kufanya mabadiliko
ambapo alikubali kufuata njia bora za ufugaji wenye tija jambo ambalo ni gumu kwa
wazee wengi wenye umri wake (97).
Rais Museveni alitumia fursa hiyo kuwaasa
vijana kuwatunza vyema wazazi wao ili waishi muda mrefu na kulaani tabia ya baadhi
ya vijana kuishi kwa kutegemea mali za wazazi wao badala ya kuzalisha mali yao wenyewe
akiongeza kuwa wazee wana hazina kubwa ya maarifa kutokana na kukumbana na changamoto
nyingi katika maisha yao. Marehemu Mzee Amos Kaguta alizaliwa mwaka 1916 katika kijiji
cha Kabahambi, Kikoni Ntungamo nchini Uganda.