2013-02-25 12:11:48

Vijana watunzeni wazazi, chakarikeni kutafuta maisha, kamwe msitegemee urithi tu!


Rais Jakaya Mrisho Kikwete wa Tanzania Februari 24, 2013 aliungana na mamia ya wananchi wa Uganda katika mazishi ya Mzee Amos Kaguta (97), Baba wa Rais Yoweri Museveni wa Uganda, yaliyofanyika katika kijiji cha Rwakitura, Magharibi ya Uganda. Rais Kikwete aliwasili katika mazishi hayo akitokea Addis Ababa, mji Mkuu wa Ethiopia alipohudhuria Mkutano wa viongozi wa kutafuta amani ya kudumu katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

Akitoa salamu zake za rambirambi katika msiba huo, Rais Kikwete alisema kuwa Watanzania wapo pamoja na ndugu zao wa Uganda wakati huu wa majonzi na kusema kuwa yeye binafsi anampa pole Rais Museveni na familia yake na kumtaka awe na moyo wa subira katika kipindi hichi na kumuombea marehemu.

Rais Museveni alimshukuru Rais Kikwete kwa kufika katika msiba huo ambapo alisema kuwa Marehemu Mzee Amos atakumbukwa kwa kuithamini elimu ambapo aliwapeleka watoto wake shule na kwa kufanya mabadiliko ambapo alikubali kufuata njia bora za ufugaji wenye tija jambo ambalo ni gumu kwa wazee wengi wenye umri wake (97).

Rais Museveni alitumia fursa hiyo kuwaasa vijana kuwatunza vyema wazazi wao ili waishi muda mrefu na kulaani tabia ya baadhi ya vijana kuishi kwa kutegemea mali za wazazi wao badala ya kuzalisha mali yao wenyewe akiongeza kuwa wazee wana hazina kubwa ya maarifa kutokana na kukumbana na changamoto nyingi katika maisha yao. Marehemu Mzee Amos Kaguta alizaliwa mwaka 1916 katika kijiji cha Kabahambi, Kikoni Ntungamo nchini Uganda.








All the contents on this site are copyrighted ©.