Serikali ya Tanzania inatafuta mchawi wa matokeo mabaya ya mtihani wa Kidato cha IV
Waziri mkuu Mizengo Pinda ameunda Tume maalum itakayofanya uchunguzi wa matokeo ya
mtihani wa kidato cha nne ambayo yalitangazwa na Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi,
Dk. Shukuru Kawambwa Februari 18, mwaka huu.
Katika matokeo hayo yaliyotangazwa
Jumatatu, tarehe 18 Februari 2013 asilimia 60 ya wanafunzi waliofanya mtihani wa kidato
cha nne Oktoba, 2012 walifeli.
Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu, Bw. Peniel
Lyimo amesema Tume hiyo ambayo inatarajiwa kuanza kazi wakati wowote, inajumuisha
wadau kutoka Chama cha Wamiliki wa Shule na Vyuo Binafsi (Tanzania Association of
Managers and Owners of Non-Government Schools/Colleges (TAMONGSCO), Taasisi za Dini
zinazotoa huduma ya elimu, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na Asasi zisizo za Kiserikali
(NGOs) zinazoshughulikia masuala ya elimu.
Wadau wengine watatoka Chama cha
Walimu Tanzania (CWT), Kamati ya Bunge ya Huduma za Jamii na Umoja wa Wakuu wa Shule
za Sekondari Tanzania (TAHOSSA).
Amesema Serikali inawaomba wadau wa elimu,
wazazi, walezi na wananchi wote kwa ujumla watoe ushirikiano kwa Tume ili iweze kufanya
kazi yake kwa ufanisi.