2013-02-19 08:43:35

Hali ni tete Zanzibar! Kuna ubaguzi na unyanyasaji wa kidini!


Kutokana na mfululizo wa matukio ya uchomaji moto wa Makanisa, madhulumu na hatimaye mauaji ya viongozi wa Kanisa, sasa ni uhakika na wala hakuna siri tena kwamba, kuna madhulumu ya kidini Zanzibar na Tanzania kwa ujumla. Watu wanaishi kwa vitisho na hofu kutokana na imani yao, kiasi kwamba, ule uhuru wa kuabudu kwa sasa uko mashakani. RealAudioMP3

Huu ni udhaifu mkubwa ambao unaoneshwa na Serikali ya Tanzania kwa wakati huu, hata baada ya kusherehekea Jubilee ya Miaka 50 ya Uhuru wa bendera.

Hayo yamesemwa na Askofu Damian Dallu wa Jimbo Katoliki Geita, Tanzania wakati wa mahojiano maalum na Radio Vatican. Anasema, jaribio la mauaji ya Padre Ambrose Mkenda ni kielelezo cha wazi kabisa cha kinzani na choko choko za kidini. Hili ni tukio ambalo lilipangwa na alama za nyakati zinabainisha hayo kutokana na kuzagaa kwa vipeperushi, CD na DVD zenye kashfa na maneno ya uchochezi dhidi ya Wakristo.

Hatua inayofuata kwa sasa mauaji ya viongozi wa Kanisa na dalili za utekelezaji wa mikakati hii zinaanza kujionesha. Watanzania wakumbuke kwamba, amani ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu, inayomwajibisha pia binadamu. Askofu Dallu anawahimiza Wakristo, Waislam na Watanzania wote wenye mapenzi mema kuendelea kushikamana kwa dhati kulinda na kutetea: haki, amani, upendo na mshikamano wa kitaifa; vikundi vinavyotaka kuvuruga amani ni watu wachache sana, ikilinganishwa na umati mkubwa wa watanzania wanaotaka kuendeleza mshikamano pamoja na kuheshimiana.

Kwa Wakristo hiki ni kipindi cha ushuhuda wa imani. Maaskofu Katoliki wamepokea kwa mshtuko mkubwa mauaji ya Padre Evaristi Mushi wa Jimbo Katoliki Zanzibar. Ni mauaji ya kikatili yaliyofanywa wakati anakwenda kutekeleza wajibu na utume wake kwa kuadhimisha Mafumbo ya Kanisa, ili kuombea: upendo, haki na amani. Kwa hakika, Zanzibar kuna unyanyasaji na ubaguzi wa kidini. Vikundi vinavyochochea chuki, uhasama na machafuko ya kidini vinajulikana, lakini Serikali inaendelea kuwafumbia macho.

Askofu Damiani Dallu anasema, Kanisa halitashangaa kuona kwamba, matukio kama haya ya madhulumu na mauaji ya viongozi wa Kanisa yatafuata. Lakini jambo la msingi kwa watanzania na watu wote wenye mapenzi mema kukumbuka ni kwamba, vita haina macho! Kila mtu ajifunge kibwebwe kudumisha misingi ya: haki, amani, umoja na mshikamano wa kitaifa.

Wasikubali kutumiwa na baadhi ya watu kuleta choko choko na ubaguzi wa kidini. Wananchi wajitahidi kusoma alama za nyakati, ili kuwachagua viongozi watakaotetea mafao ya wengi, umoja na mshikamano wa kitaifa!







All the contents on this site are copyrighted ©.