2013-02-18 13:54:10

Watu wasiokuwa na makazi Msumbiji wananyemelewa pia na ugonjwa wa Kipindu pindu!


Hofu imetanda Kaskazini mwa Msumbiji, kutokana na kulipuka kwa ugonjwa wa Kipindu pindu na kwamba, hadi sasa kuna watu zaidi ya mia tatu ambao wamekumbwa na ugonjwa huo, katika eneo la Capo Delgado. Taarifa zinasema, Pemba ina idadi kubwa ya wagonjwa wa Kipindu pindu.

Hii ni kutokana na mazingira machafu pamoja na athari za mafuriko yaliyopelekea kubomoka kwa vyoo vingi katika maeneo yaliyokumbwa mafuriko, kadiri ya taarifa zilizotolewa na Bibi Lidia Chongo, afisa mwandamizi wa Afya nchini Msumbiji. Kuna vituo vitano vilivyotengwa ili kutoa huduma kwa wagonjwa wa Kipindu pindu nchini Msumbiji. Kuna idadi kubwa ya wananchi wa Msumbiji ambao makazi yao yalibomolewa kutokana na mafuriko yaliyotokea kwenye Mto Lipopo hivi karibuni.

Mashirika ya Misaada ya Umoja wa Mataifa, yanaomba kiasi cha dolla za Kimarekani Millioni 30.6 ili kuwahudumia waathirika wa mafuriko nchini Msumbiji pamoja na kuanza mchakato wa ujenzi wa nyumba na miundo mbinu iliyoharibiwa kutokana na mafuriko hayo.







All the contents on this site are copyrighted ©.