Wizara ya ujenzi inavyopania kuboresha miundo mbinu ya barabara Tanzania
Waziri wa Ujenzi Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli (Mb), Tarehe 15 Februari 2013
amezindua Baraza la Wafanyakazi wa Wizara ya Ujenzi ambalo linakutana kwa siku mbili
mjini Morogoro. Wakati akiongea katika uzinduzi wa Baraza hilo linalojumuisha wajumbe
kutoka katika taasisi zote zilizo chini ya Wizara ya Ujenzi, Mheshimiwa Magufuli amewapongeza
watendaji wakuu wa wizara na taasisi zake kwa namna wanavyosimamia utekelezaji wa
majukumu yao kwa ufanisi. “Mafanikio yanayoonekana kupatikana kwa upande wa wizara
yetu ni matokeo ya usimamizi wenu mzuri” alielezea Waziri Magufuli na kuwataka kutorudi
nyuma kwani hiyo ni dhamana waliyopewa na Taifa. Akizungumzia changamoto zilizopo,
Waziri Magufuli alisisitiza kukerwa kwa kuendelea kujitokeza vitendo vya rushwa katika
vituo vya mizani na kwenye vivuko. Mhe. Magufuli amezipongeza hatua zilizokwisha
kuchukuliwa na Mtendaji Mkuu wa Tanroads kwa kutangaza ajira za wafanyakazi wa vituo
vya mizani na amemtaka kukamilisha mapema ajira za Wahandisi watakaosimamia vituo
hivyo. “Hatua hizi tuzimechukua baada ya kubaini kuwa karibu asilimia themanini ya
watendaji waliopo katika vituo vya mizani ni wala rushwa” alibainisha Mheshimiwa Waziri
Magufuli. Kwa upande mwingine Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA) nao umepewa
siku sitini ili kuanza zoezi la ukatishaji tiketi za elektoniki hasa katika kivuko
cha Kuvukoni jijini Dar es Salaam. Waziri Magufuli alifichua baadhi ya mbinu zinazotumiwa
na watendaji wasio waaminifu katika vivuko hivyo, kuwa ni pamoja na kujichapishia
tiketi kwa siri na wakati mwingine kutochana tiketi wanazozipokea kutoka kwa abiria
kwa lengo la kuziuza tena. Waziri Magufuli hata hivyo amepongeza zoezi la kukamata
magari ya Serikali yanayotumia namba za binafsi kinyume na sheria. “Tayari hadi sasa
jumla ya magari 1,830 tayari yamekamatwa na kusajiliwa kwa namba za Serikali” alifafanua
Mheshimiwa Magufuli.. Wakati huo huo Waziri wa Magufuli pia amekizundua Kitabu
cha Mwongozo wa Usanifu wa Barabara. Kitabu hicho kitatumiwa katika utekelezaji wa
shughuli za ujenzi na matengenezo ya barabara hapa nchini. Wakati akizindua kitabu
hicho Mheshimiwa Waziri amewapongeza Mameneja wa Tanroads wa mikoa ya Dodoma na Morogoro
kwa ubunifu ambao wameuonyesha kwa kutumia fedha wanazotengewa katika bajeti zao.
Alielezea kufurahishwa na kazi za upanuzi wa barabara unaoendelea kuanzia eneo la
Ihumwa hadi Dodoma Mjini ambao ni matokeo ya jitihada za watendaji wenyewe mkoani.
Hapa Morogoro pia kazi hizi za upanuzi wa barabara zimeelezwa kuanza kutekelezwa
wakati ambapo mkoani Tabora tayari kuna zaidi ya kilometa sita za lami zimejengwa
kwa kutumia fedha zilizotengwa katika bajeti ya mkoa. “Ninawaelekeza Mameneja wa Tanroads
katika mikoa mingine nanyi muwe na ubunifu na sio kukaa bila ya kuchukua hatua zozote
hata pale ambapo tayari kuna bajeti iliyopitishwa” alimalizia Mheshimiwa Magufuli.