2013-02-15 08:16:15

Tafakari ya Neno la Mungu, Jumapili ya Kwanza ya Kipindi cha Kwaresima


Mpendwa mwana wa Mungu tayari tuko kipindi cha kwaresima, kipindi cha mfungo mtakatifu. Tunatafakari pamoja masomo Dominika ya Kwanza ya Kipindi cha kwaresima ya mwaka C wa Kanisa. Neno la Mungu latuwekea mbele yetu ushiriki wa Mungu katika matatizo ya mwanadamu. RealAudioMP3

Tunamwona Bwana anayejaribiwa na shetani lakini pia ambaye anashinda vishawishi hivyo kwa nguvu ya Mungu. Ushiriki wake katika mateso ya mwanadamu ni namna pia ya kuonesha uaminifu wake katika ahadi alizozitoa kwa taifa la Israeli. Sote twatambua, katika Agano la Kale aliwahaidi Wana wa Israeli kwamba atawapatia nchi ya ahadi, na hivi katika somo la kwanza tunaona anakamilisha hilo na Waisraeli wanahaidi kushika Agano kati yao na Mungu. Namna ya kushika agano lao na Mungu, watatoa malimbuko ya nchi kama shukrani kwa Mungu wao. Watawafundisha watoto wao sala ya agano lao daima katika maisha yao.

Bwana wetu Yesu Kristo anajaribiwa jangwani na anashinda, hili ni fundisho kwa wale wote wanaomfuata, yakwamba katika maisha yao ya Kikristu wasitarajie maisha lelemama bali maisha dhabiti ambayo mmoja anapaswa kuwa imara, akichota uimara huo katika Roho Mtakatifu na akimfuasa Bwana aliyejaribiwa na hatimaye kushinda. Bwana anapokuwa jangwani anafunga siku arobaini na hivi kwa njia hiyo anawasiliana na Baba yake, anajitenga na ulimwengu, anakusanya nguvu kwa ajili ya mapambano dhidi ya mwovu na kwa ajili ya utume wake wa kumwokoa mwanadamu. Mwaliko kwetu nasi, ni maisha ya jangwani yaani maisha ya sala, maisha ya kufunga na kujitakatifuza kwa njia ya sakramenti ya kitubio na Ekaristi Takatifu.

Mwovu shetani kadiri ya Injili anamtembeza Bwana na kumwonesha mali zote za dunia na fahari zote, akitaka kusema kuwa mambo ya kidunia yaweza kuwa ya maana kushinda yaliyo ya mbinguni, lakini Bwana akijua hila za mwovu huyu akimtii Baba yake wa mbinguni anajibu akisema imeandikwa usimjaribu Bwana Mungu wako, bali ukamsujudie Bwana Mungu wako na umwabudu yeye peke yake. Bwana anatuonesha jinsi ambavyo mwanadamu anaweka nguvu katika kutazama mambo ya dunia hii badala ya mambo ya kimungu. Kumbe sasa tunaalikwa kutazama zaidi mambo ya mbinguni kwa njia yake.

Mwovu shetani anajaribu kumwambia Bwana kuwa Mungu atakuagizia malaika waje kukulinda, huu ni mfano wa mbinu mbalimbali ambazo shetani hutumia kumwangusha mwanadamu. Habari juu ya malaika yataka kujenga mazingira ili Bwana aingie katika kiburi, lakini Bwana akijua kuwa kwa njia ya unyenyekevu ataweza kushinda anatupilia mbali hoja hiyo. Vivyohivyo inapaswa kuwa kwa mwanadamu, kupembua upumbavu wa mwovu shetani mapema na kuutupilia mbali. Hili huwezi kulitambua bila nguvu ya sala, bila kukaa jangwani ukifunga na kumwimbia Mungu tenzi za rohoni.

Mtume Paulo anapowaandikia Warumi anasema kwa kuwa tumekombolewa tayari, linalobaki ni kumkiri Yesu Kristu kwa kinywa chako, na kwa namna hiyo hutaweza kubabaika katika maisha na safari yako ya kikristu ukielekea mbinguni. Kumkiri Bwana si kuinuka na kutangaza majukwaani bali kufuata mfano wa Bwana katika kufunga na kusali ili kujipatia fadhila mbalimbali ambazo zatujaza neema kwa ajili ya wokovu wetu na wengine.

Kumkiri Bwana ni kutimiza mapenzi yake yaani kwenda mpaka msalabani kama yeye alivyofanya. Ni kuishi upendo mkamilifu yaani unaoshirikisha furaha itokayo katika fumbo la msalaba. Kumkiri Bwana ni kushika Torati kama ambavyo wana wa Israeli walivyohaidi kufanya walipotoka utumwani Misri na hata wakaweza kutoa malimbuko ya kazi ya mikono yao. Malimbuko haya waliyoyatoa kwa Bwana yalitumiwa na wajane, yatima na Walawi. Hili latuonesha upendo wao kwa Mungu na viumbe vyake. Kumbe kumkiri Bwana ni pia kumtolea shukrani toka kazi ya mikono na akili yako katika unyenyekevu.

Mpendwa mwana wa Mungu, kipindi cha kwaresima ni kipindi cha kupanda mbegu na kufanya palizi ili baadaye tuweze kupata mavuno mazuri. Kumbe jiweke katika mwelekeo huo ili usije baadaye ukakosa mazao na kuingia kwenye baa la njaa, yaani kukaukiwa neema za Mungu. Nikutakie mpando mwema na palizi angalifu ili tukutane tukiwa wa furaha mwishoni mwa kwaresima yetu, ndiyo uzima wa milele. Tumsifu Yesu Kristo.

Tafakari hii imeletwa kwako na Pd Richard Tiganya, C.PP.S.








All the contents on this site are copyrighted ©.