Kamwe dini zisiwe ni chanzo cha choko choko na vurugu za kidini Barani Afrika! Hizi
ni njama za wajanja wachache kutaka kutajirika!
Askofu mkuu Ignatius Ayau Kaigama wa Jimbo kuu la Jos, Nigeria anasema, kuna haja
kwa wananchi Barani Afrika kuhakikisha kwamba, wanaondokana na kasumba za kikoloni
zilizotumika kuwagawa watu kwa misingi ya kidini ili kuwatawala kwa urahisi.
Majadiliano
ya kidini, amani na utulivu ni jambo muhimu sana katika ulimwengu wa utandawazi na
kamwe ukabila na dini situmiwe na wajanja wachache kwa ajili ya mafao yao binafsi
kwa kusababisha maafa makubwa katika Jamii kama inavyojionesha nchini Nigeria. Katika
miaka ya hivi karibuni kumezuka wimbi kubwa la machafuko ya kidini, hali ambayo imechafua
kwa kiasi kikubwa upendo, umoja na mshikamano wa kitaifa uliokuwepo kwa miaka kadhaa
iliyopita. Baadhi ya viongozi wa kidini wamekuwa wakiwatumia vijana kuanzisha vurugu
na matokeo yake ni maafa makubwa kwa Jamii na ni kikwazo kikuu cha maendeleo na ustawi
wa Kijamii.
Ili kuondokana na dhana potofu kuhusu dini, kuna haja kwa viongozi
wa kidini kutoa mafundisho ya kina kuhusu dini zao, daima wakitetea haki, amani, upendo
na mshikamano wa kitaifa. Kuna baadhi ya waamini wanadhani kwamba, kuna dini ambazo
zimebahatika kutoa miujiza na kwamba, wanakwenda huko kwa imani kwamba, iko siku Mwenyezi
Mungu atawapatia muujiza wao na hivyo kuwa na hali nzuri kiuchumi, kijamii pamoja
na kuwaondolea magonjwa au balaa zinazowaandama katika maisha.
Askofu mkuu
Kaigama anasema, uwezo mdogo wa kufikiri kwa baadhi ya watu, wamejikuta wakitumbukizwa
katika imani za kishirikina, kwa kudhani kwamba, viungo vya watu wenye ulemavu wa
ngozi vina fumbata bahati na matokeo yake ni wimbi la mauaji ya watu wasiokuwa na
hatia, kama ilivyo pia kwa mauaji ya vikongewe sehemu mbali mbali za Bara la Afrika.
Jamii iwekeze katika elimu, afya na maendeleo endelevu, watu waondokane na
imani, mila, desturi na tamaduni zilizopitwa na wakati. Wananchi wajifunze kufanya
kazi kwa juhudi, maarifa na bidii, wajitahidi kupata riziki kwa kufanya kazi halali
na kwamba, hakuna njia ya mkato ili kupata mafanikio.
Tofauti za kidini na
kikabila ni sehemu ya maisha ya watu, kumbe, kuna haja ya kujenga utamaduni wa kuvumiliana,
kuheshimiana na kuthaminiana, kamwe dini zisiwe ni chanzo cha choko choko na vurugu
katika Jamii, bali iwe ni nguzo inayojenga misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano.
Askofu mkuu Kaigama ameyasema hayo hivi karibuni alipokuwa anatoa mhadhara kwenye
Chuo Kikuu cha Colon, nchini Ujerumani.