2013-02-15 07:48:45

Baba Mtakatifu Benedikto XVI akutana na Makleri wa Jimbo kuu la Roma


Kwa niaba ya Makleri wote wa Jimbo kuu la Roma, Kardinali Agostino Vallini, Makamu Askofu Jimbo kuu la Roma, Alhamisi, tarehe 14 Februari, 2013, alimshukuru Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita kwa kukubali kuitikia wito wa kuweza kukutana na kuzungumza na Makleri wake, ili kuwamegea utajiri mkubwa ambao watautunza kama hazina kubwa wanapotekeleza majukumu yao kwa Familia ya Mungu, Jimboni Roma.

Anasema, mioyo yao imegubikwa na hamu ya kutaka kusikiliza kwa makini wosia kutoka kwa Mchungaji mkuu wa Kanisa anapokaribia kung’atuka kutoka madarakani, kama walivyofanya wazee walipokuwa wanamsikiliza Mtume Paulo. Alipokuwa anawaaga, akiwakumbusha kwamba, kati yao, amejitahidi kumtumikia Kristo kwa moyo na unyenyekevu mkubwa, kwa machozi na majaribu mengi, lakini bila ya kukata tamaa. Amewahubiria na kuwashuhudia kuhusu umuhimu wa kumwongokea Mungu pamoja na kuwa na imani thabiti kwa Kristo. Hata wao wana mioyo mizito iliyosheheni mambo mengi, wanakubali na kuthamini maamuzi yake.

Kama Khalifa wa Mtakatifu Petro, amewafundisha kuwa wafuasi amini wa Kristo na wachungaji bora; wakijitahidi kutolea ushuhuda wa maisha ya kujitoa kimaso maso kwa Kristo na Kanisa lake bila ya kujibakiza hata chembe kidogo! Wawe na imani inayoonesha ujasiri; unyenyekevu katika huduma, daima wakichuchumilia ukweli na hamu ya kutaka kuhubiri Injili ya Kristo; wakitoa kipaumbele cha kwanza kwa utu na heshima ya binadamu; hususan maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Mwaka wa Imani ambao Mama Kanisa anaendelea kuuadhimisha ni changamoto kubwa ya kufanya toba na kuchuchumilia utakatifu wa maisha kama kielelezo makini cha huduma kwa watu wa Mungu.

Maadhimisho ya Jubilee ya miaka 50 ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican ni ufunguo muhimu sana katika kuyafahamu maisha na utume wa Kanisa, wakati huu wa mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo. Ni mwaliko wa kuona mwendelezo wa Mapokeo ya Kanisa, kujibidisha kuzifahamu hati na nyaraka mbali mbali za Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican pamoja na kuwashirikisha wengine, kama nyezo muhimu sana ya kuleta mabadiliko ndani ya Kanisa.

Ndiyo maana, Makleri wa Roma wamemwomba, Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, aliyeshiriki katika Maadhimisho ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican kuwashirikisha yale yaliyojiri wakati wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, miaka 50 iliyopita! Makleri wa Jimbo kuu la Roma wanasema, wataendelea kumsindikiza Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, kwa njia ya sala na sadaka zao.








All the contents on this site are copyrighted ©.