Familia ya Mungu inamshukuru na kumpongeza Baba Mtakatifu Benedikto XVI kwa unyenyekevu
na ujasiri wake!
Kardinali Tarcisio Bertone, Katibu mkuu wa Vatican mara baada ya maadhimisho ya Ibada
ya Misa takatifu kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, Jumatano ya Majivu,
tarehe 13 Februari, 2013, kwa niaba ya Familia ya Mungu, alimshukuru Baba Mtakatifu
Benedikto wa kumi na sita, kwa uamuzi wake wa ujasiri na hekima, miaka minane ya uongozi
wake, amekuwa ni dirisha wazi kwa Kanisa na Ulimwengu, kwa kuonesha miali ya ukweli
na upendo wa Mungu; kwa kutoa joto katika hija ya maisha ya Kanisa hata pale giza
nene lilipoonekana kana kwamba limetanda angani na hivyo kutishia amani!
Baba
Mtakatifu ameonesha upendo mkubwa kwa Mungu na Kanisa, kwa kuonesha usafi wa roho,
imani thabiti, unyenyekevu na ujasiri; mambo yaliyoacha chapa ya kudumu katika maisha
na utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro. Haya ni matokeo ya mtu aliyeshibana
kwa kiasi kikubwa na Mwenyezi Mungu, anayefanya tafakari ya kina ya Neno la Mungu,
daima akijitahidi kukwea Mlimani ili kuweza kukutana na Muumba wake katika faragha,
ili hatimaye, kushuka na kuwasaidia wajenzi wa dunia.
Daima watakumbuka maneno
yake kwa Jumuiya ya Seminari kuu ya Roma kwamba, yale yajayo yako mikononi mwa Mwenyezi
Mungu na kwamba, Kanisa litaendelea kukua na kukomaa. Huduma katika ujenzi wa Kanisa
ni kazi inayofanywa na Mwenyezi Mungu mwenyewe, binadamu ni kama chombo kisichokuwa
na faida.
Kardinali Bertone, anamshukuru Baba Mtakatifu kwa kufanya uamuzi
huu mgumu na wa busara, mfano na kielelezo makini kwanza kabisa kwa viongozi wa Kanisa
na kwa Familia ya Mungu katika ujumla wake. Maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi takatifu
ni kielelezo cha shukrani mbele ya Mwenyezi Mungu.
Kanisa linamshukuru Baba
Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita kwa hija ya maisha na utume wake katika kipindi
cha miaka minane, kwa hakika amekuwa ni mwanga angavu na mfano wa mfanyakazi mnyenyekevu
katika shamba la Bwana, aliyetambua daima kwamba, anayo dhamana ya kumpeleka Mungu
kwa watu na kuwapeleka watu kwa Mungu.