Benedikto XVI atakumbukwa kwa mchango wake mkubwa katika majadiliano ya kiekumene,
ili wote wawe wamoja!
Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Barani Ulaya, limemwandikia Baba Mtakatifu
Benedikto wa kumi na sita, barua ya shukrani kutokana na uaminifu, ujasiri na majitoleo
makubwa aliyoyaonesha wakati wa utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro; dhamana
ambayo ilisheheni utajiri mkubwa wa mafundisho pamoja na huduma mbali mbali alizozitoa
kwa ajili ya Watu wa Mungu Barani Ulaya.
Baba Mtakatifu ameonesha ukomavu
wa imani kwa kumwaminia na kumwonesha Yesu Kristo mapendo ya hali ya juu kwa njia
ya Kanisa lake. Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Ulaya, wakati huu linapenda
kumwonesha Baba Mtakatifu upendo na uwepo wao wa karibu katika kipindi hiki kigumu
cha historia ya maisha na utume wake.
Wanapenda kumhakikishia kwamba, wataendelea
kulihudumia Kanisa kwa ari na imani ambayo Baba Mtakatifu mwenyewe ameionesha na kuishuhudia.
Barua hii imetiwa mkwaju na Kardinali Peter Erdo, Rais wa Shirikisho la Mabaraza ya
Maaskofu wa Bara la Ulaya kwa niaba ya viongozi wakuu wa Shirikisho hili.
Wakati
huo huo, Patriaki Bartolomeo wa kwanza wa Kanisa la Kiorthodox la Costantinopoli,
anamshukuru Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita kwa ushuhuda wa majadiliano ya
kiekumene aliouonesha wakati wa uongozi wake, kama: Mwanataalilimungu mahiri, Mtaalam
wa Mababa wa Kanisa na mwenye upeo mkubwa kwa masuala mamboleo.
Anasema, amesikitishwa
na taarifa ya kung’atuka kwa Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita kutoka madarakani
na kwamba, anaacha chapa ya kudumu katika mchakato wa kudumisha majadiliano ya Kiekumene
yaliyojikita katika ushuhuda wa maisha adili na historia ya Kanisa Katoliki. Miaka
minane si haba!
Daima Baba Mtakatifu amekuwa akijikita katika kushughulikia
masuala ya utu na heshima ya binadamu pamoja na mafao ya wengi. Waamini wa Kanisa
la Kiorthodox wataendelea kukumbuka hija ya kichungaji aliyoifanya kwenye Kanisa lao
wakati wa uongozi wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro.