2013-02-13 07:27:42

Matendo ya huruma yaongozwe na: imani na matumaini kama kielelezo cha mshikamano wa dhati!


Shirikisho la Vyama vya Mtakatifu Vinsenti wa Paulo Kimataifa, lililoanzishwa yapata miaka 180 iliyopita na kuwa na wanachama zaidi 780,000, wanaowahudumia maskini zaidi ya millioni 30; linaongozwa na kanuni ya imani, matumaini na mapendo yanayobubujika kutoka katika kweli za Kiinjili. RealAudioMP3
Ni Shirikisho linalopania kumhudumia mtu mzima katika mahitaji yake ya kiroho na kimwili. Hawa ni watu walioathirika kutokana na umaskini, magonjwa na ujinga. Watu ambao wakati mwingine wanajikuta wametumbukizwa katika umaskini kutokana na vita, migogoro, kinzani, majanga asilia pamoja ubinafsi wa watu kama inavyojionesha katika athari za myumbo wa uchumi kimataifa.
Ni Shirikisho ambalo limeendelea kuwa mstari wa mbele kwa kutoa huduma katika sekta ya elimu, afya na maendeleo endelevu, ili kuweza kumletea mwanadamu ukombozi kamili. Limekuwa likitoa msaada wa mikopo midogo midogo, ili kuwajengea wananchi uwezo wa kupambana na maisha, ili hatimaye, waweze kujiletea maendeleo yao wenyewe!
Kutokana na ushiriki wake katika huduma ya upendo kwa watu wenye matatizo mbali mbali, Umoja wa Mataifa mwaka 2012 ulilitambua Shirikisho la Vyama vya Mtakatifu Vinsenti wa Paulo Kimataifa, kuwa ni kati ya Mwanachama wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali ya Umoja wa Mataifa katika huduma za Kijamii (ECOSOC).
Huu ni ushuhuda uliotolewa na Dr. Michael Thio, Rais wa Shirikisho la Vyama vya Mtakatifu Vinsenti wa Paulo, wakati wa kuwasilisha ujumbe wa Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita kwa Kipindi cha Kwaresima kwa Mwaka 2013. Ni Shirikisho la Kimataifa linalotekeleza utume na dhamana yake katika ulimwengu kwa kuongozwa na Imani, Matumaini na Mapendo. Haya ni matunda ya ukimya yanayobubujika katika Sala; ni kielelezo cha Sala katika Imani na matunda ya Imani katika upendo unaopania kudumisha amani.
Hii ni sehemu ya tafakari ya kina kutoka kwa Mama Theresa wa Calcuta, moja ya Watoto wa Kanisa waliojitoa bila ya kujibakiza ili kuwamegea maskini, wasiopendwa na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii, ule upendo wa dhati unaobubujika kutoka katika Imani kwa Kristo na Kanisa lake, changamoto kwa kila mwamini kumwilisha Imani yake katika matendo, hasa wakati wa Kipindi cha Kwaresima, Kipindi cha toba na wongofu wa ndani; mwaliko wa kufanya tafakari ya kina ya Neno la Mungu pamoja na kuboresha maisha ya kiroho kwa njia ya Sakramenti za Kanisa.








All the contents on this site are copyrighted ©.