2013-02-13 09:15:52

Jifunzeni kukubali, kuthamini na kupokea tofauti za kijamii, kisiasa, kidini na kikabila, ili kujenga misingi ya haki, amani na utulivu!


Askofu mkuu Zacchaeus Okoth, Mwenyekiti wa Tume ya haki na amani ya Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya katika uzinduzi wa Kampeni ya Kwaresima kwa Mwaka 2013 amefafanua kwamba, Baraza la Maaskofu litafuatilia kwa ukaribu mchakato wote wa uchaguzi lakini halitajihusisha na Kampeni kwa ajili ya wagombea mbali mbali wanaowaminia nafasi ya uongozi nchini Kenya.

Wananchi wa Kenya bado wanayo kumbu kumbu hai ya madhara na maafa makubwa yaliyojitokeza mara tu baada ya matokeo ya uchaguzi mkuu uliofanyika nchini Kenya kunako mwaka 2007/2008. Wananchi wa Kenya wanataka kuona umoja wa kitaifa unaosimikwa katika misingi ya amani, kwani vurugu na machafuko ya kisiasa yatapelekea maafa kwa watu na mali zao.

Viongozi wanaowania madaraka wanapaswa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa mafao ya wengi, haki, amani na utulivu na kwamba, uchaguzi mkuu isiwe tena ni chanzo cha kuwagawa wananchi wa Kenya. Wananchi wajifunze: kukubali, kuthamini na kupokea tofauti zao za kijamii, kisiasa, kidini na kikabila.

Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya katika kipindi cha Majuma manne, litaangalia kwa kina na mapana: Juma la kwanza wataangalia kuhusu usalama na wajibu wa kila mwananchi; Juma la pili: Uchaguzi mkuu; Juma la tatu: utawala wa Serikali za mitaa. Juma la nne Upatanisho na msamaha na mwishoni, Watoto na Familia.







All the contents on this site are copyrighted ©.