2013-02-13 08:51:49

Baraza la Maaskofu Kenya lazindua Kampeni ya Kwaresima kwa Mwaka 2013


Kardinali John Njue, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya hivi karibuni amezindua kampeni ya kipindi cha Kwaresima kwa Mwaka 2013 inayoongozwa na kauli mbiu "Napenda kuona Kenya iliyoungana na yenye amani". Kwaresima ni hija ya maisha ya kiroho pamoja na Yesu Kristo kwa siku arobaini, ili kujiandaa kusherekea Fumbo la Pasaka. Ni kipindi cha toba na wongofu wa ndani; kufunga na kusali pamoja na kuimwilisha imani katika matendo.

Kardinali Njue anawaalika waamini kutubu na kumwongokea Mwenyezi Mungu, ili kuboresha mahusiano yao na Mwenyezi Mungu pamoja na jirani. Maneno na matendo yao yawe ni chemchemi ya upendo inayobubujika kutoka kwa Mwenyezi Mungu, changamoto ya kukimbilia huruma na upendo wake usiokuwa na kifani. Waamini na wananchi wa Kenya wakati huu wa mchakato wa uchaguzi mkuu wanaalikwa kuombea amani na utulivu ili maafa yaliyotokea kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka 2007/2008 yasijirudie tena. Hili liwe ni fundisho kwa wakenya wote kuchuchumilia amani kwa gharama yote.

Kardinali Njue katika uzinduzi wa Kampeni ya Kwaresima kwa Mwaka 2013, tukio ambalo limehudhuriwa na Familia ya Mungu nchini Kenya, anawaalika wananchi wote kuhakikisha kwamba, lugha ya amani inakuwa ni dira na mwongozo katika maisha yao, kwani huu ndio urithi mkubwa ambao Yesu mwenyewe amewaachia wanafunzi wake.

Ikumbukwe kwamba, amani ni zawadi kutoka kwa Mungu, lakini mwanadamu pia ana mchango wake. Watu wajenge utamaduni wa upendo bila kujali mahali, dini au rangi ya mtu, kwani wote wameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.

Amani na utulivu ni vikolezo vya maendeleo ya kiuchumi, kijamii na kidini, kamwe wananchi wa Kenya wasijitumbukize katika machafuko ya kisiasa kwani yatawagharimu sana. Kenya inatarajia kufanya uchaguzi mkuu hapo tarehe 4 Machi 2013.







All the contents on this site are copyrighted ©.