2013-02-13 10:57:15

Baba Mtakatifu Benedikto XVI ni mfano wa kuigwa katika uamuzi wake wa kung'atuka kutoka madarakani


Kardinali Polycarp Pengo, Rais wa Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika na Madagascar, SECAM, ameupongeza uamuzi mzito na wa kishujaa uliofanywa na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita wa kung'atuka kutoka madarakani na kwamba, huu ni mfano bora na kielelezo cha kuigwa na viongozi wengine duniani.

Ameonesha unyenyekevu wa hali ya juu kabisa baada ya kuona ukweli kutoka katika undani wake na hatimaye, kwa utashi na uhuru wake kamili akatamka hadharani kwamba, anang'atuka kutoka madarakani. Baba Mtakatifu anaonesha kwamba, Mwenyezi Mungu ndiye anayepaswa kuogopwa zaidi na kwamba, daima ataendelea kuwapo ili kuwaongoza, kwa kuishi na kutambua kwamba, wao ni watu wake.

Uamuzi huu iwe ni changamoto kwa viongozi sehemu mbali mbali za dunia katika utekelezaji wa majukumu yao kwa Jamii kwa kupima uwezo wao na pale wanapoona kwamba, hawezi kumudu tena, basi wawe na ujasiri wa kung'atuka! Kuna baadhi ya viongozi wamekaa madarakani kwa kipindi kirefu na watu wanaendelea kuteseka kwa sababu yao.

Hakuna sababu ya waamini kuingiwa na hofu kwa kung'atuka kwa Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, kwani Kanisa Katoliki litaendelea kuungana na kuwa ni kitu kimoja. Kwa hakika ni tukio ambalo limewaacha watu wengi wakiwa wameshikwa na butwaa baada ya tukio kama hili kufanyika takribani karne sita zilizopita.







All the contents on this site are copyrighted ©.