2013-02-12 07:09:17

Ujumbe wa Baba Mtakatifu Benedikto XVI kwa Kipindi cha Kwaresima 2013


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, anatarajiwa kuadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya kukianza kipindi cha Kwaresima kwa Mwaka 2013, kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro, mjini Vatican, majira ya saa 11:00 saa za Ulaya. Uamuzi huu umechukuliwa baada ya Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, kwa utashi na uamuzi wake mwenyewe kuamua kung'atuka kutoka madarakani kuanzia tarehe 28 Februari 2013, saa 2:00 Usiku.

Imani ni jibu makini la upendo wa Mungu; upendo ni kielelezo cha maisha katika imani. Upendo na imani ni chanda na pete, kamwe haviwezi kutenganishwa bali ni fadhila zinakamilishana, lakini imani inachukua kipaumbele cha kwanza kuliko upendo, kwa sababu ni zawadi kutoka kwa Mungu. Kwa ufupi huu ndio muhtasari wa Ujumbe wa Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita kwa Kipindi cha Kwaresima kwa Mwaka 2013. RealAudioMP3

Ujumbe wa Kwaresima kutoka kwa Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, kwa Mwaka 2013 unaongozwa na kauli mbiu “Kuamini katika pendo kunaamsha upendo: tumelifahamu pendo la Mungu lililoko ndani mwetu”. Kwaresima ya Mwaka huu inakwenda sanjari na Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, fursa makini ya kutafakari uhusiano uliopo kati ya imani na upendo; kati ya kumwamini Mungu; kati ya kumwamini Mungu wa Yesu Kristo na upendo ambao kimsingi ni kazi ya Roho Mtakatifu inayowaongoza waamini kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya Mungu na jirani.

Baba Mtakatifu anasema kwamba, imani ni jibu makini la upendo wa Mungu na kuwa, kuna uhusiano wa dhati kati ya fadhila hizi za kimungu, kama alivyokwisha bainisha katika Waraka wake wa kichungaji, Mungu ni Upendo. Maisha ya wakristo wa kwanza yalipata mwelekeo mpya kwa kukutana na kuonja pendo la Kristo katika hija ya maisha yao, kwa kutambua kwamba, Mungu ndiye aliyewapenda kwanza, kumbe jibu ambalo waamini wanamtolea Mungu si amri bali ni kielelezo cha zawadi ya upendo ambao kwao unamsukuma Mwenyezi mungu kumwendea mwanadamu na hivyo mwanadamu mwenyewe anakuwa na jukumu la kujishikamanisha na Mungu.

Upendo wa Mungu ni mwaliko kwa mwamini kujitoa kikamilifu katika akili na utashi wake, kumtambua Mwenyezi Mungu ambaye ni hai. Huu ni mchakato endelevu katika hija ya maisha ya mwanadamu, lakini zaidi kwa wahudumu wa upendo wanaopaswa kujishikamanisha na imani kwa Mungu nayejifunua kwa njia ya Yesu Kristo, akiwaonjesha upendo kwa Mungu na jirani. Kwa njia hii imani inatenda katika upendo. Dhana ya upendo mkamilifu inapata chimbuko lake kwa kutambua kwanza kabisa kwamba, mtu anapendwa, anasamehewa na kuhudumiwa na Kristo, aliyejinyenyekesha kiasi hata cha kuinama na kuwaosha mitume wake miguu; akayamimina maisha yake pale juu Msalabani ili kuwavuta watu wote katika pendo lake.

Imani aliyo nayo mwamini kuwa Mwenyezi Mungu amemtoa Mwanaye wa Pekee, inaamsha uhakika kwamba kweli Mungu ni upendo, unaojionesha kwa kwa njia ya Yesu Kristo aliyetobolewa kwa mkuki ubavuni, ili kumwonjesha mwanadamu upendo usiokuwa na kifani, unamkirimia nguvu ya kuishi na kutenda mintarafu upendo unaobubujika kutoka katika kisima cha imani.

Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita anasema kwamba, upendo ni kama maisha katika imani, kwani maisha yote ya Kikristo ni kama jibu muafaka la upendo wa Mungu ambao kimsingi ni zawadi, inayoonesha hija katika mwanga wa urafiki na Kristo anayetoa maana halisi ya maisha ya mwamini. Mwenyezi Mungu anapenda kuwavuta watu kwake na kuwapatia mabadiliko ya ndani, kiasi kwamba, wanaweza kudiriki kusema, si wao wanaoishi, bali Kristo anaishi ndani wao.

Baba Mtakatifu katika ujumbe wake wa Kwaresima kwa Mwaka 2013 anaendelea kubainisha kwamba, ikiwa kama waamini watamwachia Mungu nafasi katika maisha yao, wataweza kushiriki kikamilifu katika pendo lake, kiasi kwamba, imani inakuwa tendaji na Mungu mwenyewe anafanya makao kwa mwamini. Imani inatambua ukweli na kuukumbatia.

Upendo ni mchakato unaomwezesha mwamini kutembea katika ukweli na kwa njia ya imani, mwamini anajenga urafiki na Kristo; anapokea na kuimwilisha amri ya upendo pamoja na kuendelea kujisikia kuwa ni watoto wapendwa wa Mungu wakibeba ndani mwao tunda la Roho Mtakatifu. Imani inamwezesha mwamini kutambua karama ambazo Mwenyezi Mungu amemkirimia mwamini na upendo unamsaidia kuzifanya karama hizi ziweze kuzaa matunda.

Kuna uhusiano mkubwa kati ya Imani na Mapendo na kwamba si rahisi kuweza kutenganisha fadhila hizi za Kimungu, lakini ifahamike kwamba, matendo peke yake hayawezi kuwa mbadala wa imani. Vi vyema kuwa makini kwa kuiwezesha imani kuonekana katika matendo, kama hija ya kumwendea Mwenyezi Mungu, kwa kumhudumia Mungu na jirani.

Baba Mtakatifu anabainisha kwamba, Kanisa la Mwanzo liliweza kustawi kutokana na kujikita katika huduma kwa maskini na wote waliokuwa wanasukumizwa pembezoni mwa Jamii. Hapa Kanisa linaonesha sura mbili: tafakari na matendo; kama ilivyokuwa katika maisha ya Maria na Martha; kumbe sura hizi mbili zinapaswa kwenda pamoja katika maisha na utume wa Kanisa. Mwenyezi Mungu hana budi kupewa kipaumbele cha kwanza na mshikamano wa kweli wa upendo unapaswa kujikita katika imani.

Kielelezo cha hali ya juu kabisa cha Upendo ni Uinjilishaji, unaowawezesha Waamini kumegeana Mkate wa Neno la Mungu kwa kuwasaidia jirani kujenga uhusiano a karibu na Mwenyezi Mungu sanjari na huduma kwa binadamu. Uinjilishaji wa kina ni kati ya vielelezo vya juu kabisa vya maendeleo ya binadamu, kama alivyobaini Papa Paulo wa sita. Huu ni ukweli wa upendo unaobubujika kutoka kwa Mwenyezi Mungu, ukamwilishwa na kutangazwa; kama utapokelewa kwa mikono miwili unaweza kuleta maendeleo endelevu kwa kila binadamu.

Upendo wa Mungu kwa binadamu umefahamika kwa njia ya Utangazaji wa Injili, ukipokelewa kwa imani thabiti, unawawezesha pia kupenda pendo lenyewe, ili kukua na kukomaa katika Pendo ili hatimaye, kuwashirikisha wengine ile furaha inayobubujika kutoka katika Pendo hili. Mwanadamu anakombolewa kwa njia ya Imani, ambayo kimsingi ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu.

Ni Mungu mwenyewe anayeanzisha juhudi za kutaka kumkomboa mwanadamu anayepokea msamaha huu kwa njia ya imani, inayohitaji kwanza kabisa uhuru na uwajibikaji unaojielekeza katika matendo ya upendo. Haya ni matunda ya imani yanayobubujika kutoka katika neema ya Mungu na wala si juhudi za mtu binafsi. Imani bila matendo ni sawa na mti bila matunda; kumbe fadhila hizi mbili ni sawa na chanda na pete, zinafungamana na kushibana.

Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, anasema Kipindi cha Kwaresima ni mwaliko kwa waamini kujenga utamaduni wa kusoma, kutafakari na kulimwilisha Neno la Mungu katik uhalisia wa maisha; kushiriki Sakramenti za Kanisa pamoja na kutenda matendo ya huruma kwa Mungu na jirani kwa njia ya kufunga, matendo ya toba na kutoa sadaka. Lakini ikumbukwe kwamba, Imani inachukua kipaumbele cha pekee kuliko upendo, kwani Imani ni zawadi kutoka kwa Mungu na kwamba fadhila zote mbili ni kazi ya Roho Mtakatifu.

Imani ni zawadi na jibu makini linalomwezesha mwamini kuufahamu ukweli juu ya Kristo kuwa ni Upendo uliomwilishwa na kusulubishwa; upendo mkamilifu unaojikita katika mapenzi ya Mungu na huruma isiyokuwa na kifani kwa jirani. Imani inajikita katika moyo na akili ya mwamini, inayomwezesha kupata ushindi dhidi ya ubaya na kifo.

Imani inamsukuma mwamini kutumainia kwamba, siku moja upendo wa Kristo utaweza kufikia utimilifu wake. Upendo unamwezesha mwamini kuingia katika mahusiano na Mungu aliyejionesha kwa njia ya Yesu Kristo, kiasi cha mwamini kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya Mungu na jirani. Kuna uhusiano mkubwa kati ya Sakramenti ya Ubatizo ambayo ni kielelezo cha imani na sakramenti ya Ekaristi Takatifu, kielelezo cha upendo. Sakramenti ya Ubatizo inatangulia Sakramenti ya Ekaristi Takatifu, lakini zote ni muhimu katika utimilifu wa hija ya maisha ya Mkristo. Imani iwawezesha waamini kumpenda Mungu na jirani.

Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, anahitimisha Ujumbe wake wa Kwaresima kwa kuwakumbusha kwamba, Kipindi cha Kwaresima kinawawezesha kujiandaa kikamilifu katika kusherehekea Fumbo la Pasaka:Mateso yanayojionesha kwa njia ya Msalaba na Ufufuko unaodhihirisha kwamba, upendo wa Mungu umeukomboa ulimwengu; changamoto ya kuishi kikamilifu imani na mapendo kwa Mungu na jirani.








All the contents on this site are copyrighted ©.