2013-02-12 10:17:52

Makardinali wenye dhamana ya kumchagua Papa Mpya


Mkutano wa Dekania ya Makardinali kwa kama unavyojulikana na wengi "Conclave" utakaokutana mwanzoni mwa Mwezi Machi mwaka huu ili kumchagua Papa mwingine baada ya Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita kung'atuka madarakani hapo tarehe 28 Februari 2013 utaongozwa na Katiba iliyotolewa na Mwenyeheri Yohane Paulo wa pili "Universi Dominici Gregis".

Kardinali Camerlengo Tarcisio Bertone, aliyeteuliwa na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita hapo tarehe 4 Aprili 2007 atakuwa ni kiongozi mkuu katika kipindi hiki cha mpito.

Makardinali wenye haki ya kupiga na kupigiwa kura kwa sasa kutoka Barani Ulaya ni Makardinali 61, Amerika ya Kusini wako 19, Amerika ya Kaskazini kuna Makardinali 14, kutoka Barani Afrika kuna Makardinali 11, Bara la Asia ni Makardinali 11na kuna Kardinali mmoja kutoka Oceania. Idadi ya Makardinali wenye haki ya kupiga na kupigiwa kura inaweza kubadilika kadiri ya tarehe za kuzaliwa Makardinali. Kwa mfano, Kardinali Walter Kasper, tarehe 5 machi 2013 atasherehekea miaka 80 ya kuzaliwa kwake.

Hadi sasa takwimu zinaonesha kwamba, kuna Makardinali wengi kutoka Italia, ambayo ina Makardinali 21. Makardinali 67 wenye haki ya kupiga na kupigiwa kura waliteuliwa na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita katika kipindi cha uongozi wake. Makardinali 117 watakaokuwa na dhamana ya kumchagua Papa Mpya watalazimika kuishi ndani ya Vatican, nje kidogo ya Kikanisa cha Sistina, mahali ambapo mchakato wa uchaguzi wa Papa mpya utakuwa unaendelea.

Wakati wote huu, Makardinali wataishi ndani ya Vatican na hakuna atakayeruhusiwa kukutana nao wakati wote wa mkutano wa kumchagua Papa wakati wanatoka au kurudi kutoka katika Kikanisa cha Sitina. Mawasiliano yote na watu wa nje yamazuiliwa.

Uchaguzi wa Papa utakapokamilika, ishala ya moshi mweupe itatolewa na hatimaye, Papa Mpya kutangazwa. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican, itakuwa nawe sambamba ili kukujuvya yanayojiri wakati wote huu.







All the contents on this site are copyrighted ©.