2013-02-12 07:25:32

Kanisa limelipokea Tamko la Baba Mtakatifu Benedikto XVI kwa mshangao mkubwa!


Kardinalo Angelo Sodano, Dekano wa Makardinali, Jumatatu tarehe 11 Februari 2013 kwa niaba ya Makardinali wenzake amemwambia Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita kwamba, wamepokea habari za kung'atuka kwake madarakani kwa mshangao mkubwa! Ni tamko linaloonesha upendo mkuu kwa Kanisa la Mungu.

Makardinali wataendelea kumwonesha mshikamano na ushirikiano wa dhati hasa wakati huu baada ya kufanya maamuzi mazito kwa ajili ya mafao na ustawi wa Kanisa baada ya kuliongoza Kanisa Katoliki kwa takribani miaka 8. Ilikuwa ni tarehe 19 Aprili 2005 alipokubali kubeba dhamana ya uongozi wa Kanisa Katoliki, akajiweka chini ya ulinzi na usimamizi wa Bikira Maria, akifuata nyayo za watangulizi wake 265 waliowahi kuliongoza Kanisa Katoliki tangu Mtakatifu Petro, yapata miaka elfu mbili iliyopita.

Kardinali Sodano anabainisha kwamba, kabla ya tarehe 28 Februari 2013, saa 2:00 Usiku, watapata nafasi ya kutoa heshima na shukrani zao za dhati, kama ambavyo watafanya viongozi wa Kanisa, Waamini na Watu wenye mapenzi mema kutoka sehemu mbali mbali za dunia. Katika kipindi hiki cha mpito, Kanisa bado litaendelea kumsikiliza Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, katika mahubiri yake Jumatano ya Majivu, Mama Kanisa anapokianza kipindi cha Kwaresima; kwenye Katekesi zake Jumatano, Mkutano pamoja na Makleri wa Jimbo kuu la Roma pamoja na tafakari zake wakati wa Sala ya Malaika wa Bwana.







All the contents on this site are copyrighted ©.