Ujumbe wa Bikira Maria wa Lourdes: wongofu wa ndani, sala na matendo ya huruma
Maadhimisho ya Siku ya Wagonjwa Duniani ni fursa makini ya kusali, kushirikishana
na kutolea mateso kwa ajili ya mafao ya Kanisa na changamoto ya kuendelea kuiangalia
ile sura ya Kristo mteswa miongoni mwa wagonjwa na wote wanaoteseka kimwili na kiroho.
Bikira Maria ni mwombezi wa wote wanaomkimbilia katika shida na magumu ya
maisha; watu wanaojitahidi kutubu na kuongoka, hao kwa hakika wanaonja upendo na huruma
ya Mungu katika maisha yao, kama inavyojionesha kwa baadhi ya waamini wanaofanya hija
ya maisha ya kiroho kwenye Madhabahu ya Bikira Maria wa Lourdes, Ufaransa.
Hii
ni sehemu ya mahubiri yaliyotolewa na Kardinali Fernando Filoni, Mwenyekiti wa Baraza
la Kipapa la Uinjilishaji wa watu wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Wagonjwa Duniani,
kwenye Kanisa kuu la Chennai na kama sehemu ya uzinduzi wa Seminari ya Kitaifa kwa
ajili ya majiundo ya waamini walei nchini India.. Ujumbe wa Bikira Maria wa Lourdes,
daima umekuwa ukisisitiza juu ya wongofu wa ndani, sala na matendo ya huruma. Hapa
kumekuwa ni chem chemi ya neema, huruma na upendo wa Mungu kwa binadamu.
Mababa
wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican wanakazia umuhimu wa waamini walei katika maisha
na utume wa Kanisa, katika mchakato wa kuyatakatifuza malimwengu kwa njia ya ushuhuda
wa maisha yao pamoja na matumizi makini ya karama na mapaji waliyokirimiwa na Roho
Mtakatifu kwa njia ya Sakramenti ya Ubatizo. Walei wanashiriki: ukuhani, unabii na
ufalme wa Kristo na kuimarishwa kwa Sakramenti ya Kipaimara ili waweze kuwa ni mashahidi
wa Kristo na Kanisa lake.
Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, iwe ni fursa makini
kwa waamini kutambua na kutekeleza wito na dhamana yao ndani ya Kanisa. Fadhila ya
imani, matumaini na mapendo zijioneshe miongoni mwa waamini; daima wakijitahidi kutangaza
Habari Njema ya Wokovu hadi miisho ya dunia, ili kuwasaidia watu kujenga uhusiano
na mshikamano wa dhati na Mwenyezi Mungu.
Baba Mtakatifu anabainisha kwamba,
Mwaka wa Imani ukoleze maadhimisho ya Liturujia ya Kanisa yanayofikia kilele chake
katika adhimisho la Fumbo la Ekaristi Takatifu, chanzo na kilele cha maisha na utume
wa Kanisa. Waamini wajikite katika maisha ya sala na ushuhuda wa imani tendaji. Waamini
walei wajishughulishe kikamilifu katika medani mbali mbali za maisha ya watu.
Vyama
vya kitume, viwe ni cheche za majiundo, urithishaji wa imani pamoja na utekelezaji
wa mikakati ya kichungaji inayotolewa na Makanisa mahalia. Waamini wajitahidi kukuza
na kudumisha moyo na ari ya kimissionari, tayari kutangaza Injili ya Kristo hadi miisho
ya dunia.