2013-02-11 08:09:41

Tamko la Baraza la Maaskofu Katoliki Italia baada ya mkutano


Taarifa ya Baraza la Maaskofu Katoliki Italia katika mkutano wake uliohitimishwa hivi karibuni, wanamwona Yesu kuwa ndiye Msamaria mwema, changamoto kwa Kanisa kuendelea kuwa ni Msamaria mwema kwa wote wanaoteseka na kutaabika kiroho na kimwili. RealAudioMP3

Maaskofu wanaonesha mshikamano wao wa dhati na kundi kubwa la vijana ambao kwa sasa halina fursa za ajira, pamoja na familia ambazo zinaendelea kuteseka kutokana na athari za myumbo wa uchumi kimataifa; changamoto na mwaliko kwa Jumuiya ya waamini kushirikishana fadhila ya upendo na mshikamano wa dhati.

Wanasiasa wajikite katika mchakato utakaoibua mbinu mkakati wa maboresho ya uchumi na hali ya wananchi wengi wanaoendelea kuogelea katika dimbwi la umaskini wa hali na kipato. Parokia mbali mbali nchini Italia, ziendelee kujenga na kuimarisha ari na mwamko wa kimissionari, kwa kushirikishana fadhila ya imani.

Ni mwaliko kwa wadau mbali mbali wa Uinjilishaji, kujikita katika ufundishaji makini wa Katekesi, itakayowasaidia waamini kukiri, kuadhimisha, kuimwilisha, kuisali na hatimaye kuitolea ushuhuda katika uhalisia wa maisha. Iwe ni fursa kugundua utambulisho wao wa Kikristo na mwaliko wa kumfuasa Kristo kwa moyo na ari kubwa zaidi hasa wakati huu Mama Kanisa anapoadhimisha Mwaka wa Imani.

Maaskofu wameangalia na kubainisha mikakati itakayotumika kwa ajili ya kuwaandaa vijana wanaotaka kumfuasa Kristo katika maisha ya Kipadre; Umuhimu wa kuwa na majiundo endelevu ya kipadre pamoja na kuendelea kuhimiza umuhimu wa vituo vya vijana Parokiani kama mahali pa majiundo ya Kikristo, bila kusahau huduma ya upendo na mshikamano kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.

Baraza la Maaskofu Katoliki Italia, limeaanza mchakato wa maandalizi ya Kongamano la Kitaifa litakalofanyika Jimboni Firenze kunako mwaka 2015. Wanaendelea kuunga mkono jitihada za vyama vya kitume vinavyotaka uhuru kamili katika masuala ya elimu na maisha ya binadamu, yanayopaswa kulindwa na kuthaminiwa tangu pale mtoto anapotungwa mimba tumboni mwa mama yake.

Maaskofu wanasema, wataendelea kuwa ni sauti ya kinabii miongoni mwa maskini na wahitaji, kamwe hawatanyamaza bali wataendelea kuwa ni Wasamaria wema, wanaosikiliza kwa makini; wanaoelimisha na kusaidia. Ubinafsi wa kukithiri ni kati ya mambo makubwa yanayosababisha myumbo wa kiuchumi, kimaadili na kiutu. Kama viongozi wa Kanisa, wataendelea kumtangaza Yesu Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu, kiini cha imani yao.

Ni matumaini ya watu wengi kwamba, kwa njia ya Kanisa, wanaweza kujenga na kuimarisha mahusiano yao ya Kijamii, kiasi hata cha kuweza kushirikisha utajiri na maisha yao ya kiimani. Hii ni changamoto kwa Parokia kuendelea kuwa kweli ni mahali pa kukuza na kudumisha ari na moyo wa kimissionari.

Mikakati ya kichungaji kuhusu familia ipewe kipaumbele cha kwanza kwani Familia ni Kanisa dogo la nyumbani; mahali ambapo watu wanaonja na kumegeana upendo na mshikamano wa dhati, kila mtu akiwajibika barabara. Jamii inapaswa kuwekeza katika familia kama njia ya kudhibiti athari za myumbo wa uchumi kimataifa nchini Italia.








All the contents on this site are copyrighted ©.