2013-02-09 13:39:13

Caritas MONA, kukutana ili kujadili mikakati ya kuwasaidia wakimbizi kutoka Mashariki ya Kati na Afrika ya Kaskazini


Shirikisho la Mashirika ya Misaada ya Kanisa Katoliki Mashariki ya Kati, na Kaskazini mwa Afrika, Caritas MONA, linalojumuisha mashirika 17, kuanzia tarehe 20 hadi 22 Februari, 2013 litakuwa na mkutano wake mkuu, utakaofanyika mjini Amman, nchini Yordani. Tatizo la wakimbizi Mashariki ya Kati ni kati ya ajenda kuu zitakazofanyiwa kazi na wajumbe 41 waliokwisha thibitisha kwamba, watashiriki.

Kardinali Robert Sarah, Rais wa Baraza la Kipapa linaloratibu misaada ya Kanisa Katoliki, Cor Unum anatarajiwa pia kushiriki katika mkutano huu. Hapo tarehe 19 Februari, Kardinali Sarah atatembelea Familia za wakimbizi kutoka Syria ili kushiriki pamoja nao shida na mahangaiko yao ya ndani. Wajumbe wa mkutano huu wanatarajiwa pia kukutana na Mfalme Abdallah wa Pili wa Yordan.

Wajumbe pia watapembua kwa kina na mapana mikakati ya shughuli za kichungaji na utekelezaji wake katika huduma kwa wakimbizi, wahamiaji na watu wasiokuwa na makazi maalum katika maeneo yao. Mateso na mahangaiko ya wakimbizi kutoka Syria ni changamoto kwa Kanisa na Jumuiya ya Kimataifa katika ujumla wake.







All the contents on this site are copyrighted ©.