2013-02-07 13:35:30

TANZIA: Askofu Msarikie wa Jimbo Katoliki Moshi, Tanzania amefariki dunia


Askofu mstaafu Amedeus Msarikie wa Jimbo Katoliki Moshi, Tanzania amefariki dunia Alhamisi, tarehe 7 Februari 2013 wakati akiwa anaendelea na matibabu Nairobi. Habari zimethibitishwa na Padre Anthony Makunde, Katibu mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania. Naye Askofu Isack Amani wa Jimbo Katoliki Moshi katika taarifa yake anasema, Jimbo Katoliki Moshi linaendelea kufanya utaratibu wa mipango ya mazishi na ikikamilika, taarifa rasmi itaweza kutolewa.
Marehemu Askofu Msarikie alizaliwa kunako mwezi Septemba 1931, Makundi, Kirua Vunjo Moshi, Kilimanjaro. Baada ya masomo na majiundo yake ya Kipadre, kunako tarehe 8 Agosti 1961 akapadrishwa. Tarehe 21 Machi 1986 akateuliwa na Baba Mtakatifu Yohane Paulo wa Pili kuwa Askofu Mpya wa Jimbo Katoliki Moshi.
Akawekwa wakfu kuwa Askofu wa Jimbo Katoliki Moshi tarehe Mosi Mei 1986. Baada ya kuwaongoza, kuwafundisha na kuwatakatifuza waamini wa Jimbo Katoliki Moshi, kama kiongozi wao mkuu, tarehe 21 Novemba 2007, akang’atuka kutoka Madarakani.







All the contents on this site are copyrighted ©.