Mshikamano wa upendo na watoto wa Kijiji cha Matumaini Dodoma
Mke wa Waziri Mkuu wa Tanzania Mama Tunu Pinda ametoa zawadi mbalimbali kwa watoto
zaidi ya 160 wanaoishi kwenye kijiji cha Matumaini ambacho kinalea watoto yatima eneo
la Kisasa, nje kidogo ya mji wa Dodoma.
Mama Pinda alizuru kijiji hicho kinacholea
watoto yatima Alhamisi, Februari 7, 2013 akiwa amefuatana na viongozi wa Umoja wa
Wanawake (UWT) mkoa wa Dodoma wakiongozwa na Mwenyekiti wa UWT wa mkoa huo, Bi. Salome
Kiwaya.
Akizungumza na watoto wa kituo hicho, Mama Pinda alisema ameamua
kuwatembelea watoto hao ili kuwasalimia na kuwatakia heri ya mwaka mpya 2013.
Mkurugenzi
wa kijiji hicho, Sista Rosalia Gargiulo wa Shirika la Masista Waabuduo Damu ya Yesu
alimshukuru Mama Pinda na viongozi wengine alioambatana nao kwa upendo wao na kwa
kutoa muda wao kuamua kuwatembelea na kuwafariji watoto hao.
Meneja mradi wa
kijiji hicho ambacho pia kinalea watoto wanaoishi na Virusi vya UKIMWI, Padre Vincent
Boselli, C.PP.S, alisema Kijiji hicho kilianzishwa mwaka 2002 kikiwa na watoto watatu
na sasa hivi kina watoto 161 wanaolelewa kituoni hapo kwa mtindo wa familia kwenye
nyumba 14 ambazo zina baba na mama wa kujitolea.
Zawadi hizo zenye thamani
ya sh. milioni 1.1 ni mbuzi wawili, mchele (kg. 50), sukari (kg. 25), unga wa mahindi
(kg. 50), mafuta ya kupikia (lita 40), katoni moja ya sabuni za miche, ndoo moja ya
sabuni ya unga, madaftari dazeni tisa, penseli 100, vichongeo 100 na rula 100. Nyingine
ni biskuti (katoni tatu), pipi (pakiti nne), juisi (katoni tisa) na khanga.