2013-02-05 11:57:29

Vatican na Italia yazindua Maadhimisho ya Miaka 84 ya Mkataba wa Laterano; uliotenganisha Kanisa na Serikali!


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, Siku ya Jumatatu jioni, tarehe 4 Februari 2013, amemshukuru Rais Giorgio Napolitano wa Italia kwa zawadi kubwa ya Tamasha la Muziki kama sehemu ya Maadhimisho ya Miaka 84 ya Mkataba wa Laterano. Amewashukuru wanamuziki wa "Flying Angels Foundation" ambao wamekuwa mstari wa mbele katika kusaidia shughuli mbali mbali za kijamii.

Anasema, muziki ni kielelezo makini cha majadiliano ya imani kati ya mwanadamu na Muumba wake; mwaliko na changamoto ya kutubu na kumwongokea Mungu, daima akitumaini huruma na upendo ambao Mwenyezi Mungu amekuwa akimwonesha mwanadamu katika hija ya maisha yake. Baba Mtakatifu anabainisha kwamba, hakuna jambo lolote lile linaloweza kumtenga mwanadamu na upendo wa Mungu, kama anavyo andika Mtakatifu Paulo kwa Warumi. Upendo huu unajionesha kwa namna ya pekee kwa njia ya Yesu Kristo.

Muziki huu umesheheni tunu msingi za kijamii zinazofumbatwa katika uhuru na usawa; sanjari na mapambano dhidi ya kifo, changamoto kwa waamini kuwa na matumaini ya maisha ya uzima wa milele baada ya kifo.

Kwa upande wake, Rais Giorgio Napolitano amemtakia Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, afya njema wakati huu wanapozindua kwa pamoja maadhimisho ya Kumbu kumbu ya miaka 84 tangu Mkataba wa Laterano uliopotiwa sahihi kati ya Serikali ya Italia na Kanisa Katoliki. Kumekuwepo na ushirikiano mwema kati ya Serikali ya Italia na Kanisa Katoliki, kwa ajili ya mafao ya wengi, kila upande ukiheshimu na kuthamini mchango unaotolewa kwa ajili ya wananchi wa Italia.

Rais Napolitano amekiri kwamba, miaka saba ya uongozi wake, imekuwa kweli ni ya shida na taabu, si tu kwa Italia, bali ni mwelekeo wa dunia nzima, lakini pia imekuwa ni fursa kwa viongozi hawa wawili kushirikishana uzoefu na mang'amuzi ya maisha yao kwa kusikilizana kwa dhati. Majadiliano yao ya mara kwa mara yamelenga zaidi na zaidi katika kudumisha misingi ya haki, amani, mafao ya wengi, utu na maadili mema.







All the contents on this site are copyrighted ©.