Awali ya yote niruhusuni nianze kwa kuwashukuru viongozi, wana-CCM na wakazi
wa Kigoma kwa mapokezi mazuri sana mliyonipa mimi na mke wangu Salma MNEC
wa Lindi Mjini tangu tulipowasili mkoani hapa. Nawapongeza kwa kukubali kuwa wenyeji
wa Sherehe za Kuadhimisha Miaka 36 ya Kuzaliwa kwa Chama cha Mapinduzi. Lakini pongezi
kubwa kwa kuandaa sherehe hii kwa mafanikio makubwa. Utaratibu mpya wa Katibu Mkuu
na Wajumbe wa Sekretariet kutembelea matawi, kuzungumza na wanachama na wananchi ni
wa aina yake. Ni mzuri na unafaa kuigwa.
Ni jambo la faraja na kujivunia kwamba
tunasherehekea Chama chetu kufikisha umri wa miaka 36 wakati kikiwa imara na nguvu
za kutosha za kupambana na kushinda katika mfumo wa vyama vingi uliodumu kwa miongo
miwili. Pia kwamba, nchi yetu na watu wake bado ni wamoja, na kuna amani na utulivu
licha ya kuwepo kwa changamoto ndogo na kubwa zinazotishia umoja na mshikamano wetu.
Ni jambo la kufurahisha na kutia moyo kwamba tunasherehekea miaka 36 ya Uhai wa CCM
wakati nchi ya Tanzania ikiendelea kupiga hatua kwa kasi katika kujiletea maendeleo.
Tena maendeleo yaliyo dhahiri na yanayoonekana na wote isipokuwa, labda, wale ambao
hutembea wakiwa wamefumba macho.
Wana CCM wenzangu; Uimara wa Chama
cha Mapinduzi na maendeleo yanayopatikana nchini chini ya uongozi wake ni uthibitisho
wa ubora wa sera zake na umakini wa viongozi wa CCM kuongoza Chama na kusimamia serikali
katika kutekeleza Sera na hasa Ilani za Chama cha Mapinduzi. Wana-CCM wenzangu tunayo
kila sababu ya kujipongeza na kutembea kifua mbele kwa mafanikio yaliyopatikana mpaka
sasa na yale yanayoendelea kupatikana ndani ya Chama na katika taifa. Wananchi wa
Tanzania nao hawana budi kujipongeza kwa uamuzi wao wa busara wa kukiamini Chama cha
Mapinduzi kiendelee kuongoza nchi yetu. Nawaomba waendelee na imani hiyo hiyo kwa
miaka mingi ijayo. Mimi nawaahidi kwa niaba ya Chama cha Mapinduzi, tena kwa kujiamini
kuwa hatutawaangusha.
Ndugu zangu, Wana-CCM wenzangu; Tuendelee kwa
ari zaidi na nguvu zaidi kujenga na kuimarisha Chama chetu. Hayo ndiyo maagizo ya
Mkutano Mkuu wa Taifa wa CCM uliofanyika tarehe 11 mpaka 13 Novemba, 2012 kule Kizota,
Dodoma. Hayo ni maagizo kwa Chama chenyewe na kwa Jumuiya zake. Maagizo ya kujijenga
na kujiimarisha yameainishwa vizuri katika Maazimio ya Mkutano Mkuu wa Taifa uliopita.
Lakini, hii si mara ya kwanza ni maagizo ya Mikutano Mikuu yote iliyopita, ya mradi
wa Kuimarisha Chama III na ya Mageuzi ya Ndani ya Chama yaliyoamuliwa na Halmashauri
Kuu ya Taifa katika Kikao chake cha Aprili, 2011. Maombi yangu kwa viongozi na
wanachama wenzangu wa CCM kote nchini ni kuhakikisha kuwa tunatekeleza kwa ukamilifu
maagizo hayo. Kwanza tuyasome na kuyaelewa vizuri na kupanga mipango na programu nzuri
za utekelezaji wake. Viongozi wa Chama tunao wajibu maalum wa kuwaongoza viongozi
walio chini yetu na wanachama wote katika kuelewa na kutekeleza Maazimio ya Mkutano
Mkuu wa Taifa uliopita, Mradi wa Kuimarisha Chama na Mageuzi ya Ndani ya Chama.
Ndugu
zangu; Tunayotakiwa kufanya si mageni. Ni mambo tunayoyajua na tumekuwa tunayafanya
lakini tunakumbushwa na kusisitiziwa kuhakikisha kuwa kila mmoja wetu anayafanya,
tena kwa ufanisi wa hali ya juu. Chama ni wanachama. Hivyo basi lililo la awali kabisa
ni kutambua kuwa lazima tuendelee kuongeza wanachama. Wanachama ndiyo Jeshi letu la
kutuletea ushindi. Ndizo kura zetu za uhakika za kuanzia. Hivi sasa kitaifa CCM
ina wanachama 6,042,791. Hizi ni kura nyingi kwa kuanzia. Tujitahidi tufikishe wanachama
milioni 8 mpaka 10 mwaka 2015. Hakuna wa kutushinda. Hivyo basi ni muhimu kuwa na
wanachama wengi wenye imani ya dhati kwa Chama chao. Wanachama wenye ufahamu mzuri
wa Sera za Chama na Serikali yake, wasiokuwa na ajizi katika kutekeleza Sera na maagizo
ya CCM na walio tayari kukisemea na kukitetea Chama cha Mapinduzi. Kuwa na viongozi
na wanachama ambao imani yao kwa Chama ni nusu nusu au uelewa wao wa mambo ni mdogo
na si makini katika kutekeleza wajibu wao ni jambo la hatari.
Kwa sababu
hiyo viongozi wenzangu na wanachama wenzangu hatuna budi kuongeza wanachama na kuhakikisha
kuwa tunawatayarisha vizuri kuelewa vyema Sera za Chama na wajibu wao kwa Chama chao.
Lazima tujipange vyema kuzitekeleza na kushiriki kwa ukamilifu katika utekelezaji
wake. Suala la elimu kwa wanachama wetu na kujipangia majukumu ya kufanya ndani ya
Chama na katika jamii lilisisitizwa sana katika Mkutano Mkuu wa Taifa uliopita na
katika mradi wa kuimarisha Chama na malengo ya mageuzi ya ndani ya Chama. Haya shime
tutekeleze.
Viongozi kutembelea wanachama wetu na kuzungumza nao, kuwaelimisha
na kufafanua mambo mbalimbali ya Chama na Serikali na kuwaelekeza wajibu wao ni jambo
la lazima kufanya. Hali kadhalika, viongozi lazima tuwatembelee wananchi kufafanua
Sera za Chama chetu na masuala yahusuyo nchi yetu na serikali. Pia tuwasikilize mambo
wanayotaka kupatiwa ufumbuzi au ufafanuzi. Yale mambo tunayoyaweza tuyajibu na yale
tusiyoyaweza tuondoke nayo tukayatafutie majibu kisha tuwape taarifa.
Ni
kwa kufanya hivyo tu Chama chetu kitajijengea uhalali wa kuendelea kuongoza taifa
kwani watu watatuamini na kutupenda. Tusipowatembelea wananchi na kuzungumza nao
tunaacha ombwe linalojazwa na wale wasiokitakia mema Chama cha Mapinduzi. Watu wanaopotosha
wananchi na kupandikiza chuki dhidi ya Chama chetu na serikali yake. Wengine wanaweza
hata kuchukua sifa zetu isivyostahili na kujifanya ni wao waliofanya au kusababisha
yawepo.
Hali kadhalika tuhakikishe kuwa vikao vinafanyika ili viongozi wapate
fursa ya kuzungumza mambo yahusuyo ujenzi wa Chama chao na kupanga mikakati na mbinu
za kutekeleza wajibu wao. Miongoni mwa mambo ambayo Chama chetu lazima kiyape kipaumbele
cha juu ni pamoja na kujenga uwezo wa kujitegemea katika kila ngazi. Jambo hili tumelisemea
kwa muda mrefu lakini hakuna kitu cha maana kinachoonekana kufanyika. Wakati umefika
wa kulipa uzito unaostahili suala la kujitegemea. Tusilipuuze jambo hili muhimu kwa
uhai wa Chama chetu vinginevyo mambo mengi yatatushinda kufanya na Chama kitadorora
na kudhoofika.
Wapo baadhi ya wenzetu wamefanikiwa katika hili ndani ya Chama
na Jumuiya. Tuwatambue na kuwasiliana nao ili watupe maarifa ya kufanya hivyo. Jambo
hili si la hiari tena. Ni lazima tuhakikishe tunaulizana katika kila kikao. Viongozi
wenzangu na Wana-CCM wenzangu; Miongoni mwa maagizo na maelekezo makuu na ya msingi
sana ya Mkutano Mkuu wa Taifa ni Umoja wa Chama chetu. Mkutano Mkuu wa Taifa umetutaka
viongozi tuwe wamoja, wanachama tuwe wamoja na viongozi na wanachama hali kadhalika.
Tushikamane kwa pamoja kujenga Chama chetu kueneza sera, kutekeleza sera na
kukipigania Chama chetu. Ndiyo maana kauli mbiu ya Chama chetu iliyotoka katika
mkutano ule ilikuwa Umoja ni Ushindi. Ndiyo Kauli Mbiu ya maadhimisho haya ya miaka
36 ya kuzaliwa kwa CCM na ndiyo Kauli Mbiu mpaka itakapotengenezwa nyingine.
Umuhimu
wa umoja hauhitaji kuelezwa kwa muda mrefu. Sote tunaijua misemo ya wahenga isemayo
Umoja ni Nguvu, Utengano ni Udhaifu au Nguvu ya Mnyonge ni Umoja na kadhalika. Umoja
ndiyo uliowawezesha wazee wetu kuongoza harakati za kudai uhuru wa nchi yetu na kushinda.
Kina Saadani, Abdul Kandoro, Alhaji Tawakal Karago na wenzao wengi hawakuwa na nguvu
za fedha wala silaha bali umoja wao ndiyo uliyoiletea nchi yetu uhuru. Wakati mwingine
husononeka sana ninapoona viongozi na wana-CCM wakifanya vitendo vinavyovuruga umoja
na mshikamano ndani ya Chama. Nawaomba wenzangu tulinde umoja wa ndani ya Chama cha
Mapinduzi kama mboni ya macho yetu. Tukiwa na umoja wana-CCM tutapendana, tutazungumza
lugha moja, tutashirikiana vyema kupigania Chama chetu na kuwapigania wagombea wa
Chama chetu kwenye chaguzi za dola.
Pasipokuwa na umoja yote hayo hayawezekani.
Na ninyi wa Kigoma mnajua ukweli wa athari zake. Tumepoteza majimbo matano kwa sababu
ya mifarakano ndani ya Chama chetu. Tunataka kuyakomboa majimbo yetu. Tutafanya
hivyo tu iwapo tutakuwa wamoja na tuna mshikamano ndani ya Chama chetu. Tunataka
kuyakomboa majimbo yetu. Tutafanya hivyo tu iwapo tutakuwa wamoja na tuna mshikamano
wa dhati. Ni imani yangu kuwa sherehe hizi na kazi nzuri aliyofanya Katibu Mkuu Abdulrahman
Kinana, Naibu Katibu Mkuu, Mwigulu Nchemba, Katibu wa Siasa na Mambo ya Nje, Dkt.
Asha-Rose Migiro na Katibu wa Uenezi Nape Moses Nnauye itakuwa chachu itakayotufikisha
katika matumaini yetu hayo.
Ndugu Viongozi na Wana-CCM wenzangu;
Jambo lingine muhimu sana ambalo hatuna budi kulisimamia kwa ufanisi mkubwa ni utekelezaji
wa Ilani ya Uchaguzi, ahadi za Chama chetu na wagombea wetu wakati wa uchaguzi na
kuyapatia ufumbuzi matatizo ya wananchi. Lazima tukumbuke kuwa Ilani ya Uchaguzi
ndiyo mkataba rasmi baina ya wananchi wa Tanzania na Chama cha Mapinduzi walipotuchagua
mwaka 2010 tuendelee kuongoza nchi yetu.
Ilani ya Uchaguzi hujumuisha
mambo ambayo tumewaahidi Watanzania tutayafanya. Wakatuamini wakatuchagua. Ahadi
ni deni, lazima tulipe. Lakini pia zipo ahadi za papo kwa papo nilizotoa mimi, alizotoa
mgombea mwenza, walizotoa wagombea wetu wa ngazi mbalimbali na viongozi wa Chama wa
ngazi mbalimbali. Hizo nazo lazima tuzitimize. Jambo lililo muhimu ni kuzitambua
ahadi hizo na kuzitengenezea mipango ya kuzitekeleza. Mimi hufurahi sana viongozi
na wananchi wanaponikumbusha ahadi za papo kwa papo tulizotoa ili tuzitekeleze.
Wana-CCM wenzangu; Napenda kuwahakikishia kuwa mimi na wenzangu Serikalini
tunaitekeleza vyema Ilani ya Uchaguzi mliyonikabidhi mimi na Makamu wa Rais, Dkt.
Mohamed Ghalib Bilal na Rais wa Zanzibar Dkt. Ali Mohamed Shein kuinadi na baada ya
ushindi kuitekeleza. Nawaahidi kuwa hatutawaangusha katika hilo kwani hatupendi kusutwa
na wala hatupendi Chama chetu tunachokipenda sana kinyooshewe kidole au kilaumiwe
kwa kutokutimiza ahadi.
Tunaendelea kwa mafanikio makubwa kutekeleza
mambo tuliyoahidi katika Ilani ya Uchaguzi. Tumepanua sana fursa ya elimu katika ngazi
zote kuanzia ya msingi, sekondari, ufundi stadi na vyuo vikuu. Tuelekeze nguvu zetu
katika kuimarisha ubora wa elimu kwa maana tumeongeza vyuo vya ualimu na idadi ya
wahitimu ili kukabili upungufu wa walimu nchini. Tunaendelea kuongeza maabara, vifaa
vya kufundishia na vitabu ili kuboresha elimu inayotolewa. Vilevile tunaendelea kusogeza
kwa wananchi huduma ya afya kwa kuongeza idadi ya zahanati, vituo vya afya na hospitali.
Tumeanza kuona dalili njema kwani vifo vya watoto na wajawazito imeanza kupungua.
Hivi sasa juhudi kubwa zinafanyika kudhibiti magonjwa yanayoua watu wengi kama vile
Malaria na UKIMWI.
Sambamba na juhudi hizo, tunaendelea kuboresha miundombinu
na upatikanaji wa umeme, maji na huduma nyingine za jamii. Tunaelekea kufikia lengo
letu la barabara kuu zote kuwa za lami na kuunganisha mikoa yote kwa barabara za lami.
Ujenzi wa barabara zenye urefu wa kilometa 11, 154 kwa kiwango cha lami na madaraja
makubwa na madogo unaendelea katika sehemu mbalimbali hapa nchini. Ninyi wa Kigoma
ni mashahidi wa kazi hiyo. Barabara ya Kigoma – Kidahwe - Uvinza inaendelea kujengwa.
Daraja la Mto Malagarasi, ujenzi wake unakwenda vizuri.
Na kwa upande wa
Tabora nako ujenzi wa barabara za lami umeanza mambo ambayo yanaihakikishia Kigoma
barabara nzuri kutokea Pwani. Hatujaisahau barabara ya Kidahwa-Nyakanazi. Tunaendelea
kutafuta fedha kutoka kwa marafiki lakini wenyewe tutaanza kidogo kidogo mwaka huu
kuelekea Kasulu. Hapa mjini tutaendelea kuongeza barabara za lami.
Nafahamu
kuwa ujenzi wa barabara Gungu-Airport, Job Lusinde na Mji Mwema umechelewa. Nimehakikishiwa
kuwa kasi itaongezeka. Pia tutaijenga kwa kiwango cha lami barabara ya Gungu-Tibirizi.
Ujenzi na uboreshaji wa viwanja vya ndege unaendelea katika mikoa mbalimbali. Kiwanja
cha Songwa kimekamilika na kesho nitaweka jiwe la msingi la ukarabati na upanuzi wa
Kiwanja cha Ndege cha Kigoma.
Ndugu Wananchi; Kama alivyoeleza Waziri Harrison
Mwakyembe mipango yetu haiishii hapa. Tutaendelea kukipanua kiwanja hiki hadi kifikie
kilometa 3 ili ziweze kutua ndege kubwa zaidi. Narudia kusema nia yangu ya kuona
siku moja Kiwanja cha Ndege cha Kigoma kinakuwa kitovu cha usafiri wa anga kwa nchi
za Maziwa Makuu. Inshallah heri.
Safari za treni ya Reli ya Kati zimeanza
na tayari mipango ya kuagiza mabehewa mapya na vichwa vya treni vipya kutoka nje inakamilishwa
ili kuboresha huduma hiyo. Kama mambo yataenda kama tunavyotarajia ifikapo mwishoni
mwa mwaka huu hali ya usafiri itakuwa bora sana. Pia tunaendelea kuboresha reli yenyewe
na tuna mipango ya kujenga reli mpya pana zaidi itakayofika mpaka Msongati, Burundi
kutokea Uvinza.
Vile vile tumeendelea kuchukua hatua za kuongeza uzalishaji
na usambazaji wa umeme nchini. Tunaendelea kutekeleza lengo la Ilani ya Chama chetu
ifikapo mwaka 2015 asilimia 30 ya Watanzania wawe wamefikiwa na huduma ya umeme.
Hivi sasa tumefikia asilimia 18 kutoka asilimia 10 mwaka 2005. Ninyi ndugu wa Kigoma
mmenufaika na mpango huu.
Kigoma, Kasulu na Kibondo mmepata mitambo mipya
ya kuzalisha umeme. Mwaka huu tutaanza kujenga njia ya kusafirisha umeme kutoka Kibondo
kwenda Kakonko. Suala la umeme kwa upande wa Uvinza nimelisikia nitawatuma wahusika
wafuatilie ili umeme upatikane saa 24 na kwa bei nafuu. Nawaomba viongozi wa CCM
muwe mstari wa mbele kuyasemea mafanikio haya. Msiposema wapo wanaosema na kuchukua
sifa yetu wakabeba wao.
Ndugu wananchi; Jana jioni nilipokea
risala ya wazee wa Kigoma. Katika risala yao wazee wamenipongeza kwa kasi ya maendeleo
inayopata Mkoa wa Kigoma katika nyanja mbalimbali. Nawashukuru kwa maneno ya faraja
inatupa moyo; kwani wapo wenzetu wengine hapa nchini tumewafanyia mambo mengi lakini
wagumu hata kusema asante. Wamebakia kulaumu kwa yale mapya wanayoyataka, tena kwa
lugha chafu. Wazee pia wameniomba nihamie Kigoma nitakapostaafu, au nijenge nyumba
ya kupumzikia hapa Kigoma. Nawashukuru kwa moyo wao wa upendo na ukarimu nitafikiria
ingawaje sijajua nani atanipa eneo la kujenga.
Ndugu wananchi;
Katika risala yao wazee wameelezea pia kwamba hali ya upatikanaji wa maji bado haijatengemaa.Watu
wanapata maji kwa mgao na Mbunge akaongezea kuwa bei imepanda sana na watu hutakiwa
kulipa hata kama maji hawakupata inavyostahili. Nilimuita Mkurugenzi Mkuu wa KUWASA
kutaka maelezo na mipango ya kupata ufumbuzi.
Katika maelezo yake
Mkurugenzi wa KUWASA amekiri kuwepo kwa mgao wa maji na kupanda kwa bei ya maji.
Mgao upo kwa sababu ya chanzo kilichopo sasa kuwa kidogo hivyo kuleta maji kidogo
kuliko mahitaji. Mahitaji ya maji kwa mji wa Kigoma/Ujiji ni mita za ujazo 26,000
kiasi kinachopatikana sasa ni mita za ujazo 15,000. Hivyo kuna upungufu wa mita za
ujazo 11,000.
Lakini Mkurugenzi alinipa habari njema kwamba upo mradi
unafadhiliwa na Benki ya Dunia ikishirikiana na Wizara ya Maji utakaomaliza tatizo
hilo. Kitajengwa chanzo kipya cha kutekea na kusafishia maji katika eneo la Amani.
Upatikanaji wa maji utaongezeka na kufikia mita za ujazo 42,000 hivyo kuzidi mahitaji
ya sasa kwa mita za ujazo 16,000 ambazo zitatosheleza mahitaji ya mji wa Kigoma mpaka
mwaka 2030.
Yatajengwa matanki ya kuhifadhi na kusambaza maji matano huko
Mnarani, Chungu, Kigoma Sekondari, Mlole na Mji Mwema. Pia mabomba mapya makubwa
ya urefu wa kilometa 70 yatatandazwa kote mjini na watu 10,000 kuunganishwa na kufungiwa
mita. Kuhusu bei ya maji alisema malalamiko yataisha pindi kila mtumiaji atakapofungiwa
mita na kulipa kadri anavyotumia. Heri sasa wamewafikia asilimia 54 ya wateja na
mipango ya kuwafungia mita watumiaji waliosalia inaendelea.
Ndugu wananchi;
Wazee wetu hao pia walilalamikia bei ya viwanja kuwa kubwa mno kwa mtu wa kawaida
kumudu, pembejeo za kilimo za ruzuku kutokutosheleza mahitaji na kuchelewa kupatikana
na mengineyo. Nimeahidi kuwa mamlaka husika zitataarifiwa kuyatafutia ufumbuzi masuala
hayo. Vile vile wazee wa Kigoma walitahadharisha kuhusu kuwepo migogoro kidogo na
kuhatarisha amani ya Mkoa na taifa kwa ujumla.
Nakubaliana nao kwamba ni
kweli ipo na inaelekea kuibuka kila kukicha na ni kweli kwamba ni hatari kwa amani
na utulivu hapa nchini. Nimelisema jambo hili mara baada ya Uchaguzi wa 2010 lakini
wapo waliojaribu kunibeza na kudai kuwa si kweli. Watanzania wenzangu haitasaidia
kujifanya haipo wakati ipo tunaiona na kuisikia. Nilisemea jambo hili tena katika
hotuba yangu ya mwisho wa mwaka kuomba viongozi wa dini watusaidie.
Kama
wao watawakemea na kuwakataza waumini wao, magazeti yao na radio zao zisilete mifarakano
ya kidini haitatokea. Niliwaomba wafufue utaratibu mzuri wa mazungumzo baina ya viongozi
wa dini ya Kikristo na Kiislamu. Ulikuwa utaratibu wao si wa serikali. Ukitumika
vizuri utatuepusha na mengi. Nawaomba waione haraka ya kufanya hivyo. Serikali
itatimiza wajibu wake wa kulinda amani kama hapana budi. Lakini, mzuie tusifikie hapo.
Ndugu wananchi; Kabla ya kumaliza napenda kuwasihi viongozi na
wafuasi wa vyama vya siasa kuacha kushabikia siasa za kuigawa nchi yetu katika makundi
ya dini, rangi, kabila na mahali anapotoka mtu. Naomba tushabikie sera zinazojenga
umoja na mshikamano badala ya migawanyiko na mifarakano.
Ni siasa na sera
ambazo hazina faida yeyote kwa nchi yetu na watu wake. Ni siasa za maangamizi na mifano
ipo mingi duniani na hata nchi jirani ya kuthibitisha hayo. Inashangaza kuona baadhi
ya wanasiasa wanafanya siasa za chuki kuwa mtaji wao wa kisiasa. Nawaambia hawatafika
popote. Nawaomba Watanzania wenzangu msikubali kutumiwa na wanasiasa au mtu yoyote
mwenye sera za aina hiyo. Wanaendeleza maslahi yao binafsi na siyo ya taifa. Msikubali
kuweka rehani maisha yenu na amani ya nchi yetu kwa ajili ya maslahi ya mtu au kikundi
fulani. Jiulizeni hivi, nchi hii ikichafuka mimi na familia yangu tutaokolewa na nani?
Ndugu viongozi na wanaCCM wenzangu; Mwisho, napenda kuchukua nafasi hii kuwapongeza
sana wenyeji wetu wakiongozwa na Mwenyekiti wa CCM wa Mkoa Ndugu Kaburu, na wale wote
walioshiriki kuandaa sherehe hizi ambazo zimefana sana. Nawashukuru pia wanachama
wa CCM na wananchi kwa ujumla kwa kujitokeza kwa wingi kushiriki matembezi ya mshikamano
leo asubuhi na sasa katika kilele cha sherehe hizi. Sina neno zuri la kushukuru zaidi
ya kusema asanteni sana.
Nawapongeza tena viongozi, wanachama,
makada, wapenzi na wakereketwa wa CCM kwa kutimiza miaka 36 ya uhai wa CCM. Nawasihi
tutoke hapa tukiwa na ari zaidi, nguvu zaidi na kasi zaidi ya kwenda kukijenga Chama
chetu kote nchini na kuwatumikia wananchi. Daima tukumbuke Umoja ni Ushindi na kwa
pamoja tutashinda. Kidumu Chama Cha Mapinduzi! Asanteni sana kwa kunisikiliza.