2013-02-05 07:22:16

Kanisa linapania kuwekeza katika "vijiwe vya vijana" kama sehemu ya mkakati wa Uinjilishaji mpya!


Kardinali Gianfranco Ravasi, Rais wa Baraza la Kipapa la Utamaduni, tarehe 6 Februari 2013 anatarajiwa kufungua mkutano mkuu wa Baraza hili, kwenye kikao cha wazi, kitakachowashirikisha wadau mbali mbali wanaojishughulisha na utume na shughuli za kichungaji kwa vijana wa kizazi kipya. Mkutano huu utafanyika kwenye Ukumbi mkubwa wa Chuo Kikuu cha LUMSA hapa Roma. RealAudioMP3

Mkutano unapania kuangalia masuala mbali mbali yanayogusa utamaduni na lugha ya vijana wa kizazi kipya, ambao wengi wao wanapatikana katika Mitandao ya Kijamii.

Mada zinazotarajiwa kujadiliwa ni pamoja mwingiliano wa kijamii miongoni mwa vijana; vijana wanaoishi katika mitandao ya kijamii, lugha na ibada yao. Wajumbe watapata fursa ya kujadili kwa undani zaidi kuhusu imani miongoni mwa vijana, hapa vijana watatoa ushuhuda wa imani yao kadiri ya maisha yao na shughuli mbali mbali ambazo zimewasaidia kukuza na kuimarisha imani hii licha ya kinzani na migogoro mbali mbali wanayokabiliana nayo katika hija ya maisha ya ujana.

Wajumbe pia watajadili mbinu mkakati wa kuwaelimisha vijana katika vionjo vyao. Mwishoni, ratiba inaonesha kwamba, wajumbe hawa watajadili kwa kina na mapana kuhusu imani kwa ujumla na mapambano katika utamaduni. Baraza la Kipapa la Utamaduni, litajadili pia mada zitakazojadiliwa kwenye mkutano wake mkuu ujao.

Baraza la Kipapa la Utamaduni katika utekelezaji wa mikakati yake ya kichungaji kwa Mwaka 2013, linapenda kuwekeza zaidi katika maisha na utume wa vijana hasa kwenye “Vijiwe vyao” ili waweze kupata fursa ya kuimarisha imani na matumaini yao kwa Kanisa, kama njia ya ujenzi wa utamaduni wa mawasiliano na urafiki kati ya vijana wa kizazi kipya na Kanisa.
Kardinali Gianfranco Ravasi, Rais wa Baraza la Kipapa la Utamaduni, wakati wa kuwasilisha tema itakayofanyiwa kazi na Baraza lake katika mkutano mkuu unaoanza hapo tarehe 6 hadi 9 Februari, 2013, aliambatana na viongozi waandamizi kutoka katika Baraza la Kipapa la Utamaduni pamoja na vijana, ambao wametoa ushuhuda kuhusu maisha na utume wao katika ulimwengu wa vijana mamboleo, wanaopatikana kwa wingi katika Majukwa ya Mitandao ya Kijamii.
Vijana hao kutoka Italia na Madagascar, wanaosoma kwenye Vyuo Vikuu vya Italia wanabainisha kwamba, katika hija ya maisha yao ya kiimani, wamebahatika kushuhudia matukio mbali mbali yaliyogusa undani wa maisha yao, kiasi kwamba, yameacha chapa ya kudumu kama njia ya ushuhuda wa kujenga urafiki, upendo na mshikamano katika hija ya maisha ya kiroho miongoni mwa vijana.
Hii sehemu ya mchakato wa Uinjilishaji Mpya, unaogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili. Ni kweli kabisa kwamba, kuna umati mkubwa wa vijana unaopatikana katika Majukwa ya Mitandao ya Kijamii, lakini pia kuna mamillioni ya vijana ambao bado wanaendelea na maisha yao ya kila siku pasi na kuguswa na mitandao hii.
Kumbe, Kanisa linapaswa kuwa na mwelekeo mpana linapowahangaikia vijana katika hija ya maisha yao ya kila siku: kwa kuwatafuta kwenye Majukwaa ya Mitandao ya Kijamii bila kusahau kwamba, bado kuna wengine wako “Vijiweni” kama kawaida!. Jamii ijitahidi kufahamu ulimwengu unaowazunguka vijana, badala ya kubakia wakielea juu juu bila kuzama katika maisha, matumaini, kinzani, changamoto na matarajio yao kwa siku za usoni.
Vijana wanamshukuru Baba Mtakatifu kwa kujimwaga katika Mitandao ya Kijamii, lakini Kanisa bado linawajibika kuwekeza zaidi katika mitandao ya Kijamii ili kuweza kukutana na vijana wanaoendelea kujitosa huko wakiwa na sababu mbali mbali, ili waweze kukutana nao, hatimaye, kuwamegea cheche za imani zitakazowasha na kukoleza imani yao kwa Kristo na Kanisa lake. Kanisa lijitahidi kufahamu lugha ya vijana wa kizazi kipya na kuifanyia kazi, kwani ni lugha inayogusa undani wa mtu mzima: kiroho na kimwili.
Matumizi ya Mitandao ya Kijamii miongoni mwa Vijana wa kizazi kipya ni fursa ya kukutana na watu mbali mbali na hivyo kuanza kujenga mahusiano katika medani mbali mbali za maisha. Mitandao inapunguza umbali na vikwazo ambavyo kwa miaka mingi vijana walikumbana navyo katika maisha yao! Hapa ni mahali pa kujimwaga kisawa sawa na kwamba, watu wanatafuta majibu ya haraka na yenye kusheheni kweli za Kiimani kutoka katika Kanisa.
Umefika wakati kwa Mama Kanisa kuonesha ule umahiri wa kuiwezesha Imani kutembea katika mitandao ya Kijamii, ili vijana waweze kufaidika na maendeleo haya ya teknalojia ya mawasiliano na habari kama sehemu ya mchakato wa kukua katika imani, matumaini na mapendo.








All the contents on this site are copyrighted ©.