2013-02-04 09:54:11

Wananchi wengi wa Syria wanatamani kuona haki, amani na utawala wa sheria vinaheshimiwa nchini humo!


Vita na kinzani za Kijamii zinazoendelea nchini Syria zinapelekea watu wasiokuwa na hatia kuendelea kupoteza maisha yao. Umefika wakati kwa wahusika wa pande zote mbili zinazosigana nchini humo kuweka silaha chini na kuanza mchakato wa majadiliano ya kisiasa ili haki, amani na utulivu viweze kutawala tena nchini Syria.

Taarifa za Umoja wa Mataifa zinaonesha kwamba, kuna watu zaidi ya watu 60,000 wamekwisha kupoteza maisha kutokana na vita nchini Syria. Kuna watu wengine zaidi ya millioni moja wamelazimika kuyakimbia makazi yao na kwa sasa hawana makazi maalum. Hali ya ulinzi na usalama nchini Syria ni tete kutokana na ukweli kwamba, watu wengi wanamiliki silaha kali zinazotishia maisha ya watu. Ni kwa njia ya majadiliano ya kisiasa, Syria inaweza kupata ufumbuzi wa mgogoro wake.

Ni changamoto iliyotolewa hivi karibuni na Dr. Haytham Al-Manna moja ya wanaharakati wa kutetea haki msingi za binadamu alipokuwa anazungumza na viongozi wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni, kwenye Makao yake mjini Geneva, hivi karibuni. Ni ndoto ya wananchi wengi wa Syria kwamba, nchi yao siku moja itakumbatia demokrasia kwa kutambua kwamba, ni nchi ambayo ina tofauti kubwa za kidini na kikabila.

Baraza la Makanisa Ulimwenguni linajiandaa kuadhimisha Mkutano wake mkuu, Mwezi Oktoba, Korea ya Kusini, kwa kujikita zaidi katika masuala ya haki na amani.







All the contents on this site are copyrighted ©.