Maadhimisho ya Siku ya Watawa Duniani nchini Malawi
Baraza la Maaskofu Katoliki Malawi linamshukuru Mungu kwa kuliwezesha kupata miito
mbali mbali ya maisha ya kitawa, linaendelea kusali kwamba, waamini wengi wataweza
kutajirishwa na ushuhuda wa maisha na utume unaotolewa na watawa nchini humo. Itakumbukwa
kwamba, Siku ya Watawa Duniani, inaadhimishwa kila Mwaka ifikapo tarehe 2 Februari,
Sanjari na Siku kuu ya kutolewa Bwana Hekaluni. Ni Siku inayomwonesha Kristo Mwanga
wa Mataifa, changamoto kwa watawa pia kuwa kweli ni mwanga wa mataifa kwa njia ya
ushuhuda wa maisha yao. Kanisa Katoliki nchini Malawi linatambua na kuthamini mchango
wa Watawa katika maisha na utume wa Kanisa. Huu ni ujumbe kutoka kwa Askofu Thomas
Msusa, Mwenyekiti wa Tume ya Watawa, Baraza la Maaskofu Katoliki Malawi, katika Maadhimisho
ya Siku ya kumi na saba ya Watawa Duniani. Siku kuu ya kutolewa Bwana Hekaluni,
alisema Mwenyeheri Yohane Paulo wa pili ni kielelezo makini cha watawa wanaojitoa
bila ya kujibakiza kwa ajili ya Mungu na jirani zao; kwa njia ya Mashauri ya Kiinjili;
yaani: Ufukara, Utii na Usafi kamili. Kuna umuhimu wa kuendelea kuadhimisha Siku ya
Watawa Duniani kama kielelezo cha Kanisa kutambua na kuthamini maisha ya kitawa yanayojionesha
kwa njia ya karama mbali mbali ambazo Roho Mtakatifu amelijalia Kanisa, kwa ajili
ya ujenzi wa Ufalme wa Mungu. Hizi ni karama zinazojionesha kwa namna ya pekee
katika huduma katika sekta ya: elimu, afya, maendeleo ya kijamii na majitoleo kwa
wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Watawa wamekuwa mstari wa mbele kushirikisha
sala na imani yao kwa njia ya ushuhuda wa maisha, lakini zaidi pale wanapotangaza
Injili na kuadhimisha Mafumbo ya Kanisa kwa ajili ya Watu wa Mungu. Maadhimisho
ya Siku ya Watawa Duniani yawasaidie waamini kupata ufahamu mpana zaidi kuhusu Mashirika
ya Kitawa na Kazi za Kitume na jinsi ya kukabiliana na changamoto za maisha ya kiimani.
Watawa wanapaswa kutambua kwamba, mchango wao ni muhimu sana katika maisha na utume
wa Kanisa. Watawa wawe ni mfano wa kuigwa katika utamaduni wa Kusikiliza Neno la Mungu
na Maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu; chem chemi ya upendo na majitoleo makini.
Wawe ni mashahidi wa uwepo wa Mungu kati ya watu wake. Maadhimisho ya Siku ya Watawa
Duniani kwa Mwaka 2013 yamekwenda sanjari na Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, changamoto
ya kutambua kwamba, huu ni muda muafaka wa kufanya toba, wongofu wa ndani na kuendelea
kuchuchumilia utakatifu wa maisha; kwa kujitahidi kumwilisha Mashauri ya Kiinjili
katika hija ya maisha yao ya kila siku; wakiimarishwa kwa fadhila za imani, matumaini
na mapendo kama njia ya kujishikamanisha na Mwenyezi Mungu.
Ndivyo Askofu
Thomas Msusa anavyohitimisha ujumbe wake katika Maadhimisho ya Siku ya Watawa Duniani,
iliyoadhimishwa, hapo tarehe 2 Februari 2013.