Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, amemtumia salam za rambi rambi Kardinali
Norbert Rivera Carrera wa jimbo kuu la Mexico kutokana na moto mkubwa uliotokea kwenye
Jengo la Makao Makuu ya Kampuni ya Mafuta Pemex inayomilikiwa na Serikali ya Mexico
kati kati ya mji na hivyo kusababisha zaidi ya watu 33 kupoteza maisha yao na wengine
zaidi ya 121 kujeruhiwa vibaya, mapema siku ya Ijumaa, tarehe 1 Februari 2013.
Ujumbe
wa Baba Mtakatifu umeandikwa kwa niaba yake na Kardinali Tarcisio Bertone, Katibu
mkuu wa Vatican, akionesha ukaribu wake kwa njia ya sala kwa wote waliofikwa na msiba
huu. Ni matumaini ya Baba Mtakatifu kwamba, wahanga waliosalimika wataweza kupata
msaada wa hali na mali kutoka kwa Wasamaria wema. Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi
na sita, anawaweka marehemu wote chini ya ulinzi na maombezi ya Bikira Maria wa Guadalupe.