2013-02-02 08:31:24

Patriaki Louis Raphael Sako wa Kwanza achaguliwa kuongoza Kanisa la Babiloni ya Wacaldei


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, ameridhia uchaguzi wa Patriaki Louis Raphael Sako wa kwanza wa Kanisa la Babiloni ya Wacaldei, uliofanyika katika maadhimisho ya Sinodi ya Kanisa hili iliyoitishwa na Baba Mtakatifu na kusimamiwa na Kardinali Leonardo Sandri, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Makanisa ya Mashariki. Kabla ya kuchaguliwa kwake, Askofu mkuu Louis Sako, alikuwa ni Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Kerkut ya Wacaldei. Patriaki mpya anachukua nafasi ya uongozi iliyoachwa wazi na Patriaki Emmanuel Delly wa tatu. Na tangu sasa ataitwa Patriaki Louis Raphael Sako wa Kwanza.

Patriaki Sako wa Kwanza alizaliwa kunako tarehe 4 Julai 1948 huko Zakho, Iraq. Baada ya masomo na majiundo yake ya Kikasisi, akapewa daraja Takatifu la Upadre hapo tarehe 1 Juni 1974. Tangu wakati huo alitekeleza majukumu yake ya kichungaji hadi kunako mwaka 1979 alipotumwa Mjini Roma ili kuendelea na masomo ya juu na hatimaye, kujipatia Shahada ya uzamivu katika Mafundisho ya Mababa wa Kanisa. Baadaye alijiendeleza pia katika masomo ya historia na kujipatia Shahada ya pili ya Uzamivu katika Historia huko Paris, Ufaransa.

Baada ya Masomo yake, kunako Mwaka 1986 alirudi mjini Mossul na kuteuliwa kuwa Paroko wa Parokia ya Bikira Maria msaada wa daima. Kati ya Mwaka 1997 hadi mwaka 2002 alikuwa ni Gombera wa Seminari mjini Baghdad. Akarudi tena Mossul na kuendelea na huduma yake ya Uparoko, hadi tarehe 27 Septemba 2003 alipoteuliwa kuwa ni Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Kerkuk na akawekwa wakfu kuwa Askofu mkuu hapo tarehe 14 Septemba 2003.







All the contents on this site are copyrighted ©.