2013-02-01 09:22:23

Maadhimisho ya Siku ya Watawa Duniani 2013


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, katika maadhimisho ya Siku kuu ya Kutolewa Bwana Hekaluni, inayoadhimishwa kila mwaka ifikapo tarehe 2 Februari ya kila mwaka, anatarajiwa kuongoza Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro, mjini Vatican kwa ajili ya Watawa wa Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume. Ibada hii itafanyika majira ya jioni.

Baba Mtakatifu katika Waraka wake kuhusu Mwaka wa Imani, "Porta Fidei" Mlango wa Imani anabainisha kwamba, kwa njia ya imani, kuna watu ambao wamewekwa wakfu kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake; wakaacha yote ili kuanza kujikita katika mashauri ya Kiinjili, yaani: utii, ufukara na usafi kamili. Hawa ni kielelezo makini cha wale wanaomsubiri Kristo ambaye, kamwe hatachelewa kurudi.

Siku ya Watawa Duniani ilianzishwa na Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili, yapata miaka kumi na saba iliyopita, ili kutoa nafasi kwa Mama Kanisa kumshukuru Mungu kwa zawadi ya maisha ya kitawa, watu ambao ni mfano na kielelezo cha kuigwa. Ni nafasi pia ya kuombea miito mbali mbali ndani ya Kanisa.







All the contents on this site are copyrighted ©.