Tamko la Waziri Mkuu Mizengo Pinda kuhusu Gesi, Mtwara
TAARIFA KUHUSU ZIARA YA MHESHIMIWA MIZENGO P. PINDA (MB.) WAZIRI MKUU WA JAMHURI
YA MUUNGANO WA TANZANIA BUNGENI; KUHUSU ZIARA MAALUM ALIYOIFANYA MKOANI MTWARA TAREHE
27 - 29 JANUARI 2013 KUFUATIA MATUKIO YA UVUNJIFU WA AMANI – ILIYOTOLEWA TAREHE 31
JANUARI, 2013
(Imetolewa chini ya Kanuni ya 38(4) ya Kanuni za Kudumu za
Bunge)
UTANGULIZI
Mheshimiwa Spika, Hali ya ulinzi
na Usalama Mkoani Mtwara ilikuwa ya utulivu kwa kipindi chote hadi tarehe 27 Desemba
2012 yalipofanyika maandamano ya Vyama mbalimbali vya Siasa na Wafuasi wao na baadhi
ya Wakazi wa Mji wa Mtwara wakipinga Mpango wa Serikali wa kusafirisha gesi asilia
kwa bomba kutoka Mtwara kwenda Dar es Salaam. Baada ya maandamano hayo, hali ya amani
na utulivu katika Wilaya ya Mtwara na baadaye katika Wilaya ya Masasi ilianza kutoweka
kwa kutokea matukio mbalimbali ya uvunjifu wa amani.
Hali ya Vurugu Mkoani
Mtwara ilifikia kilele tarehe 25 na 26 Januari 2013 Mkoani Mtwara ambapo kulijitokeza
vitendo vya uvunjifu wa amani viliofanywa na vikundi vya vijana kwa lengo la kuharibu
majengo ya Serikali, nyumba za Watu binafsi, nyumba za Viongozi wa Kisiasa, kuchoma
moto na kuharibu magari ya Serikali na ya Watu binafsi; na miundombinu mingine ya
Umma.
Tarehe 25 Januari 2013 Mjini Mtwara, kulitokea vurugu ambapo matukio
kadhaa yalifanywa yakiwemo nyumba ya Diwani wa Kata ya Chikongola iliharibiwa kwa
kupigwa mawe, nyumba ya Mhe. Hawa Ghasia inayoendelea kujengwa iliharibiwa kwa kupigwa
mawe vioo vya madirisha pamoja na kuunguza sehemu ya jengo hilo, huko Magomeni, jengo
la Ofisi ya Kata ya Ufukoni lilichomwa moto na nyaraka mbalimbali kuunguzwa, Mahakama
ya Mwanzo ya Mjini Mtwara ilichomwa moto na kuteketeza nyaraka mbalimbali, kuchomwa
kwa nyumba ya askari mmoja katika eneo la Sabasaba, kuvunjwa kwa duka la Diwani wa
Kata ya Ufukoni na kuibiwa mali mbalimbali, kushambiliwa na kuibiwa vitu mbalimbali
katika grocery ya Askari mmoja na Askari mmoja kujeruhiwa kwa kupigwa jiwe sehemu
za kichwani; ambapo hali yake kwa sasa inaendelea vizuri.
Vurugu hizo ziliendelea
tarehe 26 Januari 2013 katika Wilaya ya Masasi ambapo kulifanyika uharibifu mkubwa
wa mali za Serikali, Viongozi na Raia. Vurugu hizo ni pamoja na kuchomwa kwa nyumba
za Waheshimiwa Wabunge Mama Anna Abdallah na Mhe. Mariam Kasembe, kuunguzwa na kuteketeza
ofisi za manunuzi Halmashauri ya Masasi, kuteketeza kwa moto ofisi ya elimu ya msingi
na nyaraka zote, kuteketeza ofisi ya ukaguzi wa shule na TSD na nyaraka zote, kuunguzwa
kwa ofisi ya Maliasili na nyaraka zote, kuharibiwa kwa baadhi ya Ofisi za Halmashauri
ya Wilaya ya Masasi, kuchomwa moto na kuteketea kabisa kwa magari kumi na moja (11)
yaliyokuwa yameegeshwa katika yadi ya Halmashauri yakiwemo ya Serikali sita na ya
watu binafsi matano. Kati ya magari ya Serikali yaliyochomwa yapo magari mawili ya
wagonjwa (moja likiwa jipya kabisa). Uharibifu huo pia ulihusisha kuchomwa moto kwa
pikipiki nne na baiskeli moja za Watu binafsi, pamoja na kuharibiwa kwa vifaa mbalimbali
vya ofisi za Halmashauri. Vilevile, kuvunjwa kwa geti kuu la kuingilia Halmashauri,
kuondolewa kwa uzio wa mabati katika jengo linalojengwa na Halmashauri, kuunguzwa
kwa strong room ya Idara ya Maliasili na kuteketea kwa bunduki moja na kuunguzwa kwa
shehena ya mbao zilizokuwa zimekamatwa na Halmashauri.
Vurugu hizo vilevile
zilisababisha vifo vya watu wanne na majeruhi 15 kutokana na mapambano kati ya Raia
(Vijana) na Polisi. Aidha, Polisi mmoja alipigwa mapanga na kujeruhiwa vibaya ambapo
kwa sasa amepelekwa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kwa ajili ya matibabu zaidi.
Napenda
kuchukua nafasi hii kuwapa pole wale wote waliopateza Ndugu, Jamaa na Marafiki zao
katika vurugu hizo. Aidha, nawapa pole waliopoteza mali na Majeruhi wote na kuwatakia
warudi kwenye hali zao za kawaida.
Mheshimiwa Spika, Kama utakavyoona, kiwango
cha vurugu na uharibifu wa mali za Serikali na Raia kilikuwa ni kikubwa. Kufuatia
hali hiyo, tarehe 27 Januari 2013, nililazimika kukatisha safari yangu ya kuja Bungeni
Dodoma na kwenda Mkoani Mtwara. Lengo la Ziara yangu hiyo maalum ilikuwa ni pamoja
na:
Kujionea hali Halisi ya Ulinzi na Usalama Mkoani Mtwara;
Kupata taarifa rasmi za matukio mbalimbali yaliyotokea katika siku
za hivi karibuni Mkoani Mtwara kutoka Kamati za Ulinzi na Usalama za Mkoa na Wilaya,
na hatua zilizochukuliwa kukabiliana na hali hiyo;
Kukutana
na Wadau mbalimbali Mkoani Mtwara ili kusikia kutoka kwao nini hasa kiini cha vurugu
hizo, na kuona namna ya kurejesha hali ya amani na utulivu Mkoani; na
Mwisho ni kusikia maoni yao kuhusu suala zima la Gesi Mkoani Mtwara.
Mheshimiwa
Spika, Katika Ziara yangu Mkoani Mtwara niliweza kukutana na Makundi mbalimbali
ya watu kusikia kutoka kwao sababu za kuzungumzia masuala ya usalama Mkoani humo na
kupata maoni yao hususan katika suala zima la Gesi. Makundi niliyokutana nayo ni pamoja
na:
Viongozi wa Vyama vya Siasa, Mashirika yasiyo ya Kiserikali
na Wanaharakati;
Viongozi wa Madhehebu ya Dini
ya Kiislamu na Kikristo,
Wafanyabiashara na
Wakuu wa Taasisi mbalimbali zikiwemo Taasisi za Fedha wa Manispaa ya Mtwara,
Madiwani na Wenyeviti wa Serikali za Mitaa; na
Wajumbe wa Kamati za Siasa za Chama Tawala za Wilaya na Mkoa.
2.0 HOJA
KUU ZILIZOJITOKEZA
Mheshimiwa Spika, Baada ya kuzungumza na Makundi hayo,
niliweza kupata hoja na mapendekezo yao, mengi yakijielekeza katika suala zima la
gesi na maendeleo ya Mkoa wa Mtwara. Hoja hizo kwa ujumla wake ni hizi zifuatazo:
Kwamba, kimsingi Wananchi wa Mtwara hawana tatizo na gesi kupelekwa Dar es Salaam,
bali wanachotaka ni kuona Mtambo wa kusafisha Gesi Asilia unajengwa Mtwara na kisha
gesi hiyo ndiyo ipelekwe Dar es Salaam kwa ajili ya matumizi mengine yakiwamo ya kufua
umeme, kuuzwa ndani na nje ya Nchi kwa ajili ya matumizi mbalimbali yakiwemo ya viwandani,
nyumbani, n.k. Lengo la kutaka mpango huo ni pamoja na kuwa, kuwepo kwa Mtambo huo
Mkoani Mtwara, utachochea maendeleo ya Mkoa huo na kuzalisha ajira kwa Wazawa wa Mtwara.
Aidha, kuwa na uhakika wa Wawekezaji wengi kuanzisha viwanda Mkoani Mtwara kutokana
na uhakika wa upatikanaji wa Nishati ya Umeme, jambo litakalosaidia ajira kwa vijana
na upatikanaji wa bidhaa kwa bei nafuu kwa Wananchi wa Mtwara;
Sambamba na suala hili la gesi, wametaka kujua lini Sera ya Gesi na Sheria
ya Gesi vitakamilika tayari kwa matumizi ili wawe na uhakika wa kunufaika na rasilimali
ya Gesi;
Walieleza kuwa, Wana Mtwara wanakabiliwa
na matatizo mengi ya msingi yakiwemo ya miundombinu ikiwemo kutelekezwa kwa Bandari
ya Mtwara na kutokukamilika kwa ujenzi wa barabara ya Mtwara - Dar es Salaam kipande
cha (Ndundu-Somanga) ambao umechukua muda mrefu. Wameeleza kuwa, masuala haya yamezidi
kufanya Maendeleo ya Wananchi wa Mtwara kuwa chini kiuchumi.
Wananchi wa Mtwara pia walieleza kuwa, kutokana na kuvumbuliwa kwa gesi
Mkoani humo, Serikali iliwaeleza kuwa, Wawekezaji wengi wameonyesha nia ya kujenga
viwanda Mkoani hapo, kama vile kiwanda cha saruji, mbolea n.k. Hata hivyo, hofu
yao ni kuwa viwanda hivyo bado havijajengwa. Hivyo, wangependa kujua hatma ya suala
hili.
Wananchi wa Mtwara pia wameeleza kuwa na tatizo
kubwa la Viongozi wao wa Kisiasa Mkoani kuwa na mpasuko na kutokuelewana. Suala ambalo
limewasababishia kutokuwa na maelewano na umoja wa Kimkoa na kupanga maendeleo yao
kwa faida ya Wananchi wa Mkoa huo. Wameeleza kuwa, katika mpasuko huo, suala zima
la maendeleo limetawaliwa na ubinafsi na hivyo kuwafanya warudi nyuma kimaendeleo.
Wananchi wa Mtwara wanalalamikia Uongozi wa Mkoa kwa kutokuwasikiliza
na kuwapokea pale walipojaribu kupeleka maoni yao kwa Mkuu wa Mkoa kupitia maandamano
ya tarehe 27 Desemba 2012 kuhusu suala zima la gesi ya Mtwara kupelekwa nje ya Mkoa.
Aidha, walieleza kupewa matamshi ya kuwadharau na kuwafedhehesha. Suala hili pia lilichangia
kwa kiasi kikubwa kuzorotesha mahusiano ya Wananchi na Uongozi wao katika kupanga
na kujadiliana masuala mbalimbali na hivyo kuwarudisha nyuma kimaendeleo.
MAELEZO
YA SERIKALI KUHUSU HOJA HIZO
Mheshimiwa Spika, Hoja zilizotolewa na
Wananchi wa Mtwara ni za muhimu. Nyingi kati ya hizo zinahitaji kutolewa maelezo ya
jinsi gani zimeshughulikiwa na kutoa ufafanuzi pale ambapo panahitaji uelewa zaidi.
Hivyo, naomba nichukue fursa hii kwa ufupi kuelezea masuala machache kuhusiana na
hoja zilizotolewa na Wananchi wa Mtwara.
MAELEZO KUHUSU UJENZI
WA MTAMBO WA KUSAFISHIA GESI NA BOMBA LA GESI
Mheshimiwa Spika, Ufahamu
mdogo wa Mradi mzima wa Mtambo wa kusafishia gesi na ujenzi wa Bomba la Gesi kutoka
Mtwara kwenda Dar es Salaa ndio ulioleta hisia tofauti na hivyo kuchochewa na kusababisha
vurugu zilizokuwa zimetokea Mkoani Mtwara. Ukweli wa Mradi huu kwa kiasi kikubwa umepotoshwa
ama kwa kujua au kwa kutokujua.
Waheshimiwa Wabunge, mtakumbuka kuwa, kufuatia
tatizo la umeme lililoikumba Nchi yetu katika kipindi cha mwaka 2011/2012 kutokana
na ukame uliotokea na kukausha mabwawa yetu ambayo kwa kiasi kikubwa ndiyo yanayotegemewa
katika kufua umeme, katika kutafuta suluhu ya kupata umeme wa uhakika, ilionekana
kuwa, njia nzuri na yenye uhakika ni kufua umeme kutokana na gesi Asilia.
Kimsingi,
Gesi Asilia iliyogunduliwa hapa Nchini ni takribani Futi za Ujazo Trilioni 35. Ingawa
tuna gesi kiasi hicho, kiasi kilichoendelezwa ni futi za ujazo Trilioni 1 tu. Kwa
mantiki hiyo tunaweza kuona kuwa kiasi cha gesi kinachotumika ni kidogo sana ukilinganisha
na kiwango cha Futi za Ujazo Trilioni 35 zilizogunduliwa.
Bomba la gesi asili
linalojengwa litasafirisha gesi nyingi zaidi ambayo itawezesha mitambo mipya itakayojengwa
Kinyerezi (Dar es Salaam) kufua umeme wa zaidi ya MegaWati 990.
Kwa kutumia
Wataalam, Serikali ilifanya upembuzi yakinifu na kubaini kuwa, ni vyema gesi ikasafirishwa
kwa njia ya Bomba hadi Dar es Salaam, kwani itakuwa na faida nyingi kuliko kufua umeme
Mtwara na kusafirisha kwa Gridi. Walipokokotoa usafirishaji wa umeme ulionekana kuwa
utahitaji “Line” zaidi ya moja, hivyo utakuwa ghali zaidi na pia usafirishaji wa umeme
kwa kutumia nyaya na nguzo zake, kutasababisha upotevu mkubwa wa umeme njiani.
Katika
Mpango mzima wa ujenzi wa Mtambo wa kusafishia gesi na bomba la kusafirishia gesi
ni kwamba, tangu awali Serikali ina mpango wa kujenga Mtambo wa kusafishia gesi palepaleMkoani
Mtwara eneo la Madimba, ambapo Gesi italetwa mpaka hapo kutoka kina kirefu cha Bahari
na kusafishwa / kuchujwa na kisha kiasi cha gesi kitabaki Mkoani Mtwara kwa ajili
ya matumizi ya viwanda, majumbani n.k. na nyingine kusafirishwa kwa bomba kwenda Dar
es Salaam. Faida ya kusafirisha Gesi kwa bomba kutoka Mtwara hadi Dar es Salaam ni
kama ifuatavyo:
Bomba litawezesha kusambaza Gesi katika maeneo
yote linapopitia kwa wateja wasio wa umeme. Mtwara - Lindi - Somangafungu na Mkuranga-
Kinyerezi.
Gesi hiyo hiyo itahudumia Viwanda (37) ambavyo
vipo tayari Dar es Salaam; na
Gesi hiyo pia itatumika
kwa matumizi mbalimbali kama vile ya majumbani, kwenye magari, na kuuzwa nje ya Nchi
kama bidhaa mojawapo itakayokuza Pato la Taifa.
Mheshimiwa Spika,
Kutokana na maelezo hayo, taarifa za kuwa Mtambo wa kuchakata / kusafisha Gesi
asilia kuwa hautajengwa Mkoani Mtwara ni potofu kwani Gesi ni lazima isafishwe kabla
ya kusafirishwa na Mtambo huo tayari upo katika Mradi mzima ukijumuisha ujenzi wa
Bomba la Gesi ambao umekadiriwa kuchukua muda wa miezi 18.
Hoja kubwa inayojionyesha
hapa ni kuwa Wananchi hawakupewa elimu ya kutosha kuhusu Mradi huu ikiwa ni pamoja
na kueleweshwa mpango mzima wa Gesi ikiwa ni pamoja na kujua fursa zilizopo na jinsi
Wananchi watakavyohusika nazo; Kama vile katika ajira, biashara, elimu, n.k. Hali
hii ndiyo imetoa nafasi kwa watu mbalimbali kutafsiri isivyo na kupotosha ukweli wa
suala hili. Kutokana na hali hiyo, suala hili limeibua hisia na hasira kwa Wananchi
ambao kimsingi hawakuwa na ufahamu sahihi wa mpango nzima.
Ninaelewa kuwa,
awali Uongozi wa Mkoa kwa kushirikiana na Shirika la Maendeleo ya Petroli Nchini (TPDC)
walitoa elimu kwa kundi la Watu wachache, wakiwemo wale walioathirika na upitishwaji
wa Bomba la Gesi Asilia na wale walio karibu na Bomba hilo ili wawe walinzi shirikishi
pamoja na Viongozi wa Siasa, Mashirika yasiyo ya Serikali, Wanaharakati n.k kwa lengo
la kundi hilo kwenda kutoa elimu kwa Umma. Hata hivyo, imeelezwa kuwa, wale wachache
waliopata elimu hiyo wamekuwa wakipotosha ukweli wa Mradi huo kwa maslahi yao binafsi
kwa kutilia maanani kuwa Wananchi wengi hawana uelewa sahihi juu ya suala hili.
Ninapenda kuwajulisha kuwa, baada ya kuzungumza na makundi mbalimbali kama nilivyoyataja
na kuwaelewesha Mpango huumzuri wa Serikali, walielewa na kukiri kuwa walikuwa hawana
uelewa wa kutosha kuhusu Mradi huu.
SUALA LA SERA NA SHERIA YA
GESI
Mheshimiwa Spika, Ili kufanikisha matumizi endelevu ya gesi asilia,
Serikali imeazimia kukamilisha mapema iwezekanavyo Sera ya Gesi Asilia na Sheria ya
Gesi. Sera ya Gesi Asilia ipo katika hatua za kukamilika kwake baada ya Serikali kufanya
mikutano Nchi nzima na kukusanya maoni ya Wadau mbalimbali kwa lengo la kukamilisha
Sera hiyo. Baadhi ya Wadau walioshirikishwa ni pamoja na Wananchi wa kawaida katika
Mikoa ya Tanzania hususan ile inayotoka katika Ukanda wa gesi ikiwemo Mtwara, Lindi
na Pwani; Makampuni ya wachimba Gesi na Mafuta yaliyopo Nchini, Wanataaluma kutoka
Vyuo vya Elimu ya Juu, Mashirika yasiyo ya Kiserikali, Wataalam mbalimbali wa Gesi,
Makundi ya Kijamii n.k.
Sambamba na Sera ya Gesi asilia, Serikali imeshaanza
kuandaa rasimu ya Sheria ya Gesi ambapo ikikamilika, itapitishwa katika ngazi stahiki
na hatimaye kuwasilishwa katika Bunge lako Tukufu.
SUALA
LA MIUNDOMBINU YA MAENDELEO MKOANI MTWARA IKIWAMO BANDARI
Mheshimiwa Spika, Ili
kutengeneza mazingira mazuri ya biashara ya gesi asilia na mafuta kwa Makampuni ya
huduma, malighafi na vitendea kazi, Serikali imetenga eneo maalumu Mkoani Mtwara,
ambalo litawekewa miundombinu ya msingi ili kuweka vivutio mbalimbali kwa Makampuni
hayo. Eneo hilo litapewa hadhi ya Ukanda Huru wa Bandari (Freeport Zone).
Eneo
hilo litavutia Makampuni mbalimbali kuja kuwekeza kwa nia ya kuhudumia na kufanya
biashara na Makampuni yenye visima vya gesi nchi kavu na kina kirefu baharini. Makampuni
makubwa duniani yameonesha nia ya kuja kuwekeza ili yafanye biashara na makampuni
yaliyoko sasa kusini mwa Tanzania na hata nchi jirani ya Msumbiji badala ya kupata
huduma hizo kutoka Qatar ambako ni mbali. Kuwepo kwa maendeleo hayo Mkoani Mtwara,
kutaharakisha maendeleo ya kiuchumi na kubadilisha kabisa hali ya uchumi ya Mikoa
ya Kusini mwa Tanzania.
Kuhusu ujenzi wa Barabara kipande cha Ndundu - Somanga,
kati ya Kilometa 62 zilizokuwa zimebakia kujengwa, Serikali inakamilisha ujenzi huo
ambapo kwa sasa zimebaki Kilomita 20 tu. Ujenzi huu ulichelewa kukamilika kutokana
na matatizo yaliyokuwa yamejitokeza katika Kampuni ya Karafi inayojenga barabara hiyo
baada ya Mmiliki wake kufariki. Kwa sasa Kampuni hiyo inaendelea na ujenzi wake na
Serikali inaahidi kuisimamia ili ujenzi huo ukamilike ndani ya mwaka huu.
UWEKEZAJI WA VIWANDA MKOANI MTWARA
Mheshimiwa Spika, Baada
ya neema hii ya gesi Mkoani Mtwara, Wakazi wa Mtwara mbali ya kufaidika kwa gesi asilia
ambayo itakuwa ni chanzo cha uhakika cha umeme na matumizi ya gesi moja kwa moja
watafaidika pia na kuwepo kwa Wawekezaji wengi walioonyesha nia ya kuwekeza Mkoani
Mtwara kutokana na fursa hii. Mpaka sasa kuna Makampuni yapatayo 51 ambayo yameonyesha
nia ya uwekezaji katika viwanda vya Saruji, Mbolea, Sekta ya Usafirishaji, Kilimo
na Usindikaji, na kuwekeza katika Utalii. Aidha, mabaki ya gesi baada ya kusafishwa
ni malighafi muhimu kwa baadhi ya viwanda vikiwemo vya mbolea, kemikali petrol, bidhaa
za plastiki, n.k.
Kutokana na kujengwa kwa viwanda hivyo na uwekezaji unaotarajiwa
Mkoani Mtwara, tatizo la ajira Mkoani humo litapungua kwa kiasi kikubwa. Nimeelezwa
kuwa, moja ya viwanda vikubwa vitakavyojengwa, kitahitaji Watumishi wa kawaida takriban
50,000 na Wataalam 2,000. Hakika huu utakuwa ni ukombozi mkubwa wa ajira kwa Wananchi
wa Mtwara na Tanzania kwa ujumla. Kampuni ya Dangote inatarajia kujenga kiwanda kikubwa
cha Saruji Mkoani Mtwara ambacho kimeelezwa kuwa moja ya Viwanda vikubwa vya Saruji
Barani Afrika, nacho kitatoa ajira nyingi na za uhakika kwa Wana Mtwara. Niseme tu
kuwa, Wananchi wa Mtwara wawe na subira katika mipango hii kwani ni ya uhakika.
Mheshimiwa
Spika, Ili kuhakikisha kuwa Wananchi wetu wakiwemo wa Mtwara na hususan Vijana
wananufaika na ajira za maana katika miradi ya gesi na viwanda vitokananvyo na fursa
za gesi, Serikali imejipanga katika kuelimisha watu wetu kama ifuatavyo:
Mpango wa mafunzo umeandaliwa kwenye Taasisi za Elimu hapa Nchini na nje
ya nchi katika eneo la Mafuta na Gesi Asilia. Hapa nchini Vyuo vinavyosomesha Wataalam
wetu ni pamoja na Chuo Kikuu cha Dodoma, Dar es Salaam, VETA-Mtwara, na Madini Dodoma.
Kwa Vyuo vya nje ya Nchi, Serikali imepeleka Wanafunzi katika Vyuo vya Trondheim –
Norway, na Vyuo vya Aberdeen, Dundee, na Coventry vya Uingereza.
Vilevile Serikali inagharamia mafunzo ya Wanafunzi 100 kutoka Mikoa ya
Mtwara na Lindi kusoma mafunzo ya muda mfupi, VETA Mtwara.
Katika
hatua nyingine, Serikali imeanzisha mpango wa mafunzo wa ushirikiano kati ya Vyuo
Vikuu vya Nchi za Angola, Norway na Tanzania (Angola, Norway, Tanzania Higher Education
Initiative - ANTHEI) kwa nia ya kutoa mafunzo katika ngazi ya shahada ya uzamili
eneo la Petroli na Gesi. Mpango huu kwa kuanzia una vijana 10 ambao wameshaanza mafunzo
katika Vyuo hivyo Vikuu kuanzia muhula wa mwezi Oktoba 2012.
SUALA LA KUTOKUELEWANA KWA WANANCHI NA UONGOZI WA MKOA WA MTWARA
Baada ya kusikia malalamiko kutoka kwa Wananchi wa Mkoa wa Mtwara kuhusiana
na mahusiano mabaya ya Wananchi na Mkuu wa Mkoa baada ya kusemekana kuwadharau na
kuwakejeli Wananchi wa Mtwara, tatizo hili kwa sasa nina uhakika litakuwa limekwisha.
Juzi kabla ya kuhitimisha Ziara yangu Mkoani Mtwara na kabla ya kufanya majumuishao,
Mkuu wa Mkoa Mhe. Kanali Mstaafu Joseph Simbakalia alionyesha uungwana wake kwa kupitia
hadhara iliyokuwepo kwa kuomba radhi Wananchi wa Mtwara kwa matatizo yaliyojitokeza
na kuwaomba waendelee na ushirikiano wao kwa lengo la kuujenga Mkoa wa Mtwara ambao
una mategemeo mengi. Napenda kumshukuru Mkuu wa Mkoa wa Mtwara kwa kuonyesha uungwana
wake na ukomavu wake. Kiongozi huyu ni Mtu makini na mwenye uzoefu mkubwa katika masuala
ya Uwekezaji. Hii ndiyo sababu kubwa ya Serikali kuamua kumpeleka Mkoani Mtwara kuweka
mazingira wezeshi ya uwekezaji na kuwaandaa Wananchi kwa fursa zinazokuja. Nina hakika
kuwa, baada ya mapatano hayo, Mkoa utarejea katika hali yake ya kawaida na kufanya
kazi kwa karibu na Uongozi wa Mkoa kwa maendeleo yao.
SUALA
LA MPASUKO WA VIONGOZI WA MKOA WA MTWARA
Mheshimkiwa Spika, Nimesikitika
kusikia kuwa katika Mkoa wa Mtwara, Viongozi wake wa Kisiasa wana mpasuko ambao kwa
maoni ya Wananchi, umesababisha kurudisha nyuma maendeleo ya Mtwara. Ninachoweza kusema
kwa sasa ni kuwasihi Viongozi wenzangu wa Bunge na wale wa Chama kukaa chini na kuondoa
tofauti zao kwa lengo la kuusaidia Mkoa wa Mtwara. Tofauti hizi ndizo zilizosababisha
hata madhara na hasara kwa baadhi ya Viongozi kama tulivyoshuhudia. Hali hii ni ya
hatari na isiyopendeza kwa Jamii. Chuki na tofauti kati yetu hazina budi kukomesha,
kwani lengo letu siku zote kama Viongozi ni kuwahudumia na kuwasikiliza Wananchi.
Hali iliyopo Mkoani Mtwara baina ya Wananchi na Viongozi wao si ya kuridhisha, na
hivyo ni wajibu wa Viongozi na wana Mtwara wenyewe kurekebisha hali hii na kusonga
mbele.
3.0 MAPENDEKEZO YA SERIKALI
Mheshimiwa Spika, Ili kuhakikisha
kuwa Wananchi wanakuwa na uelewa sahihi wa Mradi huu na Miradi mingine iliyopo na
itakayokuwapo Mkoani Mtwara, nimeushauri Uongozi wa Mkoa uunde Kamati Maalum ya Kusimamia
na Kusukuma Maendeleo ya Mkoa wa Mtwara. Kamati hii itakuwa na jukumu la kufuatilia
maendeleo ya Miradi mbalimbali Mkoani na kutoa elimu kwa Miradi inayohusu Wananchi
kwa kushirikiana na Wataalam. Lengo likiwa kuwafikishia Wananchi taarifa sahihi za
Miradi inayowahusu.
Kamati hiyo itakayokuwa nje ya Mfumo wa Serikali,
itajumuisha Wajumbe kutoka Sekta Binafsi, Mashirika yasiyo ya Kiserikali, Madhehebu
ya Dini, n.k. ambapo Serikali itakuwa ikisaidia na kutoa msukumo pale itakapohitajika.
Kutokana na maendeleo ya Gesi Mkoani Mtwara, Serikali inawashauri Wana-Mtwara
kutambua fursa walizonazo na kujipanga katika masuala yafuatayo:
Kuongeza ujenzi wa nyumba bora kwa sababu kutakuwa na ongezeko la watu
Mkoani watakaokuja kufanya shughuli mbalimbali za kiuchumi;
Kujenga
hoteli na nyumba za wageni zitakazotumiwa na Watu wa hadhi zote;
Kwa upande wa Vyombo vya Fedha kama vile mabenki ya biashara, wajipanue
zaidi katika kupokea biashara zaidi na kutoa mikopo kwa Wananchi.
Serikali kwa upande wake itaendelea na juhudi za kuimarisha miundombinu
ya Barabara, Bandari, Reli na kuboresha kiwanja cha Ndege ili kwenda sambamba na maendeleo
katika Mkoa wa Mtwara na Mikoa ya jirani.
Kutokana
na vurugu zilizotokea Mkoani Mtwara, ninatoa wito kwa Wananchi wa Mtwara kuwa, maadam
sasa Viongozi wa Mkoa huo kwa kupitia makundi mbalimbali niliyokutana nayo wameshaeleweshwa
suala hili la Mradi wa Gesi vizuri, sasa ni wajibu wao kuwaelewesha Wananchi wao kuhusu
suala hili! Lengo likiwa ni kuwaelimisha ili vurugu zilizotokea na kuleta madhara
makubwa zisitokee tena. Ninapenda kuwashauri kuwa, endapo kuna tatizio limetokea,
basi ni vizuri kukaa na Viongozi wao na kuliwasilisha ili lipatiwe ufumbuzi. Wanapoharibu
miundombinu ya Umma ambayo imejengwa kwa fedha zao wenyewe kama walipa kodi ni kujikomoa
wenyewe kwani nao watakosa huduma muhimu watakazohitaji. Katika matukio haya ni kama
vile kukosa huduma za magari ya wagonjwa, huduma za Mahakama, n.k.
Vilevile,
tabia ya Kikundi cha Wananchi kujichukulia hatua mkononi na kuharibu mali za Umma
na za Watu binafsi haitavumiliwa. Wale wote wenye kufanya vitendo kama hivyo, watachukuliwa
hatua stahiki.
HITIMISHO
Mheshimiwa Spika, Faida za gesi iliyopatikana
Nchini mwetuna ujenzi wa bomba la gesi kutoka Mtwara kwenda Dar es Salaam ni nyingi,
kwa uchache naomba kuzitaja kama ifuatavyo:
Kuwepo kwa miundombinu
madhubuti ya usafirishaji wa gesi kutoka ilikogundilika kwenda kwenye maeneo mengine
ya Nchi kwa matumizi ya kiuchumi na kufanya Nchi yetu kuwa ya uchumi wa gesi ;
Kuwezesha uzalishaji wa haraka wa umeme nchini ambao ni zaidi ya
MW 2500 kabla ya mwaka 2015 na hivyo kuchochea shughuli mbalimbali za kiuchumi ;
Kuimarika kwa Sekta ya Viwanda kutakako sababishwa na uwepo wa
umeme wa uhakika na wa bei nafuu. Kwa sasa bei ya umeme ni Dola za Marekani senti
35 - 45 kwa uniti, wakati umeme utakaozalishwa na gesi utauzwa kwa kati ya Dola za
Kimarekani senti 6 - 8 kwa uniti. Kuokoa zaidi ya kiasi cha shilingi Trilioni 1.6
kwa mwaka zinazotumika kununua mafuta ya kuendeshea mitambo ya kuzalishia umeme.
Kutokana na matumizi ya gesi asilia kwenye magari, mahotelini,
na majumbani kwa Dar es Salaam peke yake zitaokolewa zaidi ya shilingi Bilioni 320
kwa mwaka, na kiwango hicho kitaongezeka kulingana na kuongezeka kwa matumizi ya gesi
badala ya mafuta kwa eneo kubwa zaidi la Nchi.
Kuongezeka
kwa ajira katika sekta mbalimbali, maana usalama wa ajira kwa miaka ya karibuni uliathiriwa
zaidi na kutokuwepo kwa umeme wa uhakika ;
Kuimarika
kwa Sekta ya Kilimo kutokana na kuwepo kwa mbolea yenye bei nafuu itakayozalishwa
Nchini ; na
Kuwa na usalama wa mazingira yetu
kutokana na matumizi ya gesi asilia kupikia badala ya kutumia mkaa na kuni, n.k.
Mheshimiwa
Spika, baada ya kusema hayo, nawaomba Waheshimiwa Wabunge na Wananchi wote wa Tanzania
kuiunga mkono Serikali katika jitihada zake za dhati za matumizi ya gesi kutoka Mtwara
kwa manufaa mbalimbali ikiwemo kutatua tatizo kubwa la nishati ya umeme Nchini ili
tuweze kujenga Nchi yenye uchumi wa Viwanda kwa ustawi wa Wananchi wote wa Tanzania.
Ninawasihi
WanaMtwara wawe na umoja na subira katika suala hili la Gesi wakati Serikali ikikamilisha
taratibu zitakazowezesha Wananchi kuona matunda ya rasilimali hii ya Gesi.
Watanzania
hatuna budi kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa zawadi hii ya rasilimali ya Gesi aliyotupatia.
Ni vyema tukahakikisha kwamba, baraka hii haigeuki kuwa laana kwetu na kwa vizazi
vijavyo, bali iwe ni mwanzo wa neema kwetu, na kwa vizazi vyetu. Umoja wetu kwa wakati
huu ni muhimu sana kwa maendeleo ya Taifa letu.
Mwisho, napenda kuchukua kuchukua
fursa hii kuwashukuru Mawaziri Mheshimiwa Dkt. Emmanuel Nchimbi (Mb.), Waziri wa Mambo
ya Ndani ya Nchi; Mheshimiwa Dkt. Harrison Mwakyembe (Mb.), Waziri wa Uchukuzi; Mheshimiwa
Prof. Anna Tibaijuka (Mb.), Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi; na Mheshimiwa
Dkt. Shukuru Kawambwa (Mb.), Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi kwa kuambatana nami
Mkoani Mtwara na kutoa maelezo na ufafanuzi katika maeneo ya Sekta zao. Maelezo hayo
yamekuwa ya msaada mkubwa, kwani naamini yamesaidia kutoa uelewa kwa Wananchi wa Mkoa
wa Mtwara kupitia Viongozi wao.