2013-01-31 08:36:45

Haki na amani ni mambo yanayoendelea kutikisa maisha ya watu sehemu mbali mbali za dunia!


Mama Kanisa anapoendelea kuadhimisha Mwaka wa Imani, kusherehekea matunda ya miaka hamsini ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican sanjari na maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu juu ya Uinjilishaji Mpya iliyofanyika mjini Vatican, Oktoba 2012 ni wakati muafaka kwa Mama Kanisa kuendelea kufanya tafakari ya kina kuhusu misingi ya haki na amani; mambo yanayoendelea kugusa maisha ya watu wengi duniani. RealAudioMP3
Haki na Amani ni chanda na pete na mwaliko wa kutoa kipaumbele cha pekee kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii, kuonja upendo na ukarimu huu unaopata chimbuko lake katika kweli za Kiinjili, kama zilivyotangazwa na Yesu Kristo mwenyewe. Ni mambo msingi yanayopaswa kufanyiwa kazi katika maisha na utume wa Kanisa, kwa kujikita katika toba na wongofu wa ndani. Pengine umefika wakati wa kumwilisha kwa kasi zaidi uelewa wa haki jamii, kama sehemu ya mchakato wa Mama Kanisa katika utekelezaji wa dhamana ya Uinjilishaji Mpya, inayovaliwa njuga wakati huu wa Mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo.
Ni mchango wa Kardinali Peter Turkson, Rais wa Baraza la Kipapa la Haki na Amani wakati wa maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu juu ya Uinjilishaji Mpya. Anasema kwamba, Uinjilishaji Mpya ni nyenzo ya Uinjilishaji inayopania kuwaonjesha watu ile furaha ya imani na upendo; mwanadamu akipewa kipaumbele cha kwanza kama mdau na mlengwa wa maendeleo ya mwanadamu.
Uinjilishaji Mpya unapaswa kuwa ni dhamana endelevu, ili kuweza kuleta mabadiliko yanayokusudiwa na Mama Kanisa katika Jamii, hasa katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia kwani kuna kinzani nyingi kuhusu mwono na uelewa wa mwanadamu. Hali hii inaonesha haja ya kuanza kwa bidii mchakato wa Uinjilishaji Jamii kama mwendelezo makini wa Uinjilishaji; jambo ambalo ni changamoto endelevu katika maisha na utume wa Kanisa.
Kardinali Peter Turkson anasema, leo hii kuna watu wanauelewa mpana na wanaguswa kwa karibu sana na tema kama vile: haki msingi za binadamu; mafao ya wengi, ekolojia na mapambano dhidi ya rushwa, ufisadi na ubadhirifu wa mali ya umma kama kikwazo kikubwa cha maendeleo endelevu ya binadamu. Ni mambo tete yanayogusa maisha ya mtu binafsi na maisha ya Jumuiya ya Kimataifa; changamoto kwa Kanisa kujikita katika Uinjilishaji Jamii.
Ili kuweza kufikia malengo haya anasema Kardinali Peter Turkson, kuna haja ya kujikita katika majiundo ya awali na endelevu kwa waamini na watu wote wenye mapenzi mema, ili waweze kufahamu kwa kina mapana Mafundisho Jamii ya Kanisa; muhtasari wa vitendea kazi kwa waamini walei katika dhamana ya kuyatakatifuza malimwengu.
Kardinali Turkson anasema kwamba, kati ya Nyaraka ambazo zinapaswa kufanyiwa kazi kwa sasa ni Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki, Nyaraka za Mababa wa Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican sanjari na Mafundisho Jamii ya Kanisa. Kwa mantiki hii, Kardinali Turkson analihamasisha Kanisa Katoliki kuangalia uwezekano wa kuadhimisha Sinodi juu ya Uinjilishaji Jamii kwa siku zijazo.







All the contents on this site are copyrighted ©.