2013-01-30 11:21:06

Utu na heshima ya mwanadamu vipewe kipaumbele cha pekee katika sera za wahamiaji na watu wasiokuwa na makazi


Jumuiya ya Mtakatifu Egidio yenye makao makuu yake hapa mjini Roma, tarehe 29 Januari 2013 imefanya Kongamano lililokuwa linaongozwa na kauli mbiu "wahamiaji na mshikamano wa kiimani". Kongamano ambalo limehudhuriwa pia na na Kardinali Antonio Maria Veglio', Rais wa Baraza la Kipapa la shughuli za kichungaji kwa wahamiaji na watu wasiokuwa na makazi maalum.

Katika kongamano hili, Serikali ya Romania ilimpatia Kardinali Veglio' nishani, kwa kutambua mchango wake katika kulinda na kutetea haki msingi za wahamiaji na watu wasiokuwa na makazi maalum sehemu mbali mbali duniani. Anasema, ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia unaonesha utajiri na tofauti kubwa zinazojionesha miongoni mwa watu: kitamaduni, kijamii, kiuchumi, kisiasa na hata kidini, kiasi kwamba, hata hali ya wahamiaji na watu wasiokuwa na makazi maalum wanakuwa mashakani.

Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, anaonesha imani na matumaini ya pekee kwa wahamiaji kama mahujaji wa imani na matumaini, licha ya Njia ya Msalaba wanayokabiliana nayo katika hija ya maisha yao. Wananchi wa Romania wanakabiliwa pia na tatizo la wananchi wanaolazimika kuyahama makazi yao ili kutafuta hali bora zaidi ya maisha katika nchi nyingine; huko wanakumbana na hali ngumu kutokana na hofu za vitendo vya kigaidi, biashara haramu ya binadamu na dawa za kulevya; ukahaba pamoja na vitendo vinavyodhalilisha utu na heshima ya binadamu.

Katika hali zote hizi, utu na heshima ya binadamu vinapaswa kupewa kipaumbele cha kwanza anasema Kardinali Veglio'. Wahamiaji ni rasilimali ambayo ikitumiwa vyema inaweza kuwa ni msaada mkubwa katika maendeleo kwenye medani mbali mbali za maisha ya mwanadamu.







All the contents on this site are copyrighted ©.