Shutuma za udini dhidi ya Mwl. J. K. Nyerere, Baba wa Taifa la Tanzania
Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Baba wa Taifa la Tanzania ni kati ya viongozi wa
siasa wanaoheshimika sana Barani Afrika. Lakini kwa bahati mbaya, "Nabii hakosi heshima
isipokuwa kwa watu wa nyumbani kwake".
Kwa miaka
kadhaa, baadhi ya Waamini wa dini ya Kiislam nchini Tanzania amedai kwamba, wakati
wa utawala wa Mwalimu Julius K. Nyerere, waamini hao walinyanyaswa kiasi kwamba, wamebaki
nyuma kimaendeleo ikilinganishwa na waamini wa dini nyingine nchini Tanzania.
Idhaa
ya Kiswahili ya Radio Vatican, katika mahojiano maalum na Askofu Michael Msonganzila
wa Jimbo Katoliki Musoma, anakanusa uvumi huu kwa kusema kwamba, ni malalamiko ambayo
yamezagaa nchini Tanzania kiasi kwamba, kuna baadhi ya watu wamediriki hata kutengeneza
Kanda ili kueneza uvumi huu. Haya ni mawazo yaliyonunuliwa kutoka nje, ili kuvuruga
misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano wa kitaifa ambao watanzania kwa takribani
miaka 50 iliyopita wamekuwa wakiufaidi.
Askofu Msonganzila anasema, hizi ni
dalili za ukoloni mambokesho! Kinzani za kidini kwa madai kwamba, Serikali ya Tanzania
inaongozwa na mfumo Kristo ni uzushi usiokuwa na msingi. Watanzania watakumbuka kwamba,
wakati wa Azimio la Arusha, Serikali ilitaifisha shule zilizokuwa zinamilikiwa na
kuendeshwa na Kanisa, ili kutoa fursa kwa watanzania wengi zaidi kupata fursa ya elimu.
Kanisa lilitambua na kuheshimu nia njema iliyooneshwa na Baba wa Taifa bila
kunung'unika. Ikumbukwe kwamba, mikakati ya kichungaji katika sekta ya elimu ni sehemu
ya Uinjilishaji wa kina unaofanywa na Kanisa Katoliki katika mchakato wa kukomboa
mtu mzima: kiroho na kimwili, kumbe kumiliki na kuendesha shule katika viwango mbali
mbali si jambo la nasibu bali ni sehemu ya vinasaba vya Kanisa Katoliki.
Hata
baada ya kutaifishwa shule, watanzania wengi waliokuwa na kiu ya elimu walipata bila
ya ubaguzi wowote, kinyume kabisa cha madai yanayotolewa na baadhi ya waamini kwa
sasa! Kuna watanzania wengi ambao baadhi yao ni viongozi waandamizi Serikali wamesoma
katika shule zilizotaifishwa au zilizokuwa zinamilikiwa na Kanisa, bila shaka hawa
ni mashahidi makini wa hali halisi ilivyokuwa katika shule hizi.
Askofu Michael
Msonganzila anasema, hizi ni zama za ukweli na uwazi, watanzania wanapaswa kufungua
macho, masikio, mioyo na akili zao ili kuuona ukweli. Huu si muda wa malumbano, bali
watu wawekeze katika elimu inayomwangalia mtu mzima: kiroho na kimwili, ili kuweza
kuwajengea watoto wa kitanzania, kesho iliyo bora zaidi.
Elimu ya dini na
elimu dunia zina nafasi yake. Watanzania wasikubali kutumiwa na watu wasiowatakia
mema kwa kufanya ghasia na malumbano yasiyokuwa na tija kwa maendeleo yao. Wakumbuke
daima kwamba, vita na ghasia hazina macho, kwa kujiingiza katika migogoro ya kidini,
watapoteza hata kile kidogo walicho nacho kwa sasa! Ni wakati wa kujenga na kuimarisha
mshikamano na umoja wa kitaifa dhidi ya maadui walioko ndani na nje ya Tanzania wanaotaka
kulitumbukiza Taifa katika maafa ya udini.