2013-01-30 08:13:47

Mheshimiwa Padre Marco Tasca achaguliwa kuwa Mkuu wa Shirika la Wafranciskani


Shirika la Ndugu Wadogo wa Mtakatifu Francisco, katika maadhimisho ya Mkutano mkuu wa mia mbili, wamemchagua Mheshimiwa Padre Marco Tasca kuwa Mkuu wa Shirika kwa kipindi cha miaka sita, baada ya kupewa siku kumi za kusali, kutafakari na kupembua maisha yake na sasa anajikabidhi mikononi mwa Mwenyezi Mungu kwa ajili ya kuwaongoza ndugu zake katika maisha na utume wa Shirika.

Ni mwaliko na changamoto ya pekee kwanza kabisa: kulifahamu, kulitafakari na kulimwilisha Neno la Mungu kama kielelezo cha Imani tendaji kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Mheshimiwa Padre Tasca anamwomba Mtakatifu Francisco wa Assis awaombee neema na baraka za kuweza kuwa kweli ni mashahidi wa imani na matumaini, wakijitahidi kuiga mfano na maisha ya Mtakatifu Francisco wa Assis.

Ni mwaliko kwa Wafranciscan kuendelea kuwa ni wajumbe wa amani na upatanisho, changamoto endelevu inayopaswa kufanyiwa kazi kutokana na vita, kinzani na migogoro inayoendelea kujitokeza sehemu mbali mbali za dunia. Ni ushuhuda unaopaswa kujikita katika uhalisia wa maisha ya Wanashirika hawa.

Ni muhimu pia kuendeleza mchakato wa utamadunisho, kwani Shirika lina watu kutoka sehemu mbali mbali wanaotekeleza utume wao pia sehemu mbali mbali za dunia, bila kusahau majadiliano ya Kiekuemene na Kidini na Waamini wa dini ya Kiislam. Ushuhuda wa kwanza kadiri ya Sheria za Wafranciskani unajikita katika mahusiano mema!







All the contents on this site are copyrighted ©.