Majadiliano ya kidini na kiekumene ni njia muafaka katika utekelezaji wa dhamana ya
Uinjilishaji Mpya!
Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Barani Asia, hivi karibuni, limehitimisha
mkutano wake wa mwaka, uliofanyika kwa mara ya kwanza katika historia yake nchini
Vietnam.
Tukio hili
ni baraka kwa Bara la Asia na Kanisa katika ujumla wake, kwani Shirikisho hili linaadhimisha
miaka arobaini tangu lilipoanzishwa ili kukabiliana na changamoto mbali mbali zinazoendelea
kujitokeza katika maisha na utume wa Kanisa Barani Asia.
Wajumbe walipata fursa
ya kuangalia na kupembua maisha na utume wa Kanisa katika nyanja mbali mbali za maisha,
lakini zaidi wamejikita katika majadiliano ya kidini miongoni mwa waamini wa dini
mbali mbali Barani Asia; uhuru wa kidini ambao umekuwa na utata katika nchi nyingi
Barani Asia kutokana na baadhi ya waamini kuwa na misimamo mikali ya kiimani inayotishia
amani na usalama wa raia na mali zao. Maaskofu wamepembua kwa kina na mapana dhana
ya umaskini na mapambano yake, ili kuboresha idadi kubwa ya watu wanaoendelea kuogelea
katika dimbwi la umaskini wa hali na kipato.
Maaskofu wameona pia kwamba,
kuna changamoto kubwa mbele yao ya kuhakikisha kwamba, wanasimama kidete kulinda na
kuwatetea wazawa; wameangalia hali ya wahamiaji na wakimbizi wanaoyakimbia makazi
yao kutokana na sababu mbali mbali na jinsi ya kuwahudumia. Hadi hapa Maaskofu walikuwa
wanajadili kuhusu hali ya maisha ya kijamii na kisiasa Barani Asia.
Maaskofu
wamezama kwa undani zaidi kwa kuangalia dhamana na nafasi ya waamini walei katika
ushuhuda wa maisha na changamoto wanazokabiliana nazo katika kuyatakatifuza malimwengu,
ili dunia iweze kuwa ni mahali pazuri zaidi pa kuishi; pamoja na kushiriki kikamilifu
katika dhamana ya Uinjilishaji Mpya kama njia ya kurithisha imani kwa njia ya ushuhuda
wa furaha ile inayobubujika kutoka katika undani wa waamini wanaokutana na Yesu katika
hija ya maisha yao: kwa njia ya Neno la Mungu, Maisha ya Kisakramenti bila kusahau
matendo ya huruma ambayo kimsingi ni Imani katika matendo.
Wajumbe kutoka Mabaraza
mbali mbali ya Maaskofu Katoliki Barani Asia, walipata fursa ya kuelezea hali ya maisha,
utume, changamoto na matatizo wanayokabiliana nayo katika kumhudumia mwanadamu kiroho
na kimwili. Changamoto kubwa ambayo imeguswa na wengi ni umuhimu wa kuendeleza majadiliano
ya kidini na waamini wa dini mbali mbali Barani Asia kama sehemu ya mchakato wa Uinjilishaji
Mpya, changamoto iliyotolewa na Mababa wa Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican na kama
walivyokazia Mababa wa Sinodi juu ya Uinjilishaji Mpya, iliyohitimishwa hivi karibuni
mjini Vatican.
Baadhi ya wajumbe wamekiri pia umuhimu wa majadiliano ya kiekumene
na waamini wa madhehebu mbali mbali ya Kikristo ambayo yanaendelea kuongezeka kwa
kasi kubwa, kwa kujikita katika kuwapatia watu majibu ya mkato kutokana na shida na
hali ngumu ya maisha wanayokabiliana nayo! Jambo la msingi wanasema wajumbe, ni kujenga
mazingira ya kuaminiana, kuheshimiana na kuthaminiana, wote kwa pamoja wakipania kutafuta
mafao ya wengi, kudumisha misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano wa kitaifa.
Kumekuwepo na dalili nzuri za majadiliano kati ya Kanisa na Serikali ya Vietnam
na kwamba, kuna dalili za maboresho ya uhusiano kati ya Kanisa na Serikali ya China,
ingawa bado kuna kazi kubwa ya kuendelea kutekeleza.
Wakristo Barani Asia wanahitaji
kwa namna ya pekee kuchangamka ili kutolea ushuhuda wa imani yao kwa Kristo na Kanisa
lake, katika utamaduni na mazingira ambayo yanaonesha kuwa na changamoto hasi. Wazawa
wanapaswa kuheshimiwa, kuthaminiwa pamoja na kuwezeshwa katika sekta mbali mbali za
maisha, ili waweze kutekeleza vyema nyajibu zao katika maisha na utume wa Kanisa na
Jamii inayowazunguka.
Kuna hatari kwamba, mbegu ya utamaduni wa kifo inaendelea
kupandikizwa kwa kasi ya ajabu Barani Asia, kwa hofu kwamba, kuna idadi kubwa ya watu
wanaongezeka siku hadi siku, hapa waamini wanapaswa kukumbatia na kuenzi Injili ya
Uhai. Kuna madhara makubwa ambayo yametokana na athari za mabadiliko ya tabianchi,
hali ambayo imepelekea watu wengi hasa kutoka Bangaladesh kuishi katika mazingira
magumu ya kiuchumi na kijamii; wengi wanaendelea kutumbukia katika lindi la umaskini
wa hali na kipato.
Katika mazingira kama haya, utume wa Kanisa unajikita zaidi
na zaidi katika kupanga na kutekeleza mipango ya maendeleo endelevu yanayogusa mahitaji
ya mtu mzima kiroho na kimwili; kwa kuenzi utu na heshima ya kila mwanadamu aliyeumbwa
kwa sura na mfano wa Mungu; kusimama kidete kupinga rushwa, ubadhilifu wa mali ya
umma na ufisadi, mambo ambayo kwa kiasi kikubwa yanaonesha ubinafsi wa baadhi ya watu
ndani ya Jamii; hali inayoweza pia kuchangia kuporomoka kwa misingi ya haki, amani
na utulivu.
Kanisa Katoliki Barani Asia linapenda kujikita katika majadiliano
ya kidini na kiekumene, likitambua dhamana na sauti yake ya kinabii; dhidi ya utamaduni
wa kifo unaofumbatwa katika sera za utoaji mimba na kifo laini au Eutanasia kama kinavyojulikana
na wengi.
Mwishoni, wajumbe wa Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki
Asia wamekazia umuhimu wa Jumuiya Ndogo ndogo za Kikrsto kama shule ya Neno la Mungu,
Maisha ya Kisakramenti na Matendo ya huruma yanayojenga na kuimarisha Injili ya Upendo
na Mshikamano; kielelezo makini cha ushuhuda wa Imani katika matendo.