2013-01-30 14:44:13

FAO: kuna hatari ya kuzuka tena kwa Ugonjwa wa Mafua ya Ndege!


Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa, FAO linaonya kwamba, ikiwa kama Jumuiya ya Kimataifa haitachukua hatua za dharura, kuna uwezekano mkubwa kwamba, ikakumbwa tena na ugonjwa wa mafua ya ndege uliotikisa dunia kunako mwaka 2006.

Hii inatokana na ukweli kwamba, kwa sasa FAO inakabiliwa na ukata wa kuweza kupambana na ugonjwa wa Mafua ya Ndege kutokana na athari za myumbo wa uchumi kimataifa. Serikali zinapaswa kuwa makini ili kudhibiti dalili za kuibuka tena kwa ugonjwa wa Mafua ya ndege uliosababisha hasara kubwa, huko Asia na Mashariki ya Kati.

Hii ni changamoto kwa Jumuiya ya Kimataifa kuwekeza katika mikakati inayopania kudhibiti ugonjwa huu, ambao kati ya mwaka 2003 hadi mwaka 2011: kuku na bata millioni 400 walikufa na hivyo kusababisha hasara ya dolla za kimarekani billioni 20. Viongozi wa Jumuiya ya Kimataifa wasipoonesha utashi wa kisiasa, ugonjwa wa Mafua ya Ndege utalipuka tena!







All the contents on this site are copyrighted ©.