Maadhimisho ya Mwaka wa Imani iwe ni fursa makini ya kusimama kidete kulinda na kutetea
tunu msingi za maisha ya mwanadamu!
Baraza la Maaskofu Katoliki Thailand katika maadhimisho ya Mwaka wa Imani, linawaalika
waamini kumwilisha ndani mwao fadhila za kikristo zinazojikita katika haki, upendo
na mshikamano wa dhati, kama kielelezo makini cha kujibu changamoto mbali mbali zinazojitokeza
katika ulimwengu wa utandawazi. Hii ni nchi ambayo licha ya kuwa na waamini wa dini
na madhehebu mbali mbali, imeendelea kujivunia utajiri wa maisha ya kiroho pamoja
na utamaduni wa amani na utulivu, kila mtu akiheshimiwa na kuthaminiwa na Jamii husika.
Baraza la Maaskofu Katoliki Thailand linawaalika waamini na watu wenye mapenzi
mema, kusimama kidete kulinda na kutetea utu na heshima ya mwanadamu aliyeumbwa kwa
sura na mfano wa Mungu; walinde na kutunza mazingira, ili dunia iendelee kuwa ni mahali
paguri zaidi pa kuishi sanjari na kuondokana na ubinafsi unaoendelea kushika kasi
miongoni mwa Jamii, kwa watu kukumbatia mno malimwengu na kusahau Mapokeo na tamaduni
njema za nchi yao.
Kuna haja kwa Jamii kuendelea kuwekeza katika elimu ya utunzaji
bora wa mazingira, sanjari na kukuza utamaduni wa upendo na mshikamano wa dhati, mambo
ambayo yanaendelea kumong’onyoka siku hadi siku katika ulimwengu wa utandawazi. Kwenye
miji mikubwa, ubinafsi unaonekana kuwa kama ndio mtindo wamaisha, kila mtu anajitafuta
mwenyewe na wala maisha ya jirani yake, hayamgusi kamwe.
Ubinafsi unaanza
kukomaa, kiasi kwamba, ni vigumu kwa sasa kuweza kufanya mabadiliko ya dhati. Mwaka
wa Imani, iwe ni changamoto kwa waamini na watu wenye mapenzi mema, kuyatakatifuza
malimwengu, kwa kuwekeza katika fadhila za Kikristo.
Watu wamekuwa ni watumwa
wa matangazo ya biashara na mitandao ya mawasiliano ya Jamii, mambo yanayoleta athari
kubwa hata katika maisha ya familia. Watu wanatumia muda mrefu kuzungumza kwenye simu,
kuperuzi kwenye mitandao na pengine hata kukosa nafasi ya kuzungumza ndani ya familia,
hali ambayo inaweza kuleta madhara makubwa katika malezi na makuzi ya watoto pamoja
na mahusiano ndani ya Familia.
Maendeleo ya sayansi na teknolojia ya labari
yasaidie kukuza na kuimarisha tunu msingi za maisha ya kifamilia na kamwe yasiwe ni
kikwazo cha heshima, utu na maadili mema. Matumizi ya mitandao ya Jamii yamekuwa kwa
familia nyingi chanzo cha kinzani na mitigano; hatari kubwa inayoweza kuporomosha
misingi bora ya ndoa na maisha ya kifamilia.
Maadhimisho ya Mwaka wa Imani
yanayokwenda sanjari na kumbu kumbu ya Jubilee ya Miaka hamsini ya Mtaguso Mkuu wa
Pili wa Vatican iwe ni fursa kwa waamini na watu wenye mapenzi mema, kujichotea utajiri
mkubwa, uliobainishwa na Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican kuhusu: umuhimu
wa Liturujia katika maisha na utume wa Kanisa, Neno la Mungu, Nafasi na dhamana ya
waamini walei katika kuyatakatifuza malimwengu bila kusahau majadiliano ya kidini
na kiekumene, kama njia muafaka ya Uinjilishaji Mpya, iliyobainishwa na Mababa wa
Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican, ikatiliwa mkazo na Mababa wa Sinodi ya Maaskofu juu
ya Uinjilishaji Mpya.
Miaka ishirini tangu kuchapishwa kwa Katekisimu Mpya
ya Kanisa Katoliki, iwe ni fursa kwa waamini kufahamu kwa kina Imani ambayo Mama Kanisa
anaiungama, anaiadhimisha, anajitahidi kuimwilisha na kuisali. Waamini wajibidishe
kuyafahamu Mafundisho tanzu ya Kanisa bila kusahau umuhimu wa Mafundisho Jamii ya
Kanisa, kanuni na mwongozo kwa waamini walei katika mchakato unaopania kuyatakatifuza
malimwengu.
Mwaka wa Imani, wanasema Maaskofu, ujenge na kuimarisha Injili
ya Upendo inayomwilisha Imani katika matendo, kwa kuwasaidia maskini na wote wanaosukumizwa
pembezoni mwa Jamii, ili kila mtu aweze kutambua heshima na utu wake, kwani ameumbwa
kwa sura na mfano wa Mungu.
Kuna umati mkubwa wa wagonjwa, wazee, vijana na
watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi, bila kuwasahau wale ambao wanakabiliwa
kutolewa mimba kutokana na utamaduni wa kifo; wote hawa wana njaa na kiu ya Injili
ya Upendo. Ni mwaliko kwa waamini kuyatumia malimwengu kwa busara kwa ajili ya mafao
ya wengi na maendeleo endelevu ya binadamu, wawe mstari wa mbele kuyatakatifuza malimwengu,
kwa njia ya maisha yao adili na matakatifu.
Familia za Kikristo ziwe ni daraja
linalounganisha tunu msingi za maisha ya kifamilia, kiutu na kimaadili, kwa kutambua
kwamba, Familia ni shule ya kwanza ya maisha ya binadamu, kumbe wazazi wana wajibu
mkubwa katika malezi na majiundo ya watoto wao. Familia ni shule ya haki, amani na
upendo unaopaswa kujionesha katika Jamii; ziwe ni chachu ya ujenzi wa mshikamano wa
upendo na udugu, ili kweli amani iweze kutawala katika mioyo na maisha ya watu.