2013-01-29 08:39:57

Baraza la Maaskofu Katoliki Italia na changamoto wanazokabiliana nazo katika maisha na utume wa Kanisa


Kardinali Angelo Bagnasco, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Italia katika hotuba yake ya ufunguzi wa mkutano mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Italia, Jumatatu tarehe 28 Januari 2013 anasema kwamba, mkutano huu unafanyika wakati ambapo Maaskofu Katoliki Italia wanafanya hija ya kitume mjini Vatican sanjari na Maadhimisho ya Mwaka wa Imani.

Maaskofu wanamshukuru Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, kwa kutambua ushuhuda uliotolewa na Papa Paulo wa Sita na sasa anaweza kutangazwa kuwa Mwenyeheri.

Maaskofu wako katika hija ya matumaini inayowawajibisha kumtangaza Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu bila kikomo na kwamba, hii ndiyo hoja wanayotaka kuifanyia kazi katika maadhimisho ya Mwaka wa Imani, ili kuwasaidia watu wanaoogelea katika utupu wa jangwa na maisha ya kiroho na kimaadili kuonja ile furaha ya kuwa mfuasi wa Kristo, kama anavyohimiza Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita.

Idadi ya Wakristo waliouwawa kikatili sehemu mbali mbali za duniani kwa mwaka 2012 inatisha kutokana na kuibuka kwa watu wenye misimamo mikali ya kidini, utaifa pamoja na uchu wa madaraka kama ilivyotokea: Nigeria, Kenya, DRC na Mali. Kinzani za kikabila na kijamii ni kati ya mambo yanayoendelea kuvunja misingi ya haki, amani na utulivu.

Kardinali Bagnasco anasema kwamba, baa la njaa linaendelea kutesa mamillioni ya watu kuliko hata ilivyo kwa athari za myumbo wa uchumi kimataifa, changamoto ya kujenga na kuimarisha mshikamano wa upendo unaosimikwa katika kanuni ya auni. Deni kubwa la taifa na matumizi makubwa ya Serikali ni mambo ambayo yanapelekea ugumu wa maisha na umaskini miongoni mwa wananchi wengi wa Italia.

Hali hii imepelekea pia ongezeko la vijana wasiokuwa na fursa za ajira pamoja na umaskini wa kipato na kihali kwa familia nyingi nchini Italia. Ni wajibu wa wanasiasa kuibua mbinu mkakati utakaoiwezesha Jamii kukabiliana na hali ngumu ya maisha inayoendelea kukatisha tamaa pamoja na kukwamisha mchakato wa maendeleo. Sera na mikakati ya maendeleo haina budi kutoa kipaumbele cha kwanza kwa binadamu na mahitaji yake msingi: kiroho na kimwili.

Kanisa kwa upande wake, litaendelea kujikita katika mchakato wa Uinjilishaji Mpya, ili kuweza kukabiliana na changamoto mbali mbali zinazoibuliwa katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia, kwa kutangaza Injili ya Upendo; utunzaji bora wa mazingira pamoja na kutolea ushuhuda kweli za Kiinjili zinazobubujika kutoka katika Maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu.

Liturujia ya Kanisa iwe ni shule ya kusikiliza kwa makini Neno la Mungu pamoja na kukuza Ibada mbali mbali zinazorutubisha maisha ya kiroho. Yote haya yanaweza kutekelezwa barabara ikiwa kama Familia itakuwa imeshikamana kwa dhati na kwamba, msingi mkuu ni upendo wa dhati! Kanisa litaendelea kutekeleza wajibu na dhamana yake katika Jamii na wala halina mpango wa kuingilia masuala ya kisiasa, lakini, litaendelea kusimama kidete kulinda na kutetea haki msingi za binadamu, mafao ya wengi pamoja na maisha bora kwa wananchi wengi.

Ni mwaliko kwa wananchi pia kutekeleza wajibu wao wa kisiasa kwa kushiriki kikamilifu katika mchakato wa kupiga kura ili kuwapata viongozi bora watakaoliongoza taifa kwa uzalendo, hekima na unyofu wa moyo, daima wakitafuta mafao ya wengi na wala siasa lisiwe ni Jukwaa la kutafuta kujitajirisha! Zawadi ya maisha haina budi kulindwa na kutetewa tangu pale mtoto anapotungwa mimba hadi anapofikwa na mauti ya kawaida kadiri ya mpango wa Mungu.

Ni mwaliko kwa Jamii kujenga utamaduni wa uhai kama njia ya kukabiliana na athari za myumbo wa uchumi kimataifa na wala si kwa kukumbatia utamaduni wa kifo! Tunu bora za maisha ya Ndoa na Familia hazina budi kulindwa kama mhimili mkuu wa maisha ya Kijamii unaojengeka katika upendo wa dhati, kwani mahali ambapo kuna upendo wa kweli, anasema Kardinali Bagnasco, hapo Mungu yupo! Ndoa inajengeka katika uhusiano kati ya Bwana na Bibi na matunda ya ndoa ni watoto ambao wana haki ya kupata malezi ya wazazi wao. Maaskofu Katoliki Italia wanapinga ndoa za watu wa jinsia moja!







All the contents on this site are copyrighted ©.