2013-01-28 07:53:26

Mshikamano wa Kanisa na wote wanaoteseka Mashariki ya Kati kutokana na vita na kinzani za kijamii!


Patriaki Fouad Twal wa Yerusalem, katika kipindi hiki cha taabu, mateso na mahangaiko ya wananchi wengi wa Syria kutokana na vita na kinzani za kijamii zinazoendelea kujitokeza nchini humo ameamua kuwaandikia waamini na wahudumu wote kwa kutambua mchango wao katika kuwahudumia waathirika wa vita nchini Syria na kwamba, yuko pamoja nao kwa njia ya sala.
Uwepo wao ni kielelezo makini cha ushuhuda wa upendo na udugu miongoni mwa Jamiiiliyosambaratika kutoka na vita.
Anatambua na kuguswa na mahangaiko ya wananchi wa Syria wakati huu wanapoendelea kufanya hija ya Njia ya Msalaba, wakishiriki mateso ya Kristo yanayokoa; anapenda kutoa sala zake kwa wote waliotangulia mbele ya haki wakiwa na tumaini la ufufuko; wagonjwa wanaoteseka kutokana na kukosekana kwa huduma, wale wanaokimbia ili kusalimisha maisha yao bila kuwasahau wale ambao wameamua kubaki nchini mwao, licha ya mtutu wa bunduki kuendelea kurindima katika mitaa na viunga miji yao.
Haya ni mahangaiko na mateso ambayo Patriaki Twal ameyashuhudia mwenyewe wakati alipofanya hija yake ya kichungaji kule Mafraq, Kaskazini mwa Mto Yordani. Watu wenye mapenzi mema wanaendelea kujiuliza, Je, mateso na mahangaiko ya watu hawa yataendelea hadi lini? Jambo linalosikitisha ni kuona kwamba, katika taabu na mahangaiko haya, hawana lolote lile ambalo wanaweza kutekeleza ili kuokoa maisha ya watu na kusitisha vita, kinzani na mgogoro unaoendelea nchini Syria.
Patriaki Twal anasema, anapenda kuunganisha sauti yake na wapenda amani kutoka pande mbali mbali za dunia, kukazia umuhimu wa mshikamano wa upendo na udugu miongoni mwa wananchi wa Syria, kama anavyoendelea kukazia Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita. Kama viongozi wa Kanisa wanaungana na waamini wote ili kuombea amani ili watu waweze kusitisha kinzani na vita vinavyoendelea kusababisha maafa makubwa kwa watu wasiokuwa na hatia na badala yake, kuonesha ujasiri wa kuanzisha mchakato wa majadiliano ya kweli, ili hatimaye, amani, upendo na mshikamano kati ya watu viweze kushamiri katika mioyo yao!







All the contents on this site are copyrighted ©.