Baraza la Maaskofu Katoliki Italia, kuanzia tarehe 28 hadi tarehe 31 Januari 2013
linafanya mkutano wake, utakaojadili pamoja na mambo mengine kuhusu mabadiliko yaliyofanywa
na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, kuhusu Mashirika ya Misaada ya Kanisa
Katoliki kwa kuzingatia kwamba, huduma ya upendo ni sehemu ya asili na vinasaba vya
Mama Kanisa katika maisha na utume wake. Mkutano huu utakuwa chini ya Kardinali Angelo
Bagnasco, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Italia.
Maaskofu wanajadili na
hatimaye, kupitisha Angalisho la shughuli za kichungaji, kwa kutambua umuhimu wake
katika utume wa Kanisa unaojikita katika utajiri mkubwa wa Mama Kanisa kwa karne nyingi,
lakini, unaopaswa kuangaliwa kwa mapana kwa kusoma alama za nyakati mintarafu mahitaji
ya sasa.
Mkazo ni kuendelea kukazia umuhimu wa Katekesi kama njia makini ya
kurithisha Imani ya Kanisa kwa waamini wanaoendelea na hija ya maisha yao hapa duniani,
bila kusahau umuhimu wa majiundo makini na ya kina kwa Makatekista wanaopewa dhamana
ya ya kurithisha Imani ya Kanisa kwa Wakatekumeni na vijana wa kizazi kipya. Makatekista
wasipokuwa makini, Kanisa linaweza kujikuta likiwa na waamini hoi bin taabani, wasioweza
kukiri, kuadhimisha, kuiishi, kusali na kuimwilisha Imani yao katika matendo.