Maoni ya Wasomi kutoka Roma kuhusu Katiba Mpya ya Tanzania
Mchakato wa kukusanya maoni ya Katiba Mpya ya Tanzania unaendelea vyema, awamu ya
kwanza ilikuwa ni kuhamasisha na kukusanya maoni kutoka kwa watanzania mmoja mmoja.
Hatua ya pili imekuwa ni kukusanya maoni kwa makundi maalum. Yafuatayo ni baadhi ya
maoni yaliyotolewa na wanafunzi wanaosoma mjini Roma, kama sehemu ya mchango wao katika
kuandika Katiba Mpya ya Tanzania. 1. Kuhusu Mahakama ya Kadhi: Mahakama hii
ni ya kidini na inahusiana na utatuzi wa maswala ya kidini. Hivyo basi, kutokana na
kwamba Tanzania yetu tangu kupata uhuru wake inajukana kama nchi isiyo fuata misingi
ya dini yoyote, swala la Mahakama ya Kadhi isiingie kwenye katiba; mahakama iendelee
kubaki kama mmojawapo wa mihimili mikuu ya nchi inayo ratibu maswala ya dini husika,
bila kuihusisha Katiba ya nchi ambayo ni ya wananchi wote wafuasi wa dini fulani na
wasio fuata dini yoyote. Mahakama za kidini zisiingie katika katiba kwani Tanzania
haina dini. 2. Kuhusu Tanzania kujiunga na OIC Jumuiya ya Nchi za Kiislam OIC
ina malengo na itikadi zake zinazojikita hasa katika masuala ya kidini. Tanzania hadi
sasa haina dini yoyote rasmi ila ni wananchi wake wanao abudu kwenye dini na madhehebu
mbalimbali. Ikiwa kuna wananchi wanaotaka kujiunga na Jumuiya hii wapewe nafasi kama
watu binafsi na si kama nchi. Tanzania isijiunge na OIC kwa kuwa hii ni Jumuiya ya
Kidini. Suala la Tanzania kuwa na uhusiano wa kidiplomasia na Vatican halina uhusiano
wowote na madai ya baadhi ya watu kutaka Tanzania kujiunga na OIC. 3. Kuhusu mfumo
wa Elimu Kwakuwa Serikali inalo jukumu la kuhakikishia wananchi wake Elimu, mfumo
wa Elimu usiwe wa kidini badala yake uendelee kusimamiwa na serikali itakayokuwa madarakani.Mchango
wa dini mbalimbali katika sekta hii uendelee kuheshimiwa na kuthaminiwa, ila serikali
iliyoko madarakani ndiyo itoe taratibu na sheria (zisizoshikamana na dini yoyote)
zinazopaswa kufuatwa katika swala zima la utoaji Elimu. 4. Kuhusu uteuzi wa viongozi
wa serikali na wa mashirika ya kiserikali Uteuzi wa viongozi hawa uzingatie sifa
za anayeteuliwa na wala usifanyike kulingana na sera za kiundugu au kidini. Si kwa
sababu mteuliwa ni rafiki au ndugu wa Kiongozi fulani au ni muumini wa dini fulani,
basi anafaa kushika madaraka. Nyadhifa zitolewe kwa kuzingatia “Mastahili, sifa na
vigezo vinavyohitajika. 5. Kuhusu uchaguzi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano. Hadi
sasa watanzania tunajua kuwa bara na visiwani ni Taifa moja na kwamba hatuna tofauti
yoyote kama raia. Hivyo basi, kwakuwa Zanzibar na Tanzania bara ni nchi moja, Raisi
wa Jamhuri ya Muungano atoke upande wowote ule wa Muungano na kusiwepo utaratibu wa
kupata Rais kwa zamu kati ya Tanzania bara na Zanzibar. Utaratibu wa kupata Rais kwa
zamu kati ya pande hizo mbili unaweza ukawa hatari na kutishia zaidi usalama na amani
ya Taifa kwani inawezekana kutokea kwamba kusitokee aidha mgombea nafasi hiyo mahali
ambapo Rais alitakiwa kutokwa kadiri ya mfuno uliopo hadi sasa. Nafafanua: ikiwa
kwa mfano kwenye uchaguzi ujao Rais anapaswa kutokea Zanzibar au bara, na ikatokea
kwamba kwenye ukanda huo hakuna mgombea aliyejitokeza, au aliyejitokeza asipigiwe
kura, nini kitafanyika? Kumbe kipengele kinachosititza kuwa Rais achaguliwe kwa kuzingatia
bara na visiwani kingeweza kuangaliwa upya na kufanyiwa marekebisho ili Rais achaguliwe
kutoka eneo lolote la Tanzania. 6. Kuhusu utoaji mimba Utoaji mimba ni swala
linalohusu haki msingi za binadamu zinazoongozwa na dhamiri nyofu. Hakuna serikali
yoyote inayoweza kuingilia dhamira ya mwananchi. Kama vile ambavyo serikali haiwezi
kumchagulia mwananchi yeyote mwenza wa maisha, au kuwaamuru wananchi kuvaa mavazi
yaliyoshonwa kwa mtindo fulani au ya rangi fulani, hali kadhalika, serikali haipaswi
kujiingiza kwenye maswala ya kuratibu na kuhalalisha kisheria maswala yanayohusu
dhamira na hasa mauaji ya watu wasio kuwa na hatia! Jukumu la serikali ni kulinda
maisha na usalama wa raia wake wote na si kuratibu mauaji ya baadhi ya raia ambao
bado hawajazaliwa. Licha ya hilo, mila na desturi za kiafrika si mila za mauaji bali
ni mila zinazotetea uhai na kuulinda. Utoaji mimba ni utamaduni wa kifo usiopaswa
kukumbatiwa na mwanadamu yeyote na hasa chombo kinacho ratibu maisha ya wananchi kama
ilivyo Katiba ya nchi. Katiba ilinde haki za watoto ambao bado hawajazaliwa. 7.
Kuhusu ndoa za watu wa jinsia moja Serikali isitambue ndoa ya watu wa jinsia moja
na kuiweka katika Katiba ya nchi, kwa kuwa ni jambo linalo kwenda kinyume na maadili
ya kiutu na kijamii. Hivyo swala hili lisipate nafasi katika Katiba ya nchi. Kama
ilivyo hoja iliyopita, hata hii inayofuata inahusu dhamira ya mtu binafsi. Kama baadhi
ya wananchi wakiamua kuishi muunganiko (kwani haiwezi kuitwa ndoa) wa watu wa jinsia
moja, liwe ni chaguo lao binafsi, ila lisitambulike kikatiba! Katiba ya nchi izingatie
maadili na utu wema. 8. Uraia wa nchi mbili: Kuna haja kwa Katiba ya Tanzania
kusoma alama za nyakati kwa kuruhusu raia wake kuwa na fursa ya uraia wa nchi mbili
pale inapowezekana ili kuweza kufaidi matunda ya jasho la watanzania wanaoishi ughaibuni.