Tafakari ya Neno la Mungu, Jumapili ya Tatu ya Kipindi cha Mwaka C wa Kanisa
Ni mara nyingine tena katika utaratibu wa kawaida wa tafakari Neno la Mungu tunapokutana
katika mtandao kushirikishana tafakari ya Liturujia ya Neno la Mungu, Dominika ya
III ya mwaka C.
Katika tafakari
yetu tunamwona Mtume Paulo akiendelea kukazia fundisho lake la kuwa sisi sote chimbuko
letu ni Kristo. Tuko tofauti kwa maana ya kuwa wengine ni Wayahudi, wengine ni Wayunani
na hata wengine kwa sababu ya dhuluma wamekuwa watumwa. Lakini anasema, akisha kuja
Kristo hakuna tena matabaka haya bali umoja kamili katika mwili mmoja ulio na viungo
vingi.
Anatangaza uzuri wa utofauti ulio katika kufaidiana. Anajiuliza, hivi
mwili wote ungekuwa jicho, kusikia kungetokeaje? Basi, kujivuna katika maisha ya kila
siku kwa sababu ya mali au uwezo wa akili au kazi niliyonayo ni ukosefu wa maarifa
na ustadi katika kufikiri. Kumbe udhanifu yakwamba wengine ni dhaifu ni chimbuko la
mafarakano ambayo tunapaswa kuyaepuka kabisa.
Hata hivyo yafaa kukumbuka kuwa
Kristo ameweka makundi maalumu ili Neno lake lisonge mbele. Mtume Paulo anasema wa
kwanza ni Mitume ambao mahalifa wao ni Maaskofu, hawa ni nguzo za imani, yafaa kuwasikiliza
na kushika mafundisho yao ambayo ni mafundisho ya Bwana. Wanafuata manabii na Walimu
ambao hutangaza ujumbe wa Mungu na hatimaye miujiza, karama za kuponya na kunena lugha
mbalimbali.
Katika Injili ya leo Mwinjili Luka anaanza Injili yake akionesha
namna alivyoweza kuandika Injili, mbinu alizotumia kupata uhakika wa mambo, na tunapata
kuona jina la mtu ambaye Injili inaelekezwa kwake yaani Teofilo Mtukufu. Jina Teofilo
ni jina la Kigriki lenye kumaanisha “yule anayempenda Mungu”. Katika hili mara moja
twaweza pia kufikiri toka jina hili kuwa Luka anaelekeza Injili yake kwa wale wanaompenda
Mungu, wanaofanya utafiti wa kiroho na kichungaji kumjua Mungu. Watu hawa ni pamoja
sisi taifa lake.
Bwana yuko Nazareti, amerudi nyumbani na siku ya Sabato
anaingia katika Sinagogi na anasoma sehemu ya chuo cha Nabii Isaya, isemayo Roho wa
Bwana yu juu yangu amenipaka mafuta kuwahubiri maskini habari njema. Kisha kuweka
chini chuo cha Isaya anatangaza tena mara ya pili kuwa sasa maneno haya yamekamilika
katika yeye.
Bwana anajisalimisha kwa Roho wa Mungu ili aweze kufanya kazi
ya kuokoa walio katika mashaka na matatizo mbali mbali ya maisha kama vile utumwa
wa kiroho na kimwili na wanaoteswa kwa sababu ya imani yao. Kwa sababu daima Bwana
wetu Yesu Kristo ametimiza kazi yake akimtegemea Baba yake tunaweza kusema bila kusahau
kuwa yeye ndiye Mungu, ndiye Teofilo wa kweli ambaye Mt. Luka anaelekeza Injili yake.
Mpendwa, ni kwa namna gani nasi twaweza kushiriki kazi ya Teofilo kwa ajili
ya taifa la Mungu? Twaweza kuishi ule upendo ambao Mungu anatuonjesha kila siku ya
maisha yetu kwa njia ya Neno lake? Je, twatambua kuwa Kristo ni mjumbe wa Mungu wa
Agano Jipya na ambaye kwa kutaka kusema nasi kwa uhakika amejifanya mtu na ni mwaminifu
kwa Baba yake na hivi sisi tukialikwa kumfuata kila siku ya maisha yetu?
Tunaalikwa
kila siku kutambua kuwa kumpenda Mungu ni kumtambua Kristo aliyefanyika mwili na akashiriki
maisha yetu. Ni kukazia macho yetu kwake kama tulivyosikia katika Injili “waliokuwa
katika Sinagogi wakamkazia macho” Bwana anawaonesha uhalisia wake yaani mtangazaji
wa uhuru! Sisi Je, uhalisia wetu twautambua?
Tunapaswa kurudi katika ubatizo
wetu na kutambua kuwa tumekuwa makuhani, wafalme na manabii! Wajibu wa vyeo hivi unaturudisha
palepale kwa Bwana anapojionesha uhalisia wake, kuondoa dhuluma katika maisha ya watu,
kwamba tunapaswa kutenda kama Bwana alivyotenda na anavyotaka daima.
Tunapomalizia
tafakari hii tunarudi katika somo la kwanza tunapowaona Waisraeli wakirudi toka utumwani,
Nabii Nehemia anahadithia jinsi walivyosikiliza Torati na kutoa machozi. Ndiyo kusema
Neno la Bwana liliwaletea furaha mpaka wanafikia machozi ya furaha kama bibi arusi
atoavyo machozi anapoenda kuolewa. Ndiyo kusema Neno la Mungu limewaingia na kulisikiliza
kwa makini.
Tunaweza kusema Wana wa Israeli wanaporudi wanafanya Agano na
Mungu na wanahaidi kumhimidi Mungu katika maisha yao. Tunaona Ezra analeta Torati
mbele ya kusanyiko la watu, Wake kwa Wanaume anasimama juu ya Mimbari na anatangaza
ukuu wa MUNGU na kumhimidi Bwana. Watu wanaitika na kusema amina, amina na kuinua
mikono yao na kisha kuinamisha vichwa vyao na kumsujudu Bwana kifudifudi.
Naye
Nehemia alikuwa mmoja wa waliowafundisha watu na kuwaambia watu wote kuwa siku hii
ni takatifu kwa Bwana, msilie kamwe, maana walilia waliposikia maneno ya Torati. Kuleni
na kunywa kilichonona na kisha mpelekeeni yule asiyewekewa, siku hii ni takatifu na
furaha ya Bwana ni nguvu zenu. Kumbe baada ya kuelewa Neno la Mungu na kutoa machozi
ya furaha kadiri ya Nabii tunapaswa kwenda kutangaza habari njema. Bwana katika Agano
Jipya anatutuma akisema Enendeni duniani kote mkatangaze habari njema. Mt. 28:19-20.
Neno
la Mungu ni taa ya maisha yangu uwe ndiyo wimbo wako wa kila siku lakini hasa kuliweka
katika matendo ukilitangaza kwa mataifa. Tumsifu Yesu Kristo.
Tafakari hii
imeletwa kwako na Padre Richard Tiganya, C.PP.S.