2013-01-25 15:26:54

Jumapili, Siku ya Dunia ya wagonjwa wa Ukoma.


Jumapli ya wiki hii 27 Januari, itakuwa ni adhimisho la 60 la Siku ya dunia kwa ajili ya maradhi ya Ukoma, maradhi ya tangu kale yanayoendelea kutesa watu duniani. Wagonjwa wanao tengwa na kudharirishwa na hali ngumu za umaskini, kutokana na hali yao.
Kwa ajili hii, Rais wa Baraza la Kipapa kwa ajili ya Kazi za Kichungaji kwa Wahudumu wa Afya, Askofu Mkuu Zygmunt Zimowiski, ametoa ujumbe kwa ajili ya maadhimisho haya akisema ni Maadhimisho ya Wakristo wote, na kuomba misaada kwa watu wenye mapenzi mema, na kukuza dhamira zao katika kushirikiana na wagonjwa wa maradhi haya ya hatari na familia zao, na lengo la kukuza upya kasi ya kuwaunganisha na jamii.
Kwa mujibu wa takwimu za WHO za 2011, jumla ya watu 220,000 wakiwa ni wanaume, wanawake na watoto wanaishi na vijidudu vinavyosababisha ukoma, wengi wao wametambuliwa wakati ugonjwa umefika katika kiwango cha hali ya juu.
Askofu Mkuu Zimowski ameyataja maradhi haya kuwa ni kati ya mijeledi halisi dhidi ya binadamu, katika baadhi ya maeneo ya dunia, yanayohitaji ushirikiano wa Kimataifa katika utoaji wa kipaumbele kwa ajili ya kukabiliana nayo kama ilivyokuwa katika maradhi mengine sugu homa dengue, malale, kichocho na upofu.
Na katika mwanga wa Mwaka wa imani, juhudi zaidi za kidharura zinatakiwa kuchukuliwa na hasa Wakatoliki, katika kutimiza wajibu wao wa kuhudumia wahitaji, kama Yesumwwenyewe alivyoagiza, nendeni mkapozeni wagonjwa , fufueni wafu , takaseni wenye ukoma, toeni pepo, mmpewa bure toeni bure.
Askofu Mkuu Zimowski ameeleza na kutoa upya mwaliko katika maadhimisho haya ya 60 ya Siku ya Dunia ya mapambano dhidi ya ukoma, pia kama nafasi mpya ya kuimarisha huduma ya upendo katika jamii, kw akufuata mfano wa Msamaria Mwema, anayetajwa katika Injili.








All the contents on this site are copyrighted ©.