Hakikisheni kwamba, uchaguzi mkuu nchini Kenya hapo tarehe 4 Machi 2013 unakuwa huru
na wa haki!
Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya, linaitaka Tume Huru ya Uchaguzi nchini Kenya, kuhakikisha
kwamba, inasimamia uchaguzi mkuu uliopangwa kufanyika nchini humo tarehe 4 Machi 2013
unakuwa huru na wa haki. Maaskofu katika tamko lao lililotiwa sahihi na Kardinali
John Njue, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya, wanasema, wamesikitishwa na
vitendo vya baadhi ya wanasiasa kuanzisha vurugu na uvunjifu wa amani wakati wa kupitisha
majina ya wagombea wa vyama vyao hivi karibuni.
Hii ni changamoto kwa wanasiasa
nchini Kenya kuhakikisha kwamba, wanazingatia utawala wa sheria na demokrasia. Bado
kuna wanasiasa ambao wamejikita katika utoaji rushwa, vurugu, ubinafsi na upendeleo,
mambo ambayo yanadhalilisha haki msingi za binadamu, demokrasia na utawala bora nchini
Kenya. Wananchi wa Kenya wanapaswa kubadilika na kukumbatia mwelekeo mpya katika utekelezaji
wa demokrasia na utawala bora nchini humo.
Kwa sasa kuna taarifa zinazoonesha
vitendo ambavyo vinatishia amani na usalama wa raia, kinyume kabisa na matarajio yalioneshwa
na wananchi wa Kenya katika: Katiba Mpya, Tume huru ya Uchaguzi, Mwongozo Mpya wa
Vyama vya Siasa na Marekebisho makubwa yaliyofanywa katika Mahakama.
Inasikitisha
kuona kwamba, wanasiasa ambao kwa siku kadhaa wamekuwa wakihubiri siasa ya demokrasia,
utawala bora na sheria, sasa wamekuwa wa kwanza katika kuvunja misingi hii, kiasi
cha kutishia amani na utulivu wakati wa uchaguzi mkuu hapo tarehe 4 Machi 2013. Maaskofu
wanawataka wanasiasa na vyombo vya sheria, ulinzi na usalama kuhakikisha kwamba, vinajenga
mazingira ambayo yatahakikisha kwamba, uchaguzi uliopangwa kufanyika nchini humo unazingatia:
uhuru, ukweli, uwazi na amani.